Zaburi 44

Kuomba Ulinzi Wa Mungu

(Kwa Mwimbishaji: Utenzi Wa Wana Wa Kora)

1 Ee Mungu, tumesikia kwa masikio yetu,

baba zetu wametueleza

yale uliyotenda katika siku zao,

siku za kale.

2 Kwa mkono wako uliwafukuza mataifa katika nchi hii

na ukawapanda baba zetu,

uliangamiza mataifa

na kuwastawisha baba zetu.

3 Sio kwa upanga wao waliipata nchi,

wala si mkono wao uliwapatia ushindi;

ilikuwa ni kitanga cha mkono wako wa kuume,

na nuru ya uso wako,

kwa kuwa uliwapenda.

4 Wewe ni mfalme wangu na Mungu wangu,

unayeamuru ushindi kwa Yakobo.

5 Kwa uwezo wako tunawasukuma nyuma watesi wetu;

kwa jina lako tunawakanyaga adui zetu.

6 Siutumaini upinde wangu,

upanga wangu hauniletei ushindi;

7 bali wewe unatupa ushindi juu ya adui zetu,

unawaaibisha watesi wetu.

8 Katika Mungu wetu tunajivuna mchana kutwa,

nasi tutalisifu jina lako milele.

9 Lakini sasa umetukataa na kutudhili,

wala huendi tena na jeshi letu.

10 Umetufanya turudi nyuma mbele ya adui,

nao watesi wetu wametuteka nyara.

11 Umetuacha tutafunwe kama kondoo

na umetutawanya katika mataifa.

12 Umewauza watu wako kwa fedha kidogo,

wala hukupata faida yo yote kwa mauzo yao.

13 Umetufanya lawama kwa jirani zetu,

dharau na dhihaka kwa wale wanaotuzunguka.

14 Umetufanya kuwa mithali miongoni mwa mataifa,

mataifa hutikisa vichwa vyao.

15 Fedheha yangu iko mbele yangu mchana kutwa,

na uso wangu umejaa aibu tele,

16 kwa ajili ya dhihaka ya wale wanaonilaumu na kunitukana,

kwa sababu ya adui,

ambaye anatamani kulipiza kisasi.

17 Hayo yote yametutokea,

ingawa tulikuwa hatujakusahau

wala hatujaenda kinyume na Agano lako.

18 Mioyo yetu ilikuwa haijarudi nyuma;

lakini nyayo zetu zilikuwa hazijaiacha njia yako.

19 Lakini ulituponda na kutufanya makao ya mbweha

na ukatufunika kwa giza nene.

20 Kama tungalikuwa tumelisahau jina la Mungu wetu

au kunyoshea mikono yetu kwa mungu mgeni,

21 je, Mungu hangaligundua hili,

kwa kuwa anazijua siri za moyo?

22 Hata hivyo kwa ajili yako tunakabiliwa na kifo mchana kutwa;

tunahesabiwa kama kondoo wa kuchinjwa.

23 Amka, EeBwana! Kwa nini unalala?

Zinduka! Usitukatae milele.

24 Kwa nini unauficha uso wako

na kusahau taabu na mateso yetu?

25 Tumeshushwa hadi mavumbini,

miili yetu imegandamana na ardhi.

26 Inuka na utusaidie,

utukomboe kwa sababu ya upendo wako usio na mwisho.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/PSA/44-54b75441df84580e0380dbf22b6a37c2.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

8 − 8 =