2 Wakorintho 13

Maonyo Ya Mwisho

1 Hii ndiyo mara ya tatu nikija kwenu. “Shtaka lo lote lazima lithibitishwe na mashahidi wawili au watatu.”

2 Nimekwisha kuwaonya nilipokuwa pamoja nanyi mara ya pili. Sasa narudia wakati sipo, kwamba nikija tena sitawahurumia wale waliokuwa wametenda dhambi hapo awali na wengine wote,

3 kwa kuwa mnadai uthibitisho kwamba Kristo anazungumza kwa kunitumia mimi. Yeye si dhaifu katika kushughulika nanyi, bali ana nguvu katikati yenu.

4 Kwa kuwa alisulibiwa katika udhaifu, lakini anaishi kwa nguvu za Mungu. Vivyo hivyo, sisi tu dhaifu katika yeye, lakini katika kuwashughulikia ninyi tutaishi pamoja naye kwa nguvu za Mungu.

5 Jichunguzeni wenyewe mwone kama mnaishi katika imani. Jipimeni wenyewe. Je, hamtambui ya kuwa Yesu Kristo yumo ndani yenu? Kama sivyo, basi, mmeshindwa kufikia kipimo hicho!

6 Natumaini mtaona kuwa sisi hatukushindwa.

7 Lakini tunamwomba Mungu msije mkatenda kosa lo lote, si ili sisi tuonekane kuwa tumeshinda hilo jaribio, bali ili ninyi mtende lililo haki, hata kama tutaonekana kuwa tumeshindwa.

8 Kwa maana hatuwezi kufanya lo lote kinyume na kweli, bali kuithibitisha kweli tu.

9 Tunafurahi wakati wo wote sisi tunapokuwa dhaifu, lakini ninyi mkawa na nguvu. Nayo maombi yetu ni kwamba mpate kuwa wakamilifu.

10 Hii ndiyo sababu ninawaandikia mambo haya wakati sipo, ili nikija nisiwe mkali katika kutumia mamlaka yangu, mamlaka Bwana aliyonipa ya kuwajenga ninyi wala si ya kuwabomoa.

Salamu Za Mwisho

11 Hatimaye, ndugu zangu, kwaherini. Iweni wakamilifu, mkafarijike, nieni pamoja, kaeni kwa amani, naye Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi.

12 Salimianeni ninyi kwa ninyi kwa busu takatifu.

13 Watakatifu wote wanawasalimu.

14 Neema ya Bwana Yesu Kristo na upendo wa Mungu na ushirika wa Roho Mtakatifu ukae nanyi nyote. Amen.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/2CO/13-22f9965197caab0b1b9f7bf9f1d3b32e.mp3?version_id=1627—

1 Wakorintho 1

Salamu

1 Paulo, aliyeitwa kwa mapenzi ya Mungu kuwa mtume wa Yesu Kristo na Sosthene ndugu yetu.

2 Kwa Kanisa la Mungu lililoko Korintho, kwa wale waliotakaswa katika Kristo Yesu, walioitwa kuwa watakatifu, pamoja na wale wote ambao kila mahali wanaliitia Jina la Kristo Yesu Bwana wetu, aliye Bwana wao na wetu pia:

3 Neema na amani itokayo kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo iwe nanyi.

Shukrani

4 Ninamshukuru Mungu siku zote kwa ajili yenu kwa sababu ya neema yake mliyopewa katika Kristo Yesu.

5 Kwa kuwa katika Kristo mmetajirishwa kwa kila hali, katika kusema kwenu na katika maarifa yenu yote,

6 kwa sababu ushuhuda wetu kumhusu Yesu ulithibitishwa ndani yenu.

7 Kwa hiyo hamkupungukiwa na karama yo yote ya kiroho wakati mnangoja kwa shauku kudhihirishwa kwa Bwana wetu Yesu Kristo.

8 Yeye atawafanya imara mpaka mwisho, ili msiwe na hatia siku ile ya Bwana wetu Yesu Kristo.

9 Mungu ni mwaminifu, ambaye mmeitwa naye ili mwe na ushirika na Mwanawe Yesu Kristo, Bwana wetu.

Mgawanyiko Ndani Ya Kanisa

10 Nawasihi ndugu zangu, katika Jina la Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba mpatane nia zenu ninyi kwa ninyi, ili pasiwepo na matengano katikati yenu na kwamba mwe na umoja kikamilifu katika nia na katika kusudi.

11 Kwa maana ndugu zangu, nimepata habari kutoka kwa baadhi ya watu wa nyumbani mwa Kloe kwamba kuna magomvi katikati yenu.

12 Maana yangu ni kwamba: Mmoja wenu husema, “Mimi ni wa Paulo”; mwingine, “Mimi ni wa Apolo”; mwingine, “Mimi ni wa Kefa”; na mwingine, “Mimi ni wa Kristo.”

13 Je, Kristo amegawanyika? Je, Paulo ndiye aliyesulibishwa kwa ajili yenu? Je, mlibatizwa kwa jina la Paulo?

14 Namshukuru Mungu kwamba sikumbatiza mtu ye yote miongoni mwenu isipokuwa Krispo na Gayo.

15 Kwa hiyo hakuna mtu ye yote miongoni mwenu anayeweza kusema kwamba alibatizwa kwa Jina langu.

16 (Naam, niliwabatiza pia watu wa nyumbani mwa Stefana. Lakini zaidi ya hao sijui kama nilimbatiza mtu mwingine ye yote.)

17 Kwa maana Kristo hakunituma ili kubatiza bali kuhubiri Injili na nifanye hivyo si kwa kutumia maneno ya hekima ya kibinadamu ya kushawishi, ili msalaba wa Kristo usije ukakosa nguvu yake.

Kristo Hekima Na Nguvu Ya Mungu

18 Kwa maana ujumbe wa msalaba kwa wale wanaopotea ni upuzi, lakini kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu.

19 Kwa maana imeandikwa:

“Nitaiharibu hekima ya wenye hekima,

na kuzibatilisha akili za wenye akili.”

20 Yuko wapi mwenye hekima? Yuko wapi msomi? Yuko wapi mwanafalsafa wa nyakati hizi? Je, Mungu hakufanya hekima ya ulimwengu huu kuwa upumbavu?

21 Kwa kuwa katika hekima ya Mungu, ulimwengu kwa hekima yake haukumjua yeye, ilimpendeza Mungu kuwaokoa wale waaminio kwa upuzi wa lile neno lililohubiriwa.

22 Wayahudi wanataka miujiza na Wayunani wanatafuta hekima,

23 lakini sisi tunamhubiri Kristo aliyesulibiwa, ambaye kwa Wayahudi ni kitu cha kukwaza na kwa Wayunani ni upuzi.

24 Lakini kwa wale ambao Mungu amewaita, Wayahudi pia Wayunani, Kristo ni nguvu na hekima ya Mungu.

25 Kwa maana upumbavu wa Mungu una hekima zaidi kuliko hekima ya wanadamu, nao udhaifu wa Mungu una nguvu kuliko nguvu ya wanadamu.

26 Ndugu zangu, kumbukeni mlivyokuwa mlipoitwa. Kwa kipimo cha kibinadamu, si wengi wenu mliokuwa na hekima. Si wengi mliokuwa na nguvu, si wengi mliozaliwa katika jamaa zenye vyeo.

27 Lakini Mungu alivichagua vitu vipumbavu vya ulimwengu ili aviaibishe vyenye hekima, Mungu alivichagua vitu dhaifu vya ulimwengu ili aviaibishe vyenye nguvu.

28 Alivichagua vitu vya chini na vinavyodharauliwa vya dunia hii, vitu ambavyo haviko, ili avibatilishe vile vilivyoko,

29 ili mtu ye yote asijisifu mbele za Mungu.

30 Mungu ndiye chanzo cha uzima wenu katika Kristo Yesu, aliyefanyika kwetu hekima itokayo kwa Mungu na haki na utakaso na ukombozi,

31 ili kama ilivyoandikwa: “Yeye ajisifuye na ajisifu katika Bwana.”

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/1CO/1-5f6dbac1c09057b91f50cfd908d59939.mp3?version_id=1627—

1 Wakorintho 2

Kumtangaza Kristo Aliyesulibiwa

1 Ndugu zangu nilipokuja kwenu, sikuja na maneno ya ushawishi wala hekima ya hali ya juu nilipowahubiria siri ya Mungu.

2 Kwa kuwa niliamua kutokujua kitu cho chote wakati nikiwa nanyi isipokuwa Yesu Kristo, naye amesulibiwa msalabani.

3 Mimi nilikuja kwenu nikiwa dhaifu na mwenye hofu na kwa kutetemeka sana.

4 Kuhubiri kwangu na ujumbe wangu haukuwa kwa hekima na maneno ya kuwashawishi watu, bali kwa madhihirisho ya nguvu za Roho Mtakatifu

5 ili imani yenu isiwe imejengwa katika hekima ya wanadamu bali katika nguvu za Mungu.

Hekima Ya Kweli Itokayo Kwa Mungu

6 Lakini miongoni mwa watu waliokomaa twanena hekima, wala si hekima ya ulimwengu huu au ya watawala wa dunia hii wanaobatilika.

7 Sisi tunanena hekima ya Mungu ambayo ni siri, tena iliyofichika kwa wanadamu, ambayo Mungu aliikusudia kabla ya ulimwengu kuwepo, kwa ajili ya utukufu wetu.

8 Hakuna hata mtawala mmoja wa nyakati zetu aliyeelewa jambo hili. Kwa maana kama wangelielewa, wasingemsulibisha Bwana wa utukufu.

9 Lakini ni kama ilivyoandikwa:

“Lile jambo ambalo jicho halijapata kuona,

sikio halijapata kusikia,

wala halikuingia moyoni,

lile ambalo Mungu aliwaandalia

wale wampendao”:

10 Lakini mambo haya Mungu ametufunulia kwa njia ya Roho wake.

Roho huchunguza kila kitu, hata mambo ya ndani sana ya Mungu.

11 Kwa maana ni nani anayejua mawazo ya mtu isipokuwa roho iliyo ndani ya huyo mtu? Vivyo hivyo hakuna mtu ajuaye mawazo ya Mungu isipokuwa Roho wa Mungu.

12 Basi hatukupokea roho ya dunia bali Roho yule atokaye kwa Mungu, ili tuweze kuelewa kile kipawa ambacho Mungu ametupatia bure.

13 Haya ndiyo tusemayo, si kwa maneno tuliyofundishwa kwa hekima ya wanadamu bali kwa maneno tuliyofundishwa na Roho, tukifafanua kweli za kiroho kwa wale watu wa kiroho.

14 Mtu ambaye hana Roho wa Mungu hawezi kupokea mambo yatokayo kwa Roho wa Mungu, kwa kuwa ni upuzi kwake, naye hawezi kuyaelewa kwa sababu hayo yanaeleweka tu kwa jinsi ya rohoni.

15 Mtu wa kiroho hutambua mambo yote, lakini yeye mwenyewe hatambuliwi na mtu ye yote.

16 “Kwa maana ni nani aliyejua nia ya Bwana

ili apate kumfundisha?”

Lakini sisi tunayo nia ya Kristo.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/1CO/2-019a5eb9aac018c4124ae9e76d9aafcf.mp3?version_id=1627—

1 Wakorintho 3

Kuhusu Mgawanyiko Katika Kanisa

1 Ndugu zangu, mimi sikuweza kusema nanyi kama watu wa kiroho, bali kama watu wa mwilini, kama watoto wachanga katika Kristo.

2 Naliwanywesha maziwa, wala si chakula kigumu, kwa kuwa hamkuwa tayari kwa hicho chakula kigumu. Naam, hata sasa hamkiwezi.

3 Kwa maana ninyi bado ni watu wa mwilini. Kwa kuwa bado kuna wivu na magombano miongoni mwenu, je, ninyi si watu wa mwilini, nanyi mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu?

4 Kwa maana mmoja anaposema, “Mimi ni wa Paulo,” mwingine, “Mimi ni wa Apolo,” je, ninyi si wanadamu wa kawaida?

5 Kwani, Apolo ni nani? Naye Paulo ni nani? Ni watumishi tu ambao kwa kupitia wao mliamini.

6 Mimi nilipanda mbegu, Apolo akatia maji, lakini Mungu ndiye aliyekuza.

7 Hivyo mwenye kupanda mbegu na mwenye kutia maji si kitu, bali Mungu peke yake ndiye akuzaye.

8 Apandaye mbegu ni sawa na yule atiaye maji. Kila mmoja atalipwa kulingana na kazi yake.

9 Sisi ni watenda kazi pamoja na Mungu, ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo la Mungu.

10 Kwa neema Mungu aliyonipa, niliweka msingi kama mjenzi stadi na mtu mwingine anajenga juu ya huo msingi. Lakini kila mmoja inampasa awe mwangalifu jinsi anavyojenga juu yake.

11 Kwa maana hakuna mtu ye yote awezaye kuweka msingi mwingine wo wote isipokuwa ule uliokwisha kuwekwa, ambao ni Yesu Kristo.

12 Kama mtu ye yote akijenga juu ya msingi huu kwa kutumia dhahabu, fedha, mawe ya thamani, miti, majani au nyasi,

13 kazi yake itaonekana kuwa ikoje, kwa kuwa siku ile itaidhihirisha kazi yake. Itadhihirishwa kwa moto, nao moto utapima ubora wa kazi ya kila mtu.

14 Kama kile alichojenga kitabaki, atapokea thawabu.

15 Kama kazi ya mtu itateketea, atapata hasara, ila yeye mwenyewe ataokolewa, lakini kama mtu aliyenusurika kwenye moto.

16 Je, hamjui ya kwamba ninyi ni Hekalu la Mungu na kwamba Roho wa Mungu anakaa ndani yenu?

17 Kama mtu ye yote akiliharibu Hekalu la Mungu, Mungu atamwangamiza mtu huyo, Kwa maana Hekalu la Mungu ni takatifu, ambalo ndilo ninyi.

18 Msijidanganye. Kama mtu ye yote miongoni mwenu akidhani kuwa ana hekima kwa viwango vya dunia hii, inampasa awe mjinga ili apate kuwa na hekima.

19 Kwa maana hekima ya ulimwengu huu ni upuzi mbele za Mungu. Kama ilivyoandikwa: “Mungu huwanasa wenye hekima katika hila yao,”

20 Tena, “Bwana anajua kwamba mawazo ya wenye hekima ni ubatili.”

21 Hivyo basi, mtu asijivune kuhusu wanadamu! Kwa kuwa vitu vyote ni vyenu,

22 ikiwa ni Paulo au Apolo au Kefaau dunia au uzima au mauti, au wakati uliopo au wakati ujao, haya yote ni yenu

23 na ninyi ni wa Kristo, naye Kristo ni wa Mungu.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/1CO/3-460093c974171613041a242f57f32e09.mp3?version_id=1627—

1 Wakorintho 4

Mawakili Wa Siri Za Mungu

1 Basi, watu na watuhesabu sisi kuwa tu watumishi wa Kristo na mawakili wa siri za Mungu.

2 Zaidi ya hayo, litakiwalo ni mawakili waonekane kuwa waaminifu.

3 Lakini kwangu mimi ni jambo dogo sana kwamba nihukumiwe na ninyi au na mahakama yo yote ya kibinadamu. Hata mimi mwenyewe sijihukumu.

4 Dhamiri yangu ni safi, lakini hilo halinifanyi nisiwe na hatia. Bwana ndiye anihukumuye.

5 Kwa hiyo msihukumu jambo lo lote kabla ya wakati wake, ngojeni mpaka Bwana atakapokuja. Yeye atayaleta nuruni mambo yale yaliyofichwa gizani na kuweka wazi nia za mioyo ya wanadamu. Wakati huo kila mmoja atapokea sifa anayostahili kutoka kwa Mungu.

6 Basi ndugu zangu, mambo haya nimeyafanya kuwa mfano wa mimi binafsi na Apolo kwa faida yenu, ili mweze kujifunza kutoka kwetu maana ya ule usemi usemao, “Msivuke zaidi ya yale yaliyoandikwa.” Hivyo hamtajivunia mtu fulani na kumdharau mwingine.

7 Kwa maana ni nani aliyekufanya wewe kuwa tofauti na mwingine? Ni nini ulicho nacho ambacho hukupokea? Nawe kama ulipokea, kwa nini unajivuna kama vile hukupokea?

8 Sasa tayari mnayo yale yote mnayohitaji! Tayari mmekwisha kuwa matajiri! Mmekuwa wafalme, tena bila sisi! Laiti mngekuwa wafalme kweli ili na sisi tupate kuwa wafalme pamoja nanyi!

9 Kwa maana ninaona kwamba Mungu ametuweka sisi mitume katika nafasi ya mwisho kabisa, kama watu waliohukumiwa kufa, kwa sababu tumefanywa kuwa maonyesho kwa ulimwengu wote, kwa malaika na kwa wanadamu pia.

10 Kwa ajili ya Kristo sisi ni wajinga, lakini ninyi mna hekima ndani ya Kristo. Sisi tu dhaifu, lakini ninyi mna nguvu. Tunadharauliwa, lakini ninyi mnaheshimiwa.

11 Mpaka saa hii tuna njaa na kiu, tu uchi, tumepigwa na hatuna makao.

12 Tunafanya kazi kwa bidii kwa mikono yetu wenyewe. Tunapolaaniwa, tunabariki, tunapoteswa, tunastahimili,

13 tunaposingiziwa, tunajibu kwa upole. Mpaka sasa tumekuwa kama takataka ya dunia na uchafu wa ulimwengu hadi leo.

14 Siwaandikii mambo haya ili kuwaaibisha, bali ili kuwaonya, kama wanangu wapendwa.

15 Hata kama mnao walimu 10,000 katika Kristo, lakini hamna baba wengi. Mimi nilikuwa baba yenu katika Kristo Yesu kwa kuwaletea Injili.

16 Basi nawasihi igeni mfano wangu.

17 Kwa sababu hii ninamtuma Timotheo, mwanangu mpendwa na mwaminifu katika Bwana. Yeye atawakumbusha kuhusu maisha yangu katika Kristo ambayo yanakubaliana na mafundisho yangu ninayofundisha kila mahali kwenye kila kanisa.

18 Baadhi yenu mmekuwa na majivuno mkidhani kuwa sitafika kwenu.

19 Lakini kama Bwana akipenda, nitafika kwenu mapema, nami nitapenda kujua, si tu kile wanachosema hawa watu wenye kiburi, bali pia kujua nguvu yao.

20 Kwa kuwa Ufalme wa Mungu si maneno matupu tu bali ni nguvu.

21 Ninyi amueni. Je, nije kwenu na fimbo, au nije kwa upendo na kwa roho ya upole?

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/1CO/4-62bb6e9537f1f502f485c8872c8c1a9b.mp3?version_id=1627—

1 Wakorintho 5

Mwasherati Atengwe

1 Kuna habari za kweli kwamba miongoni mwenu kuna uzinzi ambao haujatokea hata miongoni mwa watu wasiomjua Mungu: Kwamba mtu anaishi na mke wa baba yake.

2 Nanyi mwajivuna! Je, haiwapasi kuhuzunika na kumtenga na ushirika wenu mtu huyo aliyefanya mambo hayo?

3 Hata kama siko pamoja nanyi katika mwili, niko nanyi katika roho. Nami nimekwisha kumhukumu mtu huyo aliyetenda jambo hili, kama vile ningekuwapo.

4 Mnapokutana katika Jina la Bwana wetu Yesu nami nikiwepo pamoja nanyi katika roho na uweza wa Bwana Yesu ukiwepo,

5 mkabidhini mtu huyu kwa Shetani, ili mwili wake uharibiwe, ili roho yake iokolewe katika siku ya Bwana.

6 Majivuno yenu si mazuri. Je, hamjui ya kwamba chachu kidogo huchachusha donge zima la unga?

7 Ondoeni chachu ya kale ili mpate kuwa donge jipya, kama vile mlivyo hamkutiwa chachu. Kwa maana Kristo, Mwana-Kondoo wetu wa Pasaka amekwisha tolewa kuwa dhabihu.

8 Kwa hiyo, tusiiadhimishe sikukuu hii, kwa chachu ya zamani, chachu ya nia mbaya na uovu, bali kwa mkate usiotiwa chachu, ndio weupe wa moyo na kweli.

9 Niliwaandikia katika waraka wangu kuwa msishirikiane na wazinzi.

10 Sina maana kwamba msishirikiane na wazinzi wa ulimwengu huu, au wenye tamaa mbaya, wanyang’anyi au waabudu sanamu. Kwa kufanya hivyo ingewalazimu mtoke humu ulimwenguni.

11 Lakini sasa nawaandikia kwamba msishirikiane na mtu ye yote anayejiita ndugu, hali akiwa ni mzinzi, au mwenye tamaa mbaya, mwabudu sanamu au msingiziaji, mlevi au mdhalimu. Mtu kama huyo hata msile naye.

12 Yanihusu nini kuwahukumu wale watu walio nje ya kanisa? Je, si mnapaswa kuwahukumu hao walio ndani ya kanisa?

13 Mungu atawahukumu hao walio nje ya kanisa. “Ninyi mwondoeni huyo mtu mwovu miongoni mwenu.”

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/1CO/5-644ab093b6c61743e90dea0d28969c66.mp3?version_id=1627—

1 Wakorintho 6

Kushtakiana Miongoni Mwa Waamini

1 Kama mtu ye yote wa kwenu ana ugomvi na mwenzake, anathubutuje kuupeleka kwa wasiomcha Mungu ili kuamuliwa badala ya kuupeleka kwa watakatifu?

2 Je, hamjui kwamba watakatifu watauhukumu ulimwengu? Nanyi kama mtauhukumu ulimwengu, je, hamwezi kuamua mambo madogo madogo?

3 Hamjui kwamba tutawahukumu malaika? Je, si zaidi mambo ya maisha haya?

4 Kwa hiyo kama kuna ugomvi miongoni mwenu kuhusu mambo kama haya ninyi mwachagua watu ambao hata hawaheshimiwi katika kanisa kuwa waamuzi?

5 Nasema hivi ili mwone aibu. Je, inawezekana kuwa miongoni mwenu hakuna mtu mwenye hekima ya kutosha kuamua ugomvi kati ya ndugu mmoja na mwenzake?

6 Badala yake ndugu mmoja anampeleka mwenzake mahakamani, tena mbele ya watu wasioamini!

7 Ukweli ni kwamba huko kuwa na mashtaka dhidi ya mwingine miongoni mwenu tayari ni kushindwa. Kwa nini msikubali kutendewa mabaya? Kwa nini msikubali kunyang’anywa?

8 Badala yake, ninyi wenyewe mwadanganya na kutenda mabaya, tena mwawatendea ndugu zenu.

9 Je, hamjui kwamba wasio haki hawataurithi Ufalme wa Mungu? Msidanganyike: Waasherati hawaurithi Ufalme wa Mungu, wala waombao sanamu, wala wahanithi, wala walawiti,

10 wala wezi, wala wenye tamaa mbaya, wala walafi, wala wanaodhihaki, wala wanyang’anyi.

11 Baadhi yenu mlikuwa kama hao. Lakini mlioshwa, mlitakaswa, mlihesabiwa haki kwa jina la Bwana Yesu Kristo na katika Roho wa Mungu wetu.

Dhambi Za Zinaa

12 “Vitu vyote ni halali kwangu”: lakini si vitu vyote vyenye faida. “Vitu vyote ni halali kwangu”: lakini sitatawaliwa na kitu cho chote.

13 “Chakula ni kwa ajili ya tumbo na tumbo ni kwa ajili ya chakula”: lakini Mungu ataviangamiza vyote viwili. Mwili wa mwanadamu haukuumbwa kwa ajili ya zinaa bali kwa ajili ya Bwana na Bwana kwa ajili ya mwili.

14 Naye Mungu aliyemfufua Bwana kutoka kwa wafu atatufufua sisi pia kwa uweza wake.

15 Je, hamjui kwamba miili yenu ni viungo vya Kristo? Je, nichukue viungo vya mwili wa Kristo na kuviunganisha na mwili wa kahaba? La hasha!

16 Hamjui kwamba aliyeungwa na kahaba anakuwa mwili mmoja naye? Kwa kuwa imenenwa, “Hao wawili watakuwa mwili mmoja.”

17 Lakini mtu aliyeungwa na Bwana anakuwa roho moja naye.

18 Ikimbieni zinaa. Dhambi nyingine zote atendazo mtu ziko nje ya mwili wake, lakini yeye aziniye hutenda dhambi ndani ya mwili wake mwenyewe.

19 Je, hamjui ya kwamba miili yenu ni Hekalu la Roho Mtakatifu akaaye ndani yenu, ambaye mmepewa na Mungu? Ninyi si mali yenu wenyewe,

20 kwa maana mmenunuliwa kwa gharama. Kwa hiyo mtukuzeni Mungu katika miili yenu na katika roho zenu ambazo ni mali ya Mungu.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/1CO/6-f2eb8bcc6623ec8de949f95d94963db8.mp3?version_id=1627—

1 Wakorintho 7

Kuhusu Ndoa

1 Basi kuhusu mambo yale mliyoniandikia: Ni vyema mwanaume asimguse mwanamke.

2 Lakini ili kuepuka zinaa, kila mwanaume na awe na mke wake mwenyewe na kila mwanamke awe na mume wake mwenyewe.

3 Mume atimize wajibu wake wa ndoa kwa mkewe, naye vivyo hivyo mke kwa mumewe.

4 Mwanamke hana mamlaka juu ya mwili wake bali mumewe, wala mume hana mamlaka juu ya mwili wake bali mkewe.

5 Msinyimane, isipokuwa mmekubaliana kufanya hivyo kwa muda fulani ili mweze kujitoa kwa maombi, kisha mrudiane tena ili Shetani asije akapata nafasi ya kuwajaribu kwa sababu ya kutokuwa na kiasi.

6 Nasema haya kama ushauri na si amri.

7 Laiti watu wangekuwa kama mimi nilivyo. Lakini kila mtu amepewa kipawa chake kutoka kwa Mungu, mmoja ana kipawa cha namna hii na mwingine ana cha namna ile.

8 Kwa wale wasiooa na kwa wajane, ingekuwa vizuri wabaki kama mimi nilivyo.

9 Lakini kama hawawezi kujizuia, basi waoe na kuolewa, kwa maana ni afadhali kuoa au kuolewa kuliko kuwaka tamaa.

10 Kwa wale waliooana nawapa amri (si mimi ila ni Bwana): Mke asimwache mumewe.

11 Lakini kama akimwacha, ni lazima akae bila kuolewa, ama sivyo apatane tena na mumewe. Wala mume asimpe mkewe talaka.

12 Lakini kwa wengine nasema (si Bwana ila ni mimi): Kama ndugu ana mke asiyeamini, naye huyo mke anakubali kuishi pamoja naye, basi asimwache.

13 Naye mwanamke aaminiye kama ameolewa na mwanaume asiyeamini na huyo mume anakubali kuishi naye, basi huyo mwanamke asimwache.

14 Kwa maana huyo mume asiyeamini anatakaswa kupitia mkewe, naye mke asiyeamini anatakaswa kupitia mumewe. Kama isingalikuwa hivyo watoto wenu wangalikuwa si safi, lakini ilivyo sasa wao ni watakatifu.

15 Lakini kama yule asiyeamini akijitenga, basi afanye hivyo. Katika hali kama hiyo mwanamke au mwanaume aaminiye hafungwi, kwa sababu Mungu ametuita tuishi kwa amani.

16 Wewe mke, unajuaje kama utamwokoa mumeo? Au wewe mume unajuaje kama utamwokoa mkeo?

Kuishi Kama Alivyoagiza Bwana

17 Lakini kila mtu na aishi maisha aliyopangiwa na Bwana, yale Mungu aliyokuitia. Hii ni sheria yangu kwa makanisa yote.

18 Je, mtu alikuwa ametahiriwa alipoitwa? Asijifanye asiyetahiriwa. Je, mtu alikuwa hajatahiriwa alipoitwa? Asitahiriwe.

19 Kutahiriwa au kutokutahiriwa si kitu. Lakini kuzitii amri za Mungu ndilo jambo muhimu.

20 Basi kila mmoja wenu na abaki katika hali aliyoitwa nayo.

21 Je, wewe ulipoitwa ulikuwa mtumwa? Jambo hilo lisikusumbue. Hata kama unaweza kupata uhuru, tumia nafasi uliyo nayo sasa kuliko wakati mwingine wo wote.

22 Kwa maana ye yote aliyeitwa katika Bwana kama mtumwa yeye ni mtu huru kwa Bwana, kama vile ye yote aliyekuwa huru alipoitwa yeye ni mtumwa wa Kristo.

23 Mlinunuliwa kwa gharama, ili msiwe watumwa wa wanadamu.

24 Ndugu zangu, kama kila mtu alivyoitwa, akae katika wito wake alioitiwa na Mungu.

Wajane Na Wasioolewa

25 Basi, kuhusu wale walio bikira, mimi sina amri kutoka kwa Bwana, lakini mimi natoa shauri kama mtu ambaye ni mwaminifu kwa rehema za Bwana.

26 Kwa sababu ya shida iliyoko, naona ni vyema mkibaki kama mlivyo.

27 Je, umeolewa? Basi usitake talaka. Je, hujaoa? Usitafute mke.

28 Lakini kama ukioa, hujatenda dhambi; na kama bikira akiolewa, hajatenda dhambi. Lakini wale wanaooa watakabiliana na matatizo mengi katika maisha haya, nami nataka kuwazuilia hayo.

29 Lakini ndugu zangu, nina maana kwamba muda uliobaki ni mfupi. Tangu sasa wale waliooa waishi kama wasio na wake;

30 nao wanaoomboleza, kama ambao hawaombolezi; wenye furaha kama wasiokuwa nayo; wale wanaonunua, kama vile vitu walivyonunua si mali yao;

31 nao wale wanaoshughulika na vitu vya dunia hii, kama ambao hawahusiki navyo. Kwa maana dunia hii kama tunavyoiona sasa inapita.

32 Ningetaka msiwe na masumbufu. Mwanaume ambaye hajaoa anajishughulisha na mambo ya Bwana, yaani, jinsi ya kumpendeza Bwana.

33 Lakini mwanaume aliyeoa anajishughulisha na mambo ya dunia, yaani, jinsi ya kumfurahisha mkewe,

34 pia kuna tofauti kati ya mwanamke aliyeolewa na msichana bikira. Mwanamke asiyeolewa hujishughulisha na mambo ya Bwana ili awe mtakatifu kimwili na kiroho, lakini yule aliyeolewa hujishughulisha na mambo ya dunia, jinsi atakavyoweza kumfurahisha mumewe.

35 Ninasema haya kwa faida yenu, sio ili kuwawekea kizuizi cho chote, bali mpate kuishi kwa jinsi ilivyo vyema bila kuvutwa pengine katika kujitoa kwenu kwa Bwana.

36 Kama mtu ye yote anadhani kwamba hamtendei ilivyo sawa mwanamwali ambaye amemposa, naye akiwa umri wake unazidi kuendelea na mtu huyo anajisikia kwamba inampasa kuoa, afanye kama atakavyo. Yeye hatendi dhambi. Yawapasa waoane.

37 Lakini kama mwanaume ambaye ameshaamua moyoni mwake kutokuoa bila kulazimishwa na mtu ye yote, kama anaweza kujitawala kabisa; basi anafanya vyema kutokumwoa huyo mwanamwali.

38 Hivyo basi, yeye mwanaume amwoaye huyo mwanamwali afanya vyema, lakini yeye asiyemwoa afanya vyema zaidi.

39 Mwanamke aliyeolewa amefungwa na sheria maadamu mumewe yu hai. Lakini kama mumewe akifa, basi mwanamke huyo yuko huru kuolewa na mume mwingine ampendaye, lakini lazima tu awe katika Bwana.

40 Lakini kwa uamuzi wangu, naona kuwa angekuwa na furaha zaidi akibaki alivyo. Nami nadhani pia nina Roho wa Mungu.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/1CO/7-5ac4c955c1a23ab3bedca62b743e7739.mp3?version_id=1627—

1 Wakorintho 8

Chakula Kilichotolewa Sadaka Kwa Sanamu

1 Sasa kuhusu chakula kilichotolewa sadaka kwa sanamu, tunajua kwamba “sisi sote tuna ujuzi.” Lakini ujuzi hujivuna, bali upendo hujenga.

2 Mtu ye yote anayedhani kwamba anajua kitu, hajui kama impasavyo kujua.

3 Lakini mtu ampendaye Mungu, hujulikana naye.

4 Hivyo basi, kuhusu kula chakula kilichotolewa sadaka kwa sanamu, tunajua kwamba “sanamu si kitu cho chote kabisa duniani na kwamba kuna Mungu mmoja tu.”

5 Kwa maana hata kama wapo hao wanaoitwa “miungu” kama ni mbinguni au duniani (kama ilivyo kweli wapo “miungu” wengi na “mabwana” wengi).

6 Lakini kwetu sisi yuko Mungu mmoja, aliye Baba, ambaye vitu vyote vyatoka kwake na kwa ajili yake sisi twaishi na kuna Bwana mmoja tu, Yesu Kristo, ambaye kwa yeye vitu vyote vimekuwepo na kwa yeye sisi tunaishi.

7 Lakini si wote wanaojua jambo hili. Baadhi ya watu bado wamezoea kufikiria kuwa sanamu ni halisi hivyo wanapokula chakula kama hicho wanadhani kimetolewa sadaka kwa sanamu na kwa kuwa dhamiri zao ni dhaifu, kinatiwa unajisi.

8 Lakini chakula hakituleti karibu na Mungu wala hatupotezi cho chote tusipokula, wala hatuongezi cho chote kama tukila.

9 Lakini angalieni jinsi mnavyotumia uhuru wenu usije ukawa kikwazo kwao walio dhaifu katika imani.

10 Kwa maana kama mtu ye yote mwenye dhamiri dhaifu akiwaona ninyi wenye ujuzi huu mkila katika hekalu la sanamu, je, si atatiwa moyo kula chakula kilichotolewa sadaka kwa sanamu?

11 Kwa njia hiyo, huyo ndugu mwenye dhamiri dhaifu, ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake, ataangamia kwa sababu ya ujuzi wenu.

12 Mnapotenda dhambi dhidi ya ndugu zenu kwa njia hii na kujeruhi dhamiri zao zilizo dhaifu, mnamkosea Kristo.

13 Kwa hiyo, kama kile ninachokula kitamfanya ndugu yangu aanguke katika dhambi, sitakula nyama kamwe muda nchi idumupo, nisije nikamfanya ndugu yangu aanguke.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/1CO/8-dbe16e0054998ff3928509dcec9b4180.mp3?version_id=1627—

1 Wakorintho 9

Haki Za Mtume

1 Je, mimi si huru? Je, mimi si mtume? Je, mimi sikumwona Yesu, Bwana wetu? Je, ninyi si matunda ya kazi yangu katika Bwana?

2 Hata kama mimi si mtume kwa wengine, hakika mimi ni mtume kwenu, kwa maana ninyi ni chapa ya utume wangu katika Bwana.

3 Huu ndio utetezi wangu kwa hao wanaokaa kunihukumu.

4 Je, hatuna haki ya kula na kunywa?

5 Je, hatuna haki ya kusafiri na mke anayeamini, kama wanavyofanya mitume wengine na ndugu zake Bwana na Kefa?

6 Au ni mimi na Barnaba tu ambao tunalazimika kufanya kazi ili tuweze kupata mahitaji yetu?

7 Ni askari yupi aendaye vitani wakati wo wote kwa gharama zake mwenyewe? Ni mkulima gani apandaye shamba la mizabibu na asile matunda yake? Ni nani achungaye kundi na asipate maziwa yake hata kidogo?

8 Je, nasema mambo haya katika mtazamo wa kibinadamu tu? Je, sheria haisemi yayo hayo?

9 Kwa maana imeandikwa katika Sheria ya Mose: “Usimfunge ng’ombe kinywa apurapo nafaka.” Je, Mungu hapa anahusika na ng’ombe?

10 Je, Mungu hasemi haya hasa kwa ajili yetu? Hakika yameandikwa kwa ajili yetu, kwa sababu mtu anapolima na mwingine akapura nafaka, wote wanapaswa kufanya hivyo wakiwa na tumaini la kushiriki mavuno.

11 Je, ikiwa sisi tulipanda mbegu ya kiroho miongoni mwenu, Je, itakuwa ni jambo kubwa iwapo tutavuna vitu vya mwili kutoka kwenu?

12 Kama wengine wana haki ya kupata msaada kutoka kwenu, sisi je, isingepasa tuwe na haki hiyo hata zaidi?

Lakini sisi hatukutumia haki hii. Kinyume chake, tunavumilia kila kitu ili tusije tukazuia injili ya Kristo.

13 Je, hamjui kwamba, watu wafanyao kazi Hekaluni hupata chakula chao kutoka Hekaluni, nao wale wahudumiao madhabahuni hushiriki kile kitolewacho madhabahuni?

14 Vivyo hivyo, Bwana ameagiza kwamba wale wanaohubiri injili wapate mahitaji yao kutokana na injili.

15 Lakini sijatumia hata mojawapo ya haki hizi. Nami siandiki haya nikitumaini kwamba mtanifanyia mambo hayo. Heri nife kuliko mtu ye yote kuninyima huku kujisifu kwangu.

16 Lakini ninapohubiri injili siwezi kujisifu maana ninalazimika kuhubiri. Ole wangu nisipoihubiri Injili!

17 Nikihubiri kwa hiari ninayo thawabu, lakini kama si kwa hiari, ni kwamba nalazimika kufanya hivyo, basi ninachofanya ni kutekeleza tu uwakili niliowekewa.

18 Basi je, thawabu yangu ni nini? Thawabu yangu ni hii: Ni kwamba katika kuhubiri Injili niitoe bila gharama, nisije nikatumia vibaya ule uwezo wangu nilio nao katika Injili.

19 Ingawa mimi ni huru, wala si mtumwa wa mtu ye yote, nimejifanya kuwa mtumwa wa kila mtu, ili niweze kuwavuta wengi zaidi.

20 Kwa Wayahudi, nilikuwa kama Myahudi, ili niwapate Wayahudi. Kwa watu wale walio chini ya sheria, nilikuwa kama aliye chini ya sheria (ingawa mimi siko chini ya sheria), ili niweze kuwapata wale walio chini ya sheria.

21 Kwa watu wasio na Sheria nilikuwa kama asiye na Sheria (ingawa siko huru mbali na Sheria ya Mungu, bali niko chini ya Sheria ya Kristo), ili niweze kuwapata wale wasio na Sheria.

22 Kwa walio dhaifu nilikuwa dhaifu, ili niweze kuwapata walio dhaifu. Nimekuwa mtu wa hali zote kwa watu wote ili kwa njia yo yote niweze kuwaokoa baadhi yao.

23 Nafanya haya yote kwa ajili ya Injili, ili nipate kushiriki baraka zake.

24 Je, hamjui kwamba katika mashindano ya mbio wote wanaoshindana hukimbia, lakini ni mmoja wao tu apewaye tuzo? Kwa hiyo kimbieni katika mashindano kwa jinsi ambavyo mtapata tuzo.

25 Kila mmoja anayeshiriki katika mashindano hufanya mazoezi makali. Wao hufanya hivyo ili wapokee taji isiyodumu, lakini sisi tunafanya hivyo ili kupata taji idumuyo milele.

26 Kwa hiyo mimi sikimbii kama mtu akimbiaye bila lengo, sipigani kama mtu anayepiga hewa,

27 la, bali nautesa mwili wangu na kuutumikisha ili nikiisha kuwahubiria wengine, mimi nisiwe mtu wa kukataliwa.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/1CO/9-dbd225cdb0b3c985857d920bedd822de.mp3?version_id=1627—