Isaya 37

Kuokolewa Kwa Yerusalemu Kunatabiriwa

1 Wakati Mfalme Hezekia aliposikia hili, alirarua nguo zake na kuvaa nguo ya gunia, naye akaenda hekaluni mwaBwana.

2 Akawatuma Eliakimu msimamizi wa jumba la kifalme, Shebna katibu na makuhani viongozi, wote wakiwa wamevaa nguo ya gunia, waende kwa nabii Isaya mwana wa Amozi.

3 Wakamwambia, “Hili ndilo asemalo Hezekia: Siku hii ni siku ya dhiki, ya kukaripiwa na ya aibu, kama vile wakati watoto wanapofikia karibu kuzaliwa na kumbe hakuna nguvu ya kuwazaa.

4 YamkiniBwana, Mungu wako atayasikia maneno ya Amirijeshi, ambaye bwana wake, mfalme wa Ashuru, amemtuma kumdhihaki Mungu aliye hai, tena kwamba atamkemea kwa maneno ambayoBwana, Mungu wako ameyasikia. Kwa hiyo omba kwa ajili ya mabaki ambao bado wako hai.”

5 Watumishi wa Mfalme Hezekia walipomjia Isaya,

6 Isaya akawaambia, “Mwambieni bwana wenu, ‘Hili ndilo asemaloBwana: Usiogope kwa ajili ya yale uliyoyasikia, yale maneno ambayo kwayo watumishi wa mfalme wa Ashuru wamenitukana mimi.

7 Sikiliza! Nitatia roho ndani yake ili kwamba atakaposikia taarifa fulani, atarudi katika nchi yake mwenyewe, nami huko nitafanya auawe kwa upanga.’ ”

8 Amirijeshi aliposikia kwamba mfalme wa Ashuru ameondoka Lakishi, alirudi akamkuta mfalme anapigana dhidi ya Libna.

9 Basi Senakeribu akapata taarifa kwamba Tirhaka, Mkushi mfalme wa Misri, alikuwa anatoka kupigana dhidi yake. Aliposikia jambo hili akatuma wajumbe kwa Hezekia kwa neno hili:

10 “Mwambieni Hezekia mfalme wa Yuda: Usikubali Mungu unayemtumainia akudanganye wakati anaposema, ‘Yerusalemu haitatiwa mikononi mwa mfalme wa Ashuru.’

11 Hakika umesikia yale ambayo wafalme wa Ashuru wametenda kwa nchi zote, wakiwaangamiza kabisa. Je, wewe utaokolewa?

12 Je, miungu ya yale mataifa ambayo yaliangamizwa na baba zangu iliwaokoa, miungu ya Gozani, Harani, Resefu na watu wa Edeni ambao walikuwa katika Telasari?

13 Yuko wapi mfalme wa Hamathi, mfalme wa Arpadi, mfalme wa mji wa Sefarvaimu, au wa Hena au wa Iva?”

Maombi Ya Hezekia

14 Hezekia alipokea barua kutoka kwa wale wajumbe naye akaisoma. Kisha akapanda hekaluni mwaBwanaakaikunjua mbele zaBwana.

15 Naye Hezekia akamwombaBwanaakisema:

16 “EeBwanaMwenye Nguvu Zote, Mungu wa Israeli, uketiye juu ya kiti cha enzi kati ya makerubi, wewe peke yako ndiwe Mungu juu ya falme zote za dunia. Umeumba mbingu na nchi.

17 EeBwana, tega sikio na usikie, fungua macho yako, EeBwana, uone, sikiliza maneno yote Senakeribu aliyotuma ili kumtukana Mungu aliye hai.

18 “Ni kweli, EeBwanakwamba wafalme wa Waashuru wameyaangamiza mataifa haya yote pamoja na nchi zao.

19 Wameitupa miungu yao kwenye moto na kuiteketeza, kwani haikuwa miungu bali ni miti na mawe tu, iliyotengenezwa kwa mikono ya wanadamu.

20 EeBwana, Mungu wetu, sasa utuokoe toka mkononi mwake ili kwamba falme zote za dunia zipate kujua ya kwamba wewe peke yako, EeBwana, ndiwe Mungu.”

Kuanguka Kwa Senakeribu

21 Kisha Isaya mwana wa Amozi akapeleka ujumbe kwa Hezekia akisema: “Hili ndilo asemaloBwana, Mungu wa Israeli: Kwa sababu umeniomba kuhusu Senakeribu mfalme wa Ashuru,

22 hili ndilo neno ambaloBwanaamesema dhidi yake:

“Bikira binti Sayuni

anakudharau na kukudhihaki.

Binti Yerusalemu

anatikisa kichwa chake ukimbiapo.

23 Wewe ni nani uliyenitukana na kunikufuru?

Ni dhidi ya nani umeinua sauti yako

na kuinua macho yako kwa kiburi?

Ni dhidi ya yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli!

24 Kwa kutumia wajumbe wako

umelundika matukano juu ya Bwana.

Nawe umesema,

‘Kwa magari yangu mengi ya vita,

nimekwea kwenye vilele vya milima,

kwenye vilele vya juu kabisa vya Lebanoni.

Nimeikata mierezi yake iliyo mirefu kuliko yote,

misonobari yake iliyo bora sana.

Nimefika mahali pake palipoinuka palipo mbali sana,

katika msitu wake ulio mzuri kuliko yote.

25 Nimechimba visima katika nchi za kigeni

na kuyanywa maji huko.

Kwa nyayo za miguu yangu

nimevikausha vijito vyote vya Misri.’

26 “Je, hukusikia?

Zamani sana nililisimika.

Katika siku za zamani nililipanga,

na sasa nimelitimiza,

kwamba umeigeuza miji yenye maboma

kuwa malundo ya mawe.

27 Watu wa miji hiyo, wakiwa wameishiwa nguvu,

wanatiwa hofu na kuaibishwa.

Wao ni kama mimea katika shamba,

kama machipukizi mororo ya kijani,

kama majani yachipuayo juu ya paa la nyumba,

ambayo hukauka kabla ya kukua.

28 “Lakini ninajua mahali ukaapo,

kutoka kwako na kuingia kwako

na jinsi unavyoghadhibika dhidi yangu.

29 Kwa sababu unaghadhibika na ufedhuli dhidi yangu

na kwa sababu ufidhuli wako umefika masikioni mwangu,

nitaweka ndoana yangu kwenye pua yako

na hatamu yangu kinywani mwako,

nami nitakufanya urudi kwa njia uliyoijia.

30 “Hii itakuwa ndiyo ishara kwako, Ee Hezekia:

“Mwaka huu utakula kile kiotacho chenyewe

na mwaka wa pili utakula kutoka machipukizi yake.

Lakini katika mwaka wa tatu panda na kuvuna,

panda shamba la mizabibu

na ule matunda yake.

31 Mara nyingine tena mabaki ya nyumba ya Yuda

yataeneza mizizi chini na kuzaa matunda.

32 Kwa kuwa kutoka Yerusalemu yatatokea mabaki,

na kutoka Mlima Sayuni kikosi cha wale walionusurika.

Wivu waBwanaMwenye Nguvu Zote,

utatimiza hili.

33 “Kwa hiyo hili ndiloBwanaasemalo kuhusu mfalme wa Ashuru:

“Hataingia katika mji huu

wala hatapiga mshale hapa.

Hatakuja mbele yake na ngao

wala kupanga majeshi kuzunguka dhidi yake.

34 Kwa njia ile aliyoijia ndiyo atakayorudi kwayo;

hataingia katika mji huu,”

asemaBwana.

35 “Nitaulinda mji huu na kuuokoa,

kwa ajili yangu mwenyewe

na kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu!”

36 Ndipo malaika waBwanaakaondoka na kuwaua watu mia themanini na tano elfu katika kambi ya Waashuru. Watu walipoamka asubuhi yake, wote huko walikuwa maiti!

37 Kwa hiyo Senakeribu mfalme wa Ashuru akavunja kambi na kuondoka. Alirudi Ninawi na kukaa huko.

38 Siku moja, alipokuwa akiabudu katika hekalu la mungu wake Nisroki, wanawe Adrameleki na Shareza walimwua kwa upanga, nao wakakimbilia nchi ya Ararati. Naye Esar-Hadoni mwanawe akawa mfalme badala yake.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/ISA/37-d4d0dc7573517cdf553c345d2888fe39.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

one + 6 =