Marko 5

Yesu Amponya Mtu Mwenye Pepo

1 Wakafika upande wa pili wa bahari wakaingia katika nchi ya Wagerasi.

2 Yesu alipotoka kwenye mashua, mara mtu mmoja mwenye pepo mchafu akatoka makaburini akakutana naye.

3 Mtu huyu aliishi makaburini, wala hakuna aliyeweza kumzuia hata kwa kumfunga minyororo,

4 kwa kuwa mara kwa mara alikuwa amefungwa kwa minyororo mikononi na miguuni, akaikata hiyo minyororo na kuzivunja zile pingu miguuni mwake. Hapakuwa na mtu ye yote aliyekuwa na nguvu za kumzuia.

5 Usiku na mchana alikuwa makaburini na milimani, akipiga kelele na kujikatakata kwa mawe.

6 Alipomwona Yesu kwa mbali, alimkimbilia akapiga magoti mbele yake.

7 Akapiga kelele kwa nguvu akisema, “Una nini nami, Yesu, Mwana wa Mungu Aliye Juu Sana? Ninakusihi kwa jina la Mungu, usinitese!”

8 Kwa kuwa Yesu alikuwa amemwambia, “Mtoke mtu huyu, wewe pepo mchafu!”

9 Yesu akamwuliza, “Jina lako ni nani?”

# Akamjibu, “Jina langu ni Legioni, kwa kuwa tuko wengi.”

10 Akamwomba sana Yesu asiwapeleke nje ya nchi ile.

11 Kundi kubwa la nguruwe lilikuwa karibu likilisha kando ya kilima.

12 Wale pepo wachafu wakamsihi Yesu wakisema, “Tuamuru twende kwenye wale nguruwe, turuhusu tuwaingie.”

13 Basi Yesu akawaruhusu, nao wale pepo wachafu wakatoka wakawaingia hao nguruwe. Lile kundi lilikuwa na nguruwe wapatao 2,000, likatelemkia gengeni kwa kasi nalo likazama baharini.

14 Wale waliokuwa wakichunga hao nguruwe wakakimbilia mjini na vijijini kueleza yaliyotukia. Watu wakatoka kwenda kuona hayo yaliyokuwa yametukia.

15 Walipofika kwa Yesu, wakamwona yule mtu aliyekuwa amepagawa na pepo wachafu Legioni, akiwa ameketi hapo, amevaa nguo na pia akiwa na akili zake timamu. Wakaogopa.

16 Wale walioyaona mambo haya wakawaeleza watu wengine yaliyomtokea yule aliyekuwa na pepo wachafu na lile kundi la nguruwe.

17 Basi watu wakaanza kumwomba Yesu aondoke katika nchi yao.

18 Yesu alipokuwa anaingia kwenye mashua, yule mtu aliyekuwa amepagawa na pepo wachafu akamsihi Yesu waende pamoja.

19 Yesu hakumruhusu, bali alimwambia, “Nenda nyumbani kwa jamaa yako ukawaeleze mambo makuu aliyokutendea Bwana na jinsi alivyokuhurumia.”

20 Yule mtu akaenda zake akaanza kutangaza katika Dekapoli jinsi Yesu alivyomtendea, nao watu wote wakastaajabu.

Mwanamke Aponywa

21 Yesu alipokwisha kuvuka tena na kufika ng’ambo, umati mkubwa wa watu ukamzunguka, yeye akiwa kando ya bahari.

22 Kisha mmoja wa viongozi wa sinagogi aliyeitwa Yairo, akafika pale, naye alipomwona Yesu akapiga magoti miguuni pake,

23 akamsihi akisema, “Binti yangu mdogo ni mgonjwa mahututi. Tafadhali nakusihi njoo uweke mikono yako juu yake ili apate kupona.”

24 Hivyo Yesu akaenda pamoja naye.

Umati mkubwa wa watu ukamfuata, watu wakawa wanamsonga.

25 Hapo palikuwa na mwanamke aliyekuwa amesumbuliwa na tatizo la kutokwa damu kwa miaka kumi na miwili.

26 Mwanamke huyu alikuwa ameteseka sana kwa mikono ya matabibu wengi na kutumia kila kitu alichokuwa nacho lakini badala ya kupona hali yake ilizidi kuwa mbaya.

27 Alikuwa amesikia habari za Yesu naye akaja kwa nyuma yake kwenye umati wa watu, akaligusa vazi lake,

28 kwa maana alisema moyoni mwake, “Kama nikiweza kuligusa vazi lake tu, nitapona.”

29 Mara kutoka damu kwake kukakoma, naye akajisikia mwilini mwake amepona kabisa.

30 Ghafula Yesu akatambua kuwa nguvu zimemtoka. Akaugeukia ule umati wa watu na kuuliza, “Ni nani aliyenigusa?”

31 Wanafunzi wake wakamjibu, “Unaona jinsi umati wa watu unavyokusonga, wawezaje kuuliza, ‘Ni nani aliyenigusa?’ ”

32 Lakini Yesu akaangalia pande zote ili aone ni nani aliyemgusa.

33 Yule mwanamke, akijua kilichomtokea, akaja, akaanguka miguuni pake akitetemeka kwa hofu, akamweleza ukweli wote.

34 Yesu akamwambia, “Binti, imani yako imekuponya. Nenda kwa amani, upone kabisa ugonjwa wako.”

Yesu Amfufua Binti Yairo

35 Alipokuwa bado anaongea, watu wakafika kutoka nyumbani kwa Yairo wakamwambia, “Binti yako amekufa. Kwa nini kuendelea kumsumbua Mwalimu?”

36 Kwa kusikia hayo waliyosema, Yesu akamwambia huyo kiongozi wa sinagogi, “Usiogope. Amini tu.”

37 Hakumruhusu mtu mwingine ye yote amfuate isipokuwa Petro, Yakobo na Yohana nduguye Yakobo.

38 Walipofika nyumbani kwa yule kiongozi wa sinagogi, Yesu akaona ghasia, watu wakilia na kuomboleza kwa sauti kubwa.

39 Alipokwisha kuingia ndani, akawaambia, “Kwa nini mnafanya ghasia na kulia? Mtoto hajafa bali amelala tu.”

40 Wale watu wakamcheka kwa dharau.

Lakini yeye akawatoa wote nje, akawachukua baba na mama wa yule mtoto pamoja na wale wanafunzi aliokuwa nao. Wakaingia ndani mpaka pale alipokuwa yule mtoto.

41 Akamshika mtoto mkono akamwambia, “Talitha koum!” (Maana yake, “Msichana, ninakuambia, amka!”)

42 Mara yule msichana akasimama, akaanza kutembea (alikuwa na umri wa miaka kumi na miwili). Walipoona haya, wakastaajabu sana.

43 Yesu akawaagiza kwa ukali wasimweleze mtu ye yote jambo hili, naye akawaambia wampe yule msichana chakula.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/MRK/5-d7305734c75087550fefe4722ed44c12.mp3?version_id=1627—

Marko 6

Nabii Hana Heshima Kwao

1 Yesu akaondoka huko na kwenda mji wa kwao, akiwa amefuatana na wanafunzi wake.

2 Ilipofika siku ya Sabato, akaanza kufundisha katika sinagogi na wengi waliomsikia wakashangaa.

Wakauliza, “Mtu huyu ameyapata wapi mambo haya yote? Tazama ni hekima ya namna gani hii aliyopewa? Tazama matendo ya miujiza ayafanyayo kwa mikono yake!

3 Huyu si yule seremala, mwana wa Maria? Na ndugu zake si Yakobo, Yosefu, Yuda na Simoni? Dada zake wote si tuko nao hapa petu?” Nao wakachukizwa sana kwa ajili yake wakakataa kumwamini.

4 Yesu akawaambia, “Nabii hakosi heshima isipokuwa katika mji wake mwenyewe na miongoni mwa jamaa na ndugu zake.”

5 Hakufanya miujiza yo yote huko isipokuwa kuweka mikono yake juu ya wagonjwa wachache na kuwaponya.

6 Naye akashangazwa sana kwa jinsi wasivyokuwa na imani.

Yesu Awatuma Wale Kumi Na Wawili

Kisha Yesu akawa anakwenda huku na huko kutoka kijiji kimoja hadi kingine akifundisha.

7 Akawaita wale kumi na wawili, akawatuma wawili wawili na kuwapa mamlaka kutoa pepo wachafu.

8 Akawaagiza akisema, “Msichukue cho chote kwa ajili ya safari isipokuwa fimbo tu. Msichukue mkate, wala mkoba, wala fedha kwenye mikanda yenu,

9 bali mvae viatu, lakini msivae nguo ya ziada.”

10 Akawaambia, “Mkiingia kwenye nyumba yo yote, kaeni humo hadi mtakapoondoka katika mji huo.

11 Kama mahali po pote hawatawakaribisha wala kuwasikiliza, mtakapoondoka huko, kung’uteni mavumbi yaliyoko miguuni mwenu, ili kuwa ushuhuda dhidi yao.”

12 Kwa hiyo wakatoka na kuhubiri kwamba inawapasa watu kutubu na kuacha dhambi.

13 Wakatoa pepo wachafu wengi, wakawapaka wagonjwa wengi mafuta na kuwaponya.

Yohana Mbatizaji Akatwa Kichwa

14 Mfalme Herode akasikia habari hizi, kwa maana jina la Yesu lilikuwa limejulikana kila mahali. Watu wengine walikuwa wakisema, “Yohana Mbatizaji amefufuka kutoka kwa wafu ndiyo maana uwezo wa kutenda miujiza unafanya kazi ndani yake!”

15 Wengine wakasema, “Yeye ni Eliya.”

Nao wengine wakasema, “Yeye ni nabii, kama mmojawapo wa wale manabii wa zamani.”

16 Lakini Herode aliposikia habari hizi, akasema, “Huyo ni Yohana Mbatizaji, niliyemkata kichwa, amefufuka!”

17 Kwa kuwa Herode alikuwa ameagiza kwamba Yohana Mbatizaji akamatwe, afungwe na kutiwa gerezani. Alifanya hivi kwa sababu ya Herodia, mke wa Filipo ndugu yake, ambaye alikuwa amemwoa.

18 Yohana alikuwa amemwambia Herode, “Si halali wewe kumwoa mke wa ndugu yako.”

19 Kwa hiyo Herodia alikuwa amemwekea Yohana kinyongo akataka kumwua. Lakini hakuweza,

20 kwa sababu Herode alimwogopa Yohana akijua kwamba ni mtu mwenye haki na mtakatifu, akawa anamlinda. Herode alifadhaika sana alipomsikia Yohana, lakini bado alipenda kumsikiliza.

21 Mfalme Herode alifanya karamu kubwa, wakati wa sikukuu ya kuzaliwa kwake. Akawaalika maafisa wake wakuu, majemadari wa jeshi na watu mashuhuri wa Galilaya. Hatimaye Herodia alipata wasaa aliokuwa akiutafuta.

22 Binti yake Herodia alipoingia na kucheza, akamfurahisha Herode pamoja na wageni wake walioalikwa chakulani.

Mfalme Herode akamwambia yule binti, “Niombe kitu cho chote utakacho, nami nitakupa.”

23 Tena akamwahidi kwa kiapo akamwambia, “Cho chote utakachoomba nitakupa, hata kama ni nusu ya ufalme wangu.”

24 Yule binti akatoka nje akaenda kumwuliza mama yake, “Niombe nini?”

Mama yake akajibu, “Omba kichwa cha Yohana Mbatizaji.”

25 Yule binti akarudi haraka kwa mfalme akamwambia, “Nataka unipe sasa hivi kichwa cha Yohana Mbatizaji kwenye sinia.”

26 Mfalme akasikitika sana, lakini kwa sababu alikuwa ameapa mbele ya wageni wake hakutaka kumkatalia.

27 Mara mfalme akatuma askari mmojawapo wa walinzi wake kukileta kichwa cha Yohana. Akaenda na kumkata Yohana kichwa humo gerezani,

28 akakileta kichwa chake kwenye sinia na kumpa yule msichana, naye yule msichana akampa mama yake.

29 Wanafunzi wake walipopata habari hizi, wakaja kuuchukua mwili wake, wakauzika kaburini.

Yesu Awalisha Watu 5,000

30 Wale wanafunzi wa Yesu wakamkusanyikia na kumpa taarifa ya mambo yote waliyokuwa wamefanya na kufundisha.

31 Basi kwa kuwa watu wengi mno walikuwa wakija na kutoka, hata wakawa hawana nafasi ya kula, Yesu akawaambia wanafunzi wake, “Twendeni peke yetu mahali pa faragha, mpate kupumzika.”

32 Hivyo wakaondoka kwa mashua peke yao wakaenda mahali pa faragha pasipo na watu.

33 Lakini watu wengi waliowaona wakiondoka, wakawatambua, nao wakawatangulia haraka kwa miguu kutoka katika miji yote, nao wakatangulia kufika.

34 Yesu alipofika nchi kavu na kuuona huo umati wa watu, aliwaonea huruma kwa maana walikuwa kama kondoo wasiokuwa na mchungaji. Kwa hiyo akaanza kuwafundisha mambo mengi.

35 Mchana ulipokuwa umeendelea sana, wanafunzi wake wakamwendea, wakamwambia, “Mahali hapa ni mbali na pasipo na watu, nazo saa zimekwenda sana.

36 Waage watu ili waweze kwenda sehemu za mashambani na vijiji vya jirani, wakajinunulie chakula.”

37 Lakini Yesu akawajibu, “Wapeni ninyi chakula.”

# Wakamwambia, “Je, twende tukanunue mikate ya dinari 200ili tuwape watu hawa wale?”

38 Akawauliza, “Kuna mikate mingapi? Nendeni mkaangalie.”

Walipokwisha kuona wakarudi, wakamwambia, “Kuna mikate mitano na samaki wawili.”

39 Kisha Yesu akawaamuru wawaketishe watu makundi makundi kwenye majani,

40 nao wakaketi kwenye makundi ya watu mia mia na wengine hamsini hamsini.

41 Yesu akaichukua ile mikate mitano na wale samaki wawili akatazama mbinguni, akashukuru, kisha akaimega ile mikate, akawapa wanafunzi wake ili wawagawie wale watu wote. Pia akawagawia wote wale samaki wawili.

42 Watu wote wakala, wakashiba.

43 Wanafunzi wake wakakusanya vipande vilivyosalia vya mikate na samaki, wakajaza vikapu kumi na viwili.

44 Idadi ya wanaume waliokula walikuwa 5,000.

Yesu Atembea Juu Ya Maji

45 Mara Yesu akawataka wanafunzi wake waingie kwenye mashua watangulie kwenda Bethsaida, wakati yeye anauaga ule umati wa watu.

46 Baada ya kuwaaga wale watu, akaenda mlimani kuomba.

47 Ilipofika jioni, ile mashua ilikuwa imefika katikati ya bahari na Yesu alikuwa peke yake katika nchi kavu.

48 Akawaona wanafunzi wake wanahangaika na kupiga makasia kwa nguvu, kwa sababu upepo ulikuwa wa mbisho. Karibu na mapambazuko, Yesu akawaendea wanafunzi wake, akitembea juu ya maji. Alikuwa karibu kuwapita,

49 lakini walipomwona akitembea juu ya maji, wakadhani ni mzimu, wakapiga yowe,

50 kwa sababu wote walipomwona waliogopa.

Mara Yesu akasema nao, akawaambia, “Jipeni moyo! Ni Mimi, msiogope!”

51 Akapanda kwenye mashua yao na ule upepo ukakoma! Wakashangaa kabisa.

52 Kwa kuwa walikuwa hawajaelewa kuhusu ile mikate, mioyo yao ilikuwa migumu.

53 Walipokwisha kuvuka, wakafika Genesareti, wakatia nanga.

54 Mara waliposhuka kutoka katika mashua yao, watu wakamtambua Yesu,

55 wakaenda katika vijiji vyote upesi, wakawabeba wagonjwa kwenye mikeka ili kuwapeleka mahali po pote waliposikia kuwa Yesu yupo.

56 Kila mahali Yesu alipokwenda, iwe vijijini, mijini na mashambani, watu waliwaweka wagonjwa wao masokoni, wakamwomba awaruhusu hao wagonjwa waguse japo upindo wa vazi lake. Nao wote waliomgusa, waliponywa.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/MRK/6-6c9770ed2bdb5cff6a5f180b2ee16308.mp3?version_id=1627—

Marko 7

Kilicho Safi Na Kilicho Najisi

1 Mafarisayo na baadhi ya walimu wa sheria waliokuwa wametoka Yerusalemu wakakusanyika mbele ya Yesu.

2 Wakawaona baadhi ya wanafunzi wake wakila chakula kwa mikono iliyo najisi, yaani, bila kunawa kama ilivyotakiwa na sheria ya dini ya Wayahudi.

3 Kwa kuwa Mafarisayo na Wayahudi wote hawali chakula pasipo kunawa kwa kufuata desturi za wazee wao.

4 Wanapotoka sokoni hawawezi kula pasipo kunawa. Pia kuna desturi nyingine nyingi wanazofuata kama vile jinsi ya kuosha vikombe, vyungu na vyombo vya shaba.

5 Kwa hiyo wale Mafarisayo na walimu wa sheria wakamwuliza Yesu, “Mbona wanafunzi wako hawafuati desturi za wazee wetu na badala yake wanakula kwa mikono najisi?”

6 Yesu akawajibu, “Nabii Isaya alisema ukweli alipotabiri juu yenu, ninyi wanafiki, kama ilivyoandikwa:

“ ‘Watu hawa wananiheshimu kwa midomo yao,

lakini mioyoni mwao wako mbali nami.

7 Huniabudu bure,

wakifundisha mapokeo ya wanadamu.’

8 Ninyi mmeziacha amri za Mungu na kushika desturi za watu.”

9 Naye akawaambia, “Ninyi mnayo njia nzuri ya kukataa amri za Mungu ili mpate kuzishika desturi zenu!

10 Kwa mfano, Mose alisema, ‘Waheshimu baba yako na mama yako’ na ‘Ye yote amtukanaye baba yake au mama yake auawe.’

11 Lakini ninyi mwasema mtu akimwambia baba yake au mama yake kuwa, ‘Msaada ambao ningekupa ni Korbani’ (yaani, umetengwa kama sadaka kwa Mungu),

12 basi hawajibiki tena kumsaidia baba yake au mama yake.

13 Kwa njia hiyo ninyi mnabatilisha neno la Mungu kwa taratibu zenu mlizojiwekea. Nanyi mnafanya mambo mengi ya jinsi hiyo.”

14 Yesu akaita tena ule umati wa watu akawaambia, “Nisikilizeni, kila mmoja wenu na mwelewe jambo hili.

15 Hakuna kitu kinachomwingia mtu kimtiacho unajisi, lakini kile kimtokacho ndicho kimtiacho unajisi.

16 Kama mtu ye yote ana masikio ya kusikia na asikie.”

17 Akiisha kuuacha ule umati wa watu na kuingia ndani, wanafunzi wake wakamwuliza maana ya mfano ule.

18 Akawajibu, “Hata nanyi hamwelewi? Hamtambui kwamba kitu kimwingiacho mtu hakimtii unajisi?

19 Mtu akila kitu hakiingii moyoni mwake bali tumboni na baadaye hutolewa nje ya mwili wake.” (Kwa kusema hivi, Yesu alivihalalisha vyakula vyote kuwa ni “safi.”)

20 Akaendelea kusema, “Kile kimtokacho mtu ndicho kimtiacho unajisi.

21 Kwa maana kutoka ndani ya moyo wa mtu hutoka: Mawazo mabaya, uasherati,

22 wizi, uuaji, uzinzi, tamaa mbaya, uovu, udanganyifu, ufisadi, wivu, matukano, kiburi na upumbavu.

23 Maovu haya yote hutoka ndani ya mtu nayo ndiyo yamtiayo mtu unajisi.”

Imani Ya Mwanamke Msirofoinike

24 Ndipo Yesu akaondoka hapo akaenda sehemu za Tiro. Akaingia katika nyumba moja, naye hakutaka mtu ye yote ajue kwamba yuko humo. Lakini hakuweza kujificha.

25 Lakini mwanamke mmoja ambaye binti yake mdogo alikuwa na pepo mchafu, akaja na kumpigia magoti miguuni pake.

26 Basi huyo mwanamke alikuwa Myunani, aliyezaliwa Foinike ya Siria. Akamsihi Yesu amtoe binti yake huyo pepo mchafu.

27 Yesu akamwambia, “Waache watoto washibe kwanza, kwa maana si vyema kuchukua chakula cha watoto na kuwatupia mbwa.”

28 Lakini yule mwanamke akamjibu, “Bwana, hata mbwa walio chini ya meza hula makombo ya chakula cha watoto.”

29 Ndipo Yesu akamjibu, “Kwa sababu ya jibu lako, enenda zako nyumbani, yule pepo mchafu amemtoka binti yako.”

30 Akaenda zake nyumbani akamkuta binti yake amelala kitandani, yule pepo mchafu akiwa amemtoka.

Yesu Amponya Mtu Aliyekuwa Kiziwi Na Bubu

31 Kisha Yesu akaondoka sehemu za Tiro, akapita katikati ya Sidoni, hadi Bahari ya Galilaya na kuingia eneo la Dekapoli.

32 Huko, watu wakamletea Yesu mtu mmoja kiziwi, ambaye pia alikuwa na kigugumizi, wakamwomba aweke mkono wake juu ya huyo mtu na amponye.

33 Baadaye Yesu akampeleka yule kiziwi kando mbali na watu, Yesu akatia vidole vyake masikioni mwa yule mtu. Kisha akatema mate na kuugusa ulimi wa yule mtu.

34 Ndipo Yesu akatazama mbinguni, akavuta hewa ndani kwa nguvu akamwambia, “Efatha!” Yaani, “Funguka!”

35 Mara masikio yake yakafunguka na ulimi wake ukaachiwa akaanza kuongea sawasawa.

36 Yesu akawaamuru wasimwambie mtu ye yote habari hizi. Lakini kadiri alivyowazuia, ndivyo walivyozidi kutangaza kwa bidii.

37 Walistaajabu mno. Wakasema, “Amefanya mambo yote vizuri mno! Amewawezesha viziwi wasikie na bubu waseme!”

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/MRK/7-1d73435573c4112f154ccd8e010579c0.mp3?version_id=1627—

Marko 8

Yesu Alisha Watu 4,000

1 Katika siku hizo, umati mkubwa wa watu ulikusanyika tena. Kwa kuwa walikuwa hawana chakula, Yesu akawaita wanafunzi wake akawaambia,

2 “Ninauhurumia huu umati wa watu, kwa sababu sasa wamekuwa nami kwa muda wa siku tatu na hawana chakula.

3 Nikiwaaga waende nyumbani bila kula, watazimia njiani kwa sababu baadhi yao wametoka mbali.”

4 Wanafunzi wake wakamjibu, “Lakini hapa nyikani tutapata wapi mikate ya kutosha kuwalisha?”

5 Yesu akawauliza, “Mna mikate mingapi?”

Wakajibu, “Tuna mikate saba.”

6 Akawaambia watu waketi chini. Akiisha kuichukua mikate saba na kushukuru, akaimega na kuwapa wanafunzi wake ili wawagawie watu. Wanafunzi wake wakafanya hivyo.

7 Walikuwa pia na visamaki vichache, Yesu akavibariki, akawaamuru wanafunzi wake wawagawie watu.

8 Wale watu walikula na kutosheka, baadaye wanafunzi wakakusanya vipande vilivyosalia wakajaza vikapu saba.

9 Watu waliokula walikuwa wapata 4,000. Akiisha kuwaaga,

10 aliingia kwenye mashua pamoja na wanafunzi wake akaenda sehemu za Dalmanutha.

11 Mafarisayo wakaja, wakaanza kumhoji Yesu. Ili kumtega, wakamwomba awaonyeshe ishara kutoka mbinguni.

12 Akahuzunika moyoni, akawaambia, “Kwa nini kizazi hiki kinataka ishara? Amin, nawaambieni, hakitapewa ishara yo yote.”

13 Kisha akawaacha, akarudi kwenye mashua, akavuka hadi ng’ambo.

Chachu Ya Mafarisayo Na Ya Herode

14 Wanafunzi walikuwa wamesahau kuleta mikate ya kutosha. Walikuwa na mkate mmoja tu kwenye mashua.

15 Yesu akawaonya: “Jihadharini na chachu ya Mafarisayo na ya Herode.”

16 Wakaanza kujadiliana wao kwa wao wakasema, “Anasema hivi kwa kuwa hatukuleta mikate.”

17 Yesu akifahamu majadiliano yao, akawauliza: “Mbona mnazungumzia kuhusu kutokuwa na mikate? Bado hamtambui wala kuelewa? Je, mbona mioyo yenu ni migumu kiasi hicho?

18 Mna macho lakini mnashindwa kuona, mna masikio lakini mnashindwa kusikia? Je, hamkumbuki?

19 Nilipoimega ile mikate mitano kuwalisha watu 5,000, mlikusanya vikapu vingapi vilivyojaa vya masazo?”

Wakamjibu, “Kumi na viwili.”

20 “Je, nilipomega ile mikate saba kuwalisha watu 4,000, mlikusanya vikapu vingapi vilivyojaa vya masazo?”

Wakamjibu, “Saba.”

21 Ndipo akawauliza, “Je, bado tu hamwelewi?”

Yesu Amponya Kipofu Huko Bethsaida

22 Wakafika Bethsaida na baadhi ya watu wakamleta mtu mmoja kipofu wakamsihi Yesu amguse.

23 Yesu akamshika mkono huyo kipofu akampeleka nje ya kijiji. Baada ya kuyatemea mate macho ya yule kipofu na kumwekea mikono, Yesu akamwuliza, “Unaona cho chote?”

24 Yule kipofu akaangalia, akasema, “Ninaona watu, wanaonekana kama miti inayotembea.”

25 Yesu akamwekea tena mikono machoni. Kisha macho yake yakafunguka, kuona kwake kukarejea naye akaona kila kitu dhahiri.

26 Yesu akamuaga aende nyumbani kwake, akimwambia, “Hata kijijini usiingie.”

Petro Amkiri Yesu Kuwa Ndiye Kristo

27 Yesu na wanafunzi wake wakaondoka kwenda katika vijiji vya Kaisaria-Filipi. Walipokuwa njiani Yesu akawauliza, “Watu husema mimi ni nani?”

28 Wakamjibu, “Baadhi husema wewe ni Yohana Mbatizaji, wengine husema ni Eliya na wengine husema wewe ni mmojawapo wa manabii.”

29 Akawauliza, “Je, ninyi, mnasema mimi ni nani?”

# Petro akajibu, “Wewe ndiwe Kristo.”

30 Akawaonya wasimwambie mtu ye yote habari zake.

Yesu Atabiri Juu Ya Kifo Chake

31 Ndipo akaanza kuwafundisha wanafunzi wake kuwa Mwana wa Adamu atapata mateso mengi na kukataliwa na wazee, viongozi wa makuhani, na walimu wa sheria na kwamba atauawa na baada ya siku tatu atafufuka.

32 Aliyasema haya waziwazi, ndipo Petro akamchukua kando akaanza kumkemea.

33 Lakini Yesu alipogeuka na kuwaangalia wanafunzi wake, akamkemea Petro, akasema, “Rudi nyuma yangu Shetani! Wewe huwazi yaliyo ya Mungu bali ya wanadamu.”

34 Ndipo akauita ule umati wa watu pamoja na wanafunzi wake, akasema, “Mtu ye yote akitaka kunifuata, ni lazima ajikane mwenyewe, auchukue msalaba wake, anifuate.

35 Kwa maana mtu ye yote anayetaka kuiokoa nafsi ataipoteza, lakini yeye ayapotezaye maisha yake kwa ajili yangu na kwa ajili ya Injili atayaokoa.

36 Mtu atafaidiwa nini kama akiupata ulimwengu wote lakini akaipoteza nafsi yake?

37 Au mtu atatoa nini apate tena maisha yake?

38 Mtu ye yote anayenionea aibu mimi na maneno yangu katika kizazi hiki cha uzinzi na cha dhambi, Mwana wa Adamu, atamwonea aibu wakati atakapokuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu.”

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/MRK/8-7ce75f79a9969e587597c7701faaa16c.mp3?version_id=1627—

Marko 9

1 Yesu akaendelea kuwaambia, “Amin, amin nawaambia, kuna watu waliosimama hapa ambao hawataonja mauti kabla ya kuuona Ufalme wa Mungu ukija katika nguvu.”

Yesu Ageuka Sura

2 Baada ya siku sita, Yesu akawachukua Petro, Yakobo na Yohana akawapeleka juu ya mlima mrefu, mahali walipokuwa faraghani. Huko, Yesu akageuka sura mbele yao.

3 Mavazi yake yakawa na weupe wa kuzima macho, meupe kuliko ambavyo mtu ye yote duniani angaliweza kuyang’arisha.

4 Mose na Eliya wakawatokea, wakawa wanazungumza na Yesu.

5 Petro akamwambia Yesu, “Mwalimu, ni vizuri sisi tukae hapa. Turuhusu tujenge vibanda vitatu: Kimoja chako, kimoja cha Mose na kingine cha Eliya.”

6 Petro hakujua aseme nini kwa maana yeye na wenzake walikuwa wameogopa sana.

7 Ndipo pakatokea wingu, likawafunika, nayo sauti kutoka katika lile wingu ikasema, “Huyu ni Mwanangu, nimpendaye, msikilizeni yeye.”

8 Mara walipotazama huku na huku, hawakuona tena mtu mwingine ye yote pamoja nao isipokuwa Yesu.

9 Walipokuwa wakishuka kutoka mlimani, Yesu akawakataza wasimwambie mtu ye yote mambo waliyoona, mpaka Mwana wa Adamu atakapofufuka kutoka kwa wafu.

10 Wakalihifadhi jambo hilo wao wenyewe, lakini wakawa wanajiuliza, “Huku kufufuka kwa wafu maana yake nini?”

11 Wakamwuliza, “Kwa nini walimu wa sheria husema kwamba ni lazima Eliya aje kwanza?”

12 Yesu akawajibu, “Ni kweli, Eliya yuaja kwanza, ili kurudisha upya mambo yote. Mbona basi imeandikwa kwamba Mwana wa Adamu ni lazima ateseke sana na kudharauliwa?

13 Lakini ninawaambia, Eliya amekwisha kuja nao wakamtendea walivyopenda, kama ilivyoandikwa kumhusu yeye.”

Kuponywa Kwa Mvulana Mwenye Pepo Mchafu

14 Walipowafikia wale wanafunzi wengine, wakawakuta wamezungukwa na umati mkubwa wa watu na baadhi ya walimu wa sheria wakibishana nao.

15 Mara wale watu walipomwona Yesu, wakastaajabu sana, wakamkimbilia, ili kumsalimu.

16 Akawauliza wanafunzi wake, “Mnabishana nao kuhusu nini?”

17 Mtu mmoja miongoni mwa ule umati wa watu akajibu, “Mwalimu, nilimleta kwako mwanangu ambaye ana pepo mchafu anamfanya asiweze kuongea.

18 Kila mara huyo pepo mchafu ampagaapo mwanangu, humwangusha chini na kumfanya atokwe povu mdomoni na kusaga meno, kisha mwili wake hukauka. Niliwaomba wanafunzi wako wamtoe huyo pepo mchafu, lakini hawakuweza.”

19 Yesu akawaambia, “Enyi kizazi kisicho na imani! Nitakuwa pamoja nanyi mpaka lini? Nitachukuliana nanyi mpaka lini? Mleteni huyo mvulana kwangu.”

20 Nao wakamleta yule mvulana. Yule pepo mchafu alipomwona Yesu, mara akamtia yule mvulana kifafa, akaanguka, akagaagaa chini huku akitokwa na povu kinywani.

21 Yesu akamwuliza baba yake, “Mwanao amekuwa akitokewa na hali hii tangu lini?”

Akamjibu, “Tangu utoto wake.

22 Mara kwa mara huyo pepo mchafu amekuwa akimwangusha kwenye moto au kwenye maji ili kumwangamiza. Lakini kama unaweza kufanya jambo lo lote, tafadhali tuhurumie utusaidie.”

23 Yesu akamwambia, “Kama ukiweza kuamini, yote yawezekana kwake yeye aaminiye.”

24 Mara baba yake yule mvulana akapiga kelele akisema, “Ninaamini. Nisaidie kutokuamini kwangu!”

25 Yesu alipoona kwamba umati wa watu unakusanyika pamoja mbio, akamkemea yule pepo mchafu, akimwambia, “Wewe pepo bubu na kiziwi, nakuamuru umtoke wala usimwingie tena!”

26 Yule pepo mchafu akiisha kupiga kelele, akamtia kifafa kwa nguvu, akamtoka. Yule mvulana alikuwa kama maiti, hivyo watu wengi wakasema, “Amekufa.”

27 Lakini Yesu akamshika mkono akamwinua, naye akasimama.

28 Baada ya Yesu kuingia ndani ya nyumba, wanafunzi wake wakamwuliza wakiwa peke yao, “Mbona sisi hatukuweza kumtoa huyo pepo mchafu?”

29 Yesu akawajibu, “Hali hii haiwezi kutoka isipokuwa kwa kuomba na kufunga.”

Yesu Atabiri Tena Kifo Chake Na Ufufuo

30 Wakaondoka huko, wakapitia Galilaya. Yesu hakutaka mtu ye yote afahamu mahali walipo,

31 kwa maana alikuwa anawafundisha wanafunzi wake. Akawaambia, “Mwana wa Adamu atasalitiwa na kutiwa mikononi mwa watu nao watamwua, naye siku tatu baada ya kuuawa atafufuka.”

32 Lakini wao hawakuelewa kile alichokuwa akisema, nao waliogopa kumwuliza.

Mabishano Kuhusu Aliye Mkuu Zaidi Ya Wote

33 Basi wakafika Kapernaumu na baada ya kuingia nyumbani akawauliza, “Mlikuwa mnabishana nini kule njiani?”

34 Lakini hawakumjibu, kwa sababu njiani walikuwa wakibishana kuhusu nani miongoni mwao aliyekuwa mkuu zaidi ya wote.

35 Akaketi, akawaita wote kumi na wawili akawaambia: “Kama mtu ye yote akitaka kuwa wa kwanza hana budi kuwa wa mwisho na mtumishi wa wote.”

36 Kisha akamchukua mtoto mdogo akamsimamisha katikati yao, akamkumbatia, akawaambia,

37 “Mtu ye yote amkaribishaye mmoja wa hawa watoto wadogo, kwa Jina langu anikaribisha mimi. Naye anikaribishaye mimi, amkaribisha Baba yangu aliyenituma.”

Ye Yote Asiye Kinyume Nasi Yuko Upande Wetu

38 Yohana akamwambia, “Mwalimu, tumemwona mtu akitoa pepo wachafu kwa jina lako nasi tukamkataza kwa sababu yeye si mmoja wetu.”

39 Yesu akasema, “Msimkataze, hakuna ye yote atendaye miujiza kwa Jina langu ambaye baada ya kitambo kidogo aweza kunena lo lote baya dhidi yangu.

40 Kwa maana ye yote asiye kinyume chetu yuko upande wetu.

41 Amin, amin nawaambia, ye yote awapaye ninyi kikombe cha maji kwa Jina langu kwa sababu ninyi ni mali ya Kristo, hakika hataikosa thawabu yake.”

Kusababisha Kutenda Dhambi

42 “Kama mtu ye yote akimsababisha mmojawapo wa wadogo hawa wanaoniamini kutenda dhambi, ingekuwa afadhali mtu huyo afungiwe shingoni mwake jiwe kubwa la kusagia na kutoswa baharini.

43 Kama mkono wako ukikusababisha kutenda dhambi, ukate. Ni afadhali kuingia katika uzima ukiwa na mkono mmoja kuliko kuwa na mikono miwili ukaingia jehanamu mahali ambako moto hauzimiki.

44 [Mahali ambako funza wake hawafi wala moto wake hauzimiki].

45 Kama mguu wako ukikusababisha kutenda dhambi, ukate. Ni afadhali kuingia katika uzima ukiwa kilema kuliko kuwa na miguu miwili ukaingia jehanamu mahali ambako moto hauzimiki.

46 [Mahali ambako funza wake hawafi wala moto hauzimiki.]

47 Nalo jicho lako likikusababisha kutenda dhambi, ling’oe. Ni afadhali kuwa chongo ukaingia katika Ufalme wa Mungu kuliko kuwa na macho mawili na ukatupwa jehanamu,

48 mahali ambako

“ ‘funza wake hawafi,

wala moto wake hauzimiki.’

49 Kila mmoja atatiwa chumvi kwa moto.

50 “Chumvi ni nzuri, lakini ikipoteza ladha yake utaifanyaje ili iweze kukolea tena? Mwe na chumvi ndani yenu, mkaishi kwa amani, kila mmoja na mwenzake.”

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/MRK/9-f009a19c2ad7844af1d3beb07da297a9.mp3?version_id=1627—

Marko 10

Mafundisho Kuhusu Talaka

1 Yesu akaondoka huko akavuka Mto wa Yordani, akaenda sehemu ya Uyahudi. Umati mkubwa wa watu ukamjia tena na kama ilivyokuwa desturi yake akawafundisha.

2 Baadhi ya Mafarisayo wakaja ili kumjaribu kwa kumwuliza, “Je, ni halali mtu kumwacha mke wake?”

3 Yesu akawajibu, “Je, Mose aliwaamuru nini?”

4 Wakajibu, “Mose aliruhusu kwamba mume anaweza kumwandikia mkewe hati ya talaka na kumwacha.”

5 Yesu akawaambia, “Mose aliwaandikia sheria hiyo kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu.

6 Lakini tangu mwanzo wa uumbaji, ‘Mungu aliwaumba mume na mke.

7 Kwa sababu hii mwanaume atamwacha baba yake na mama yake na kuambatana na mkewe na hao wawili, watakuwa mwili mmoja.’

8 Kwa hiyo hawatakuwa wawili tena bali mwili mmoja.

9 Basi, alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe.”

10 Walipokuwa tena ndani ya nyumba, wanafunzi wake wakamwuliza kuhusu jambo hili.

11 Akawajibu, “Mtu ye yote anayemwacha mkewe na kuoa mke mwingine, azini naye.

12 Naye mwanamke anayemwacha mumewe na kuolewa na mume mwingine, anazini.”

Yesu Anawabariki Watoto Wadogo

13 Watu walikuwa wakimletea Yesu watoto wadogo ili awaguse lakini wanafunzi wake wakawakemea.

14 Yesu alipoona yaliyokuwa yakitukia akachukizwa, akawaambia wanafunzi wake, “Waacheni watoto wadogo waje kwangu, wala msiwazuie, kwa maana Ufalme wa Mungu ni wa watu kama hawa.

15 Amin, amin nawaambia, mtu ye yote asiyeukubali Ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo, hatauingia kamwe.”

16 Akawachukua watoto mikononi mwake, akawakumbatia, akaweka mikono yake juu yao, akawabariki.

Kijana Tajiri

17 Yesu alipokuwa anaondoka, mtu mmoja akamkimbilia, akapiga magoti mbele yake, akamwuliza, “Mwalimu mwema, nifanye nini ili niurithi uzima wa milele?”

18 Yesu akamwambia, “Mbona unaniita mwema? Hakuna aliye mwema isipokuwa Mungu peke yake.

19 Unazijua amri: ‘Usiue, usizini, usiibe, usishuhudie uongo, usidanganye, waheshimu baba yako na mama yako.’ ”

20 Akamjibu, “Mwalimu, amri hizi zote nimezishika tangu nikiwa mtoto.”

21 Yesu akamtazama na kumpenda, akamwambia, “Umepungukiwa na kitu kimoja, nenda ukauze kila kitu ulicho nacho uwape maskini hizo fedha, nawe utakuwa na hazina mbinguni. Kisha njoo, unifuate.”

22 Yule mtu aliposikia hayo, akasikitika sana, akaondoka kwa huzuni kwa sababu alikuwa na mali nyingi.

23 Yesu akatazama pande zote, akawaambia wanafunzi wake, “Itakuwa vigumu sana kwa wenye mali kuingia kwenye Ufalme wa Mungu!”

24 Wanafunzi wake wakashangazwa sana na maneno hayo. Lakini Yesu akawaambia tena, “Wanangu, tazama jinsi ilivyo vigumu kwa wale wanaotumainia mali kuingia katika Ufalme wa Mungu.

25 Ni rahisi zaidi kwa ngamia kupita kwenye tundu la sindano kuliko tajirikuingia katika Ufalme wa Mungu.”

26 Wanafunzi wake wakashangaa mno. Wakaulizana wao kwa wao, “Ni nani basi awezaye kuokolewa?”

27 Yesu akawatazama, akawaambia, “Kwa mwanadamu hili haliwezekani, lakini kwa Mungu sivyo. Yote kwa Mungu yanawezekana.”

28 Petro akaanza kumwambia, “Tazama, tumeacha kila kitu na kukufuata wewe!”

29 Yesu akasema, “Amin, nawaambia, hakuna mtu ye yote aliyeacha nyumba, ndugu wa kiume, au ndugu wa kike, mama, baba, watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya Injili,

30 ambaye hatalipwa mara mia katika ulimwengu huu, nyumba, ndugu wa kiume, ndugu wa kike, mama, baba, watoto, mashamba pamoja na mateso, kisha uzima wa milele katika ulimwengu ujao.

31 Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho na wa mwisho watakuwa wa kwanza.”

Yesu Atabiri Mara Ya Tatu Kufa Na Kufufuka Kwake

32 Walikuwa njiani wakipanda kwenda Yerusalemu na Yesu alikuwa ametangulia. Wanafunzi wake walishangaa, nao watu waliowafuata walijawa na hofu. Yesu akawachukua tena wale wanafunzi wake kumi na wawili kando na kuwaambia yatakayompata.

33 Akasema, “Tunapanda kwenda Yerusalemu, na Mwana wa Adamu atasalitiwa kwa viongozi wa makuhani na walimu wa sheria. Wao watamhukumu kifo na kumtia mikononi mwa watu Mataifa,

34 ambao watamdhihaki, watamtemea mate, watampiga na kumwua. Siku tatu baada ya kifo chake atafufuka.”

Ombi La Yakobo Na Yohana

35 Kisha Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo, wakaja mbele alikokuwa na kumwambia, “Mwalimu, tunataka utufanyie lo lote tutakalokuomba.”

36 Naye akawaambia, “Je, mwataka niwafanyie jambo gani?”

37 Wakamwambia, “Tupe kukaa mmoja upande wako wa kuume na mwingine upande wako wa kushoto katika utukufu wako.”

38 Lakini Yesu akawaambia, “Hamjui mnaloliomba. Je, mnaweza kukinywea kikombe ninyweacho mimi, au kubatizwa ubatizo nibatizwao mimi?”

39 Wakajibu, “Tunaweza.”

Kisha Yesu akawaambia, “Kikombe nikinyweacho mtakinywea na ubatizo nibatizwao mtabatizwa,

40 lakini kuketi mkono wangu wa kuume au wa kushoto si juu yangu mimi kuwapa. Nafasi hizi ni kwa ajili ya wale walioandaliwa.”

41 Wale wanafunzi wengine kumi waliposikia hayo wakaanza kuwakasirikia Yakobo na Yohana.

42 Yesu akawaita wanafunzi wake pamoja akawaambia, “Mnafahamu kuwa watawala wa watu Mataifa huwatawala watu kwa nguvu, nao wenye vyeo huwaonyesha mamlaka yao.

43 Lakini sivyo kwenu. Badala yake ye yote anayetaka kuwa mkuu miongoni mwenu hana budi kuwa mtumishi wenu

44 na ye yote anayetaka kuwa wa kwanza, hana budi kuwa mtumwa wa wote.

45 Kwa kuwa hata Mwana wa Adamu hakuja kutumikiwa, bali kutumika na kuutoa uhai wake kuwa ukombozi kwa ajili ya wengi.”

Yesu Amponya Kipofu Bartimayo

46 Kisha wakafika Yeriko. Wakati Yesu alipokuwa akiondoka mjini na wanafunzi wake pamoja na umati mkubwa wa watu, kipofu mmoja, jina lake Bartimayo, mwana wa Timayo, alikuwa ameketi kando ya njia akiomba msaada.

47 Aliposikia kuwa ni Yesu wa Nazareti aliyekuwa anapita, akaanza kupaza sauti akisema, “Yesu, Mwana wa Daudi, unihurumie!”

48 Watu wengi wakamkemea, wakamwambia akae kimya, lakini yeye akazidi kupaza sauti akisema, “Mwana wa Daudi, unihurumie!”

49 Yesu akasimama na kusema, “Mwiteni.”

Hivyo wakamwita yule mtu kipofu wakamwambia, “Jipe moyo! Inuka, anakuita.”

50 Akiwa analivua lile joho lake, alisimama na kumwendea Yesu.

51 Yesu akamwuliza, “Unataka nikufanyie nini?”

Yule kipofu akajibu, “Mwalimu, nataka kuona.”

52 Yesu akamwambia, “Nenda zako, imani yako imekuponya.” Mara akapata kuona, akamfuata Yesu njiani.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/MRK/10-ad18ee103ff7a732e1668087d6d415de.mp3?version_id=1627—

Marko 11

Yesu Aingia Yerusalemu Kwa Shangwe

1 Walipokaribia Yerusalemu, wakafika Bethfage na Bethania katika Mlima wa Mizeituni, Yesu akawatuma wawili wa wanafunzi wake,

2 akiwaambia, “Nendeni kwenye kijiji kilichoko mbele yenu na mara mwingiapo kijijini, mtakuta mwana punda amefungwa, ambaye hajapandwa na mtu ye yote. Mfungueni, mkamlete hapa.

3 Kama mtu ye yote akiwauliza, ‘Mbona mnamfungua?’ Mwambieni, ‘Bwana anamhitaji na atamrudisha hapa baada ya muda mfupi.’ ”

4 Wakaenda, wakamkuta mwana punda amefungwa kando ya barabara, karibu na mlango wa nyumba.

5 Walipokuwa wanamfungua, watu waliokuwa wamesimama karibu wakawauliza, “Mna maana gani mnapomfungua huyo mwana punda?”

6 Wakawajibu kama vile Yesu alivyokuwa amewaagiza, nao wale watu wakawaruhusu.

7 Kisha wakamleta huyo mwana punda kwa Yesu na kutandika mavazi yao juu yake, naye akampanda.

8 Watu wengi wakatandaza mavazi yao barabarani na wengine wakatandaza matawi waliyokuwa wamekata mashambani.

9 Kisha wale waliokuwa wametangulia mbele na wale waliokuwa wakifuata nyuma wakapaza sauti, wakisema,

# “Hosana!”

“Amebarikiwa yeye ajaye kwa jina la Bwana!

10 “Umebarikiwa Ufalme unaokuja wa baba yetu Daudi!”

“Hosana kwake yeye aliye juu!”

11 Yesu akaingia Yerusalemu na kwenda Hekaluni. Akaangalia kila kitu kilichokuwemo, lakini kwa kuwa ilishakuwa jioni, akaenda zake Bethania pamoja na wale kumi na wawili.

Yesu Alaani Mtini Usiozaa

12 Kesho yake walipokuwa wakitoka Bethania, Yesu alikuwa na njaa.

13 Alipouona mtini kwa mbali, akaenda ili aone kama ulikuwa na matunda. Alipoufikia, akakuta una majani tu, kwa kuwa hayakuwa majira ya tini.

14 Yesu akauambia ule mti, “Tangu leo mtu ye yote na asile kamwe matunda kutoka kwako.” Wanafunzi wake walimsikia akisema hayo.

Yesu Atakasa Hekalu

15 Walipofika Yerusalemu, Yesu akaingia Hekaluni akaanza kuwafukuza wale waliokuwa wananunua na kuuza humo ndani. Akapindua meza za wale waliokuwa wakibadilisha fedha na viti vya wale waliokuwa wakiuza njiwa,

16 wala hakumruhusu mtu ye yote kuchukua bidhaa kupitia ukumbi wa Hekalu.

17 Naye alipokuwa akiwafundisha, akasema, “Je, haikuandikwa kuwa:

“ ‘Nyumba yangu itaitwa

nyumba ya sala kwa mataifa yote’?

Lakini ninyi mmeifanya kuwa ‘pango la wanyang’anyi.’ ”

18 Viongozi wa makuhani na walimu wa sheria wakapata habari hizi, nao wakaanza kutafuta njia ya kumwua, kwa kuwa walikuwa wakimwogopa, kwa sababu umati wote wa watu walikuwa wanashangazwa na mafundisho yake.

19 Ilipofika jioni, Yesu na wanafunzi wake wakatoka nje ya mji.

Mtini Ulionyauka

20 Asubuhi yake, walipokuwa wakipita, wakauona ule mtini umenyauka kutoka juu hadi kwenye mizizi yake.

21 Petro akakumbuka na kumwambia Yesu, “Mwalimu, tazama! Ule mtini ulioulaani umenyauka!”

22 Yesu akawajibu akawaambia, “Mwaminini Mungu.

23 Amin, amin nawaambia, mtu ye yote atakayeuambia mlima huu, ‘Ng’oka ukatupwe baharini,’ wala asione shaka moyoni mwake, bali aamini kwamba hayo asemayo yametukia, yatakuwa yake.

24 Kwa sababu hiyo nawaambia, yo yote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mmeyapokea nayo yatakuwa yenu.

25 Nanyi kila msimamapo kusali, sameheni, mkiwa na neno na mtu ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu.

26 Lakini kama ninyi msiposamehe, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu.”

Wauliza Kuhusu Mamlaka Ya Yesu

27 Wakafika tena Yerusalemu, wakati Yesu akitembea Hekaluni, viongozi wa makuhani, walimu wa sheria pamoja na wazee wakamjia.

28 Wakamwuliza, “Unafanya mambo haya kwa mamlaka gani? Naye ni nani aliyekupa mamlaka ya kufanya hayo?”

29 Yesu akawajibu, “Nitawauliza swali moja. Nijibuni, nami nitawaeleza ni kwa mamlaka gani ninafanya mambo haya.

30 Niambieni, ubatizo wa Yohana ulitoka mbinguni au kwa wanadamu?”

31 Wakasemezana wao kwa wao, wakisema, “Kama tukisema, ‘Ulitoka mbinguni,’ atatuuliza, ‘Mbona hamkumwamini?’

32 Lakini tukisema, ‘Ulitoka kwa wanadamu,’…” (Waliwaogopa watu, kwa sababu kila mtu aliamini kwamba Yohana alikuwa nabii kweli kweli.)

33 Kwa hiyo wakamjibu Yesu, “Hatujui.”

Naye Yesu akawaambia, “Wala mimi sitawaambia ni kwa mamlaka gani ninafanya mambo haya.”

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/MRK/11-6f63ade6f661027e9f142c452ec6d12a.mp3?version_id=1627—

Marko 12

Mfano Wa Wapangaji Waovu

1 Yesu akaanza kusema nao kwa mifano, akawaambia: “Mtu mmoja alipanda shamba la mizabibu. Akajenga ukuta kulizunguka, akachimba shimo ndani yake kwa ajili ya shinikizo la kusindika divai, akajenga mnara wa ulinzi. Akalikodisha shamba hilo kwa wakulima, kisha akasafiri kwenda nchi nyingine.

2 Wakati wa mavuno ulipofika, mwenye shamba akamtuma mtumishi wake kwa hao wakulima ili kuchukua sehemu yake ya mavuno kutoka kwa hao wapangaji.

3 Lakini wale wakulima walimkamata yule mtumishi, wakampiga, wakamfukuza mikono mitupu.

4 Kisha yule mwenye shamba akamtuma mtumishi mwingine kwao, wale wakulima wakampiga kichwani na kumfanyia mambo ya aibu.

5 Kisha akatuma mtumishi mwingine, huyu wakamwua. Akatuma wengine wengi, baadhi yao wale wakulima wakawapiga na wengine wakawaua.

6 “Mwenye shamba alikuwa amebakiwa na mmoja wa kumtuma, huyu ni mwanawe mpendwa. Hatimaye akamtuma akisema, ‘Watamheshimu mwanangu.’

7 “Lakini wale wapangaji wakasemezana wao kwa wao, wakisema, ‘Huyu ndiye mrithi, njoni tumwue, nao urithi utakuwa wetu.’

8 Hivyo wakamkamata, wakamwua na kumtupa nje ya lile shamba la mizabibu.

9 “Mnadhani yule mwenye shamba atafanya nini? Atakuja na kuwaua hao wapangaji, kisha atawapa wapangaji wengine hilo shamba la mizabibu.

10 Je, hamjasoma maandiko haya:

“ ‘Jiwe lile walilolikataa waashi

limekuwa jiwe kuu la pembeni;

11 Bwana amefanya jambo hili,

nalo ni ajabu machoni petu’?”

12 Walipotambua kuwa amesema mfano huu kwa ajili yao wakataka kumkamata, lakini wakaogopa ule umati wa watu. Wakamwacha wakaondoka, wakaenda zao.

Swali Kuhusu Kulipa Kodi

13 Baadaye wakawatuma baadhi ya Mafarisayo na Maherode ili kuja kumtega Yesu katika yale anayosema.

14 Wakamjia, wakamwambia, “Mwalimu, tunajua ya kuwa wewe ni mtu mwadilifu. Wewe huyumbishwi na wanadamu, kwa kuwa hujali kwamba wao ni nani. Lakini wewe hulifundisha neno la Mungu sawasawa na kweli. Je, ni haki kumlipa Kaisari kodi au la?

15 Je, tulipe kodi au tusilipe?”

# Lakini Yesu alijua unafiki wao. Akawauliza “Mbona mnajaribu kunitega? Nileteeni hiyo dinariniione.”

16 Wakamletea hiyo sarafu. Naye akawauliza, “Picha hii ni ya nani na maandishi haya ni ya nani?”

Wakamjibu, “Ni ya Kaisari.”

17 Ndipo Yesu akawaambia, “Mpeni Kaisari kilicho cha Kaisari, na kilicho cha Mungu mpeni Mungu.”

Nao wakamstaajabia sana.

Ndoa Wakati Wa Ufufuo

18 Kisha Masadukayo, wale wasemao kuwa hakuna ufufuo wakamjia Yesu,

19 wakasema, “Mwalimu, Mose alituandikia kuwa kama ndugu wa mtu akifa na kumwacha mkewe bila mtoto, basi ndugu yake atamwoa huyo mjane ili amzalie ndugu yake watoto.

20 Basi walikuwapo ndugu saba. Yule wa kwanza akaoa na akafa pasipo kuwa na mtoto ye yote.

21 Wa pili akamwoa yule mjane, lakini naye akafa bila kuacha mtoto ye yote. Ikawa vivyo hivyo kwa yule wa tatu.

22 Hakuna hata mmojawapo wa hao ndugu wote saba aliyeacha mtoto. Hatimaye yule mwanamke naye akafa.

23 Kwa hiyo wakati wa ufufuo, watakapofufuka wote, huyo atakuwa mke wa nani maana aliolewa na ndugu wote saba?”

24 Yesu akawajibu, “Je, hampotoki kwa sababu hamjui maandiko wala uweza wa Mungu?

25 Wafu watakapofufuka, hawataoa wala kuolewa, watakuwa kama malaika wa mbinguni.

26 Basi kuhusu ufufuo wa wafu: Je, hamjasoma katika kitabu cha Mose jinsi Mungu alivyosema na Mose kutoka katika kile kichaka akisema, ‘Mimi, ni Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaki na Mungu wa Yakobo?’

27 Mungu si Mungu wa wafu, bali ni Mungu wa walio hai. Kwa hiyo mmekosea kabisa.”

Amri Iliyo Kuu

28 Mwalimu mmoja wa sheria akaja akawasikia wakijadiliana. Akiona kwamba Yesu amewajibu vyema, naye akamwuliza, “Katika amri zote, ni ipi iliyo kuu?”

29 Yesu akajibu, “Amri iliyo kuu ndiyo hii, ‘Sikia Ee Israeli, Bwana Mungu wetu, Bwana ndiye mmoja.

30 Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa roho yako yote, kwa akili zako zote na kwa nguvu zako zote.’

31 Ya pili ndiyo hii: ‘Mpende jirani yako kama nafsi yako.’ Hakuna amri nyingine iliyo kuu kuliko hizi.”

32 Yule mwalimu wa sheria akamwambia Yesu, “Mwalimu, umejibu vyema kwamba Mungu ni mmoja wala hakuna mwingine ila yeye.

33 Kumpenda Mungu kwa moyo wote na kwa akili zote na kwa nguvu zote na kumpenda jirani kama mtu anavyojipenda mwenyewe ni bora zaidi kuliko kutoa sadaka ya kuteketezwa na dhabihu.”

34 Yesu alipoona kwamba amejibu kwa busara, akamwambia, “Wewe hauko mbali na Ufalme wa Mungu.” Tangu wakati huo, hakuna mtu ye yote aliyethubutu kumwuliza maswali tena.

Kristo Ni Mwana Wa Nani?

35 Wakati Yesu alipokuwa akifundisha Hekaluni, akauliza, “Imekuwaje walimu wa sheria wanasema kwamba Kristoni Mwana wa Daudi?

36 Kwa maana Daudi mwenyewe akinena kwa kuongozwa na Roho Mtakatifu alisema:

“ ‘BWANA alimwambia Bwana wangu:

“Keti mkono wangu wa kuume,

hadi nitakapowaweka adui zako

chini ya miguu yako.” ’

37 Kwa hiyo Daudi mwenyewe anamwita ‘Bwana.’ Awezaje basi yeye kuwa mwanawe?”

Ule umati wote wa watu wakamsikiliza kwa furaha.

Yesu Awatahadharisha Watu Kuhusu Walimu Wa Sheria

38 Alipokuwa akifundisha, Yesu alisema, “Jihadharini na walimu wa sheria. Wao hupenda kutembea wakiwa wamevaa mavazi marefu na kusalimiwa kwa heshima masokoni.

39 Pia wao hupenda kukaa kwenye viti vya mbele katika masinagogi na kupewa nafasi za heshima katika karamu.

40 Wao hula nyumba za wajane na ili waonekane kuwa wema wanasali sala ndefu. Watapata adhabu iliyo kuu sana.”

Sadaka Ya Mjane

41 Kisha Yesu akaketi mkabala na sehemu sadaka zilikokuwa zinawekwa na kuangalia umati wa watu wakati wakitoa fedha zao kwenye hazina ya Hekalu. Matajiri wengi wakaweka kiasi kikubwa cha fedha.

42 Lakini mjane mmoja maskini akaja na kuweka sarafu mbili ndogo za shaba zenye thamani ya senti mbili.

43 Yesu akawaita wanafunzi wake akawaambia, “Amin, amin, nawaambia, huyu mjane maskini ametoa zaidi katika hazina kuliko wengine wote.

44 Wengine wote wametoa kutokana na ziada ya mali zao, lakini huyu mjane kutokana na umaskini wake, ametoa kila kitu alichokuwa nacho, hata kile alichohitaji ili kuishi.”

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/MRK/12-871221fbc07c33e442e245a59b0b988e.mp3?version_id=1627—

Marko 13

Dalili Za Siku Za Mwisho

1 Wakati Yesu alipokuwa akitoka Hekaluni, mmojawapo wa wanafunzi wake akamwambia, “Mwalimu! Tazama jinsi mawe haya yalivyo makubwa na majengo haya yalivyo mazuri!”

2 Ndipo Yesu akajibu akasema, “Je, unayaona majengo haya yalivyo makubwa? Hakuna hata jiwe moja litakalobaki juu ya jingine, yote yatabomolewa.”

3 Yesu alipokuwa ameketi kwenye Mlima wa Mizeituni mkabala na Hekalu, Petro, Yakobo, Yohana na Andrea wakamwuliza faraghani,

4 “Tafadhali tuambie, mambo haya yatatukia lini? Nayo ni nini ishara ya wakati hayo yote yanapokaribia kutimia?”

5 Yesu akawaambia: “Jihadharini mtu ye yote asiwadanganye.

6 Wengi watakuja kwa Jina langu wakidai, ‘Mimi ndiye,’ nao watawadanganya wengi.

7 Msikiapo habari za vita na uvumi wa vita, msiwe na hofu. Mambo haya hayana budi kutukia, lakini ule mwisho bado.

8 Taifa litainuka dhidi ya taifa na ufalme dhidi ya ufalme. Kutakuwa na matetemeko sehemu mbalimbali na njaa. Huu ndio mwanzo wa utungu.

Mateso Yatabiriwa

9 “Lakini ninyi jihadharini. Kwa maana watawapeleka mahakamani na kuwapiga mijeledi katika masinagogi. Mtashtakiwa mbele ya watawala na wafalme kwa ajili yangu, ili kuwa ushuhuda kwao.

10 Nayo habari njema lazima ihubiriwe kwanza kwa mataifa yote kabla ule mwisho haujawadia.

11 Mtakapokamatwa na kushtakiwa, msisumbuke kuhusu mtakalosema. Semeni tu lo lote mtakalopewa wakati huo, kwa kuwa si ninyi msemao bali ni Roho Mtakatifu.

12 “Ndugu atamsaliti ndugu yake ili auawe, baba atamsaliti mwanawe. Watoto watawaasi wazazi wao na kusababisha wauawe.

13 Watu wote watawachukia kwa ajili ya Jina langu, lakini atakayevumilia hata mwisho ataokoka.

Chukizo La Uharibifu

14 “Mtakapoona chukizo la uharibifu limesimama mahali pasipolipasa (asomaye na afahamu), basi wale walioko Uyahudi na wakimbilie milimani.

15 Yeye aliyeko juu ya dari ya nyumba asishuke au kuingia ndani ili kuchukua kitu cho chote.

16 Aliye shambani asirudi nyumbani kuchukua vazi lake.

17 Ole wao wenye mimba na wale wanaonyonyesha watoto siku hizo!

18 Ombeni mambo haya yasitokee wakati wa baridi.

19 Kwa maana siku hizo itakuwako dhiki kuu ambayo haijapata kuwako tangu mwanzo wa uumbaji, hapo Mungu alipoumba ulimwengu mpaka leo na wala haitakuwako tena kamwe.

20 Kama Bwana asingelifupiza siku hizo, kamwe asingeliokoka mtu ye yote, lakini kwa ajili ya wateule, wale aliowachagua, amezifupiza siku hizo.

21 Wakati huo mtu ye yote akiwaambia, ‘Tazama, Kristohuyu hapa!’ au, ‘Tazama, yuko kule,’ msiamini.

22 Kwa maana watatokea makristo wa uongo na manabii wa uongo, nao watafanya ishara na maajabu ili kuwapotosha, ikiwezekana hata wale wateule.

23 Hivyo jihadharini, nimekwisha kuwaambia mambo haya yote mapema kabla hayajatukia.

Kuja Kwa Mwana Wa Adamu

24 “Lakini katika siku hizo, baada ya hiyo dhiki,

“ ‘jua litatiwa giza

na mwezi hautatoa nuru yake;

25 nyota zitaanguka kutoka angani,

nazo nguvu za anga zitatikisika.’

26 “Ndipo watu wote watakapomwona Mwana wa Adamu akija mawinguni kwa nguvu nyingi na utukufu.

27 Naye atawatuma malaika zake wawakusanye wateule wake kutoka pande zote nne za dunia, kutoka miisho ya dunia hadi miisho ya mbingu.

Somo Kuhusu Mtini

28 “Basi jifunzeni somo hili kutokana na mtini: Mara mwonapo matawi yake yakichipua na kutoa majani, mnajua kwamba wakati wa kiangazi umekaribia.

29 Vivyo hivyo, myaonapo mambo haya yakitukia, tambueni kwamba Kristo yu karibu malangoni.

30 Amin, amin nawaambia, kizazi hiki hakitapita hadi mambo haya yote yametukia.

31 Mbingu na nchi zitapita, lakini maneno yangu hayatapita kamwe.

Hakuna Ajuaye Siku Wala Saa

32 “Lakini kwa habari ya siku ile na saa hakuna ye yote ajuaye, hata malaika walioko mbinguni wala Mwana hajui, ila Baba peke yake.

33 Jihadharini! Kesheni! Kwa maana hamjui wakati ule utakapowadia.

34 Ni kama mtu anayesafiri akiiacha nyumba yake na kuwaachia watumishi wake kuiangalia, kila mtu na kazi yake, kisha akamwambia yule bawabu aliye mlangoni akeshe.

35 “Basi kesheni kwa sababu hamjui ni lini mwenye nyumba atakaporudi, iwapo ni jioni, au kwamba ni usiku wa manane, au alfajiri awikapo jogoo, au wakati wa mapambazuko.

36 Kama akija ghafula, asije akawakuta mmelala.

37 Lile ninalowaambia ninyi, nawaambia watu wote: ‘Kesheni!’ ”

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/MRK/13-50067f3d3b3fd092b326b47433d9b7f4.mp3?version_id=1627—

Marko 14

Shauri La Kumwua Yesu

1 Zilikuwa zimebaki siku mbili tu kabla ya Sikukuu ya Pasaka na Sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu. Viongozi wa makuhani na walimu wa sheria walikuwa wakitafuta njia ya kumkamata Yesu kwa hila na kumwua,

2 kwa kuwa walisema, “Tusilifanye jambo hili wakati wa Sikukuu, maana watu wanaweza wakafanya ghasia.”

Yesu Kupakwa Mafuta Huko Bethania

3 Yesu alipokuwa huko Bethania nyumbani kwa Simoni aliyekuwa na ukoma, wakati alipokuwa ameketi mezani akila chakula cha jioni, mwanamke mmoja aliingia akiwa na chupa ya marhamu yenye manukato ya nardosafi ya thamani kubwa. Akaivunja hiyo chupa, akamiminia hayo manukato kichwani mwa Yesu.

4 Baadhi ya watu waliokuwapo pale walikuwa wakisemezana wao kwa wao, “Kwa nini ubadhirifu huu wa manukato?

5 Mafuta haya yangeweza kuuzwa kwa zaidi ya dinari300 na fedha hizo wakapewa maskini.” Wakamkemea vikali huyo mwanamke.

6 Lakini Yesu akawaambia, “Kwa nini mnamsumbua? Mwacheni! Amenitendea jambo la kupendeza.

7 Maskini mnao pamoja nanyi siku zote na mnaweza kuwasaidia wakati wo wote mnaotaka. Lakini mimi hamko nami daima.

8 Huyu mwanamke amenitendea lile aliloweza. Ameutia mwili wangu manukato kuniandaa kwa maziko yangu.

9 Amin, amin nawaambia, mahali po pote duniani ambapo Injili itahubiriwa, jambo hili alilotenda huyu mwanamke litatajwa kwa ukumbusho wake.”

Yuda Akubali Kumsaliti Yesu

10 Kisha Yuda Iskariote, mmoja wa wale wanafunzi kumi na wawili wa Bwana Yesu, akaenda kwa viongozi wa makuhani ili kumsaliti Yesu kwao.

11 Walifurahi sana kusikia jambo hili na wakaahidi kumpa fedha. Hivyo yeye akawa anatafuta wasaa mzuri wa kumtia Yesu mikononi mwao.

Yesu Ala Pasaka Na Wanafunzi Wake

12 Siku ya kwanza ya Sikukuu ya Mikate Isiyotiwa Chachu, siku ambayo kwa desturi kondoo wa Pasaka huchinjwa, wanafunzi wa Yesu wakamwuliza, “Unataka tuende wapi ili tukuandalie mahali pa kula Pasaka?”

13 Basi akawatuma wawili miongoni mwa wanafunzi wake, akawaambia, “Nendeni mjini, huko mtakutana na mwanaume amebeba mtungi wa maji. Mfuateni.

14 Mwambieni mwenye nyumba ile atakayoingia, ‘Mwalimu anauliza, kiko wapi chumba changu kwa ajili ya wageni ambamo nitakula Pasaka pamoja na wanafunzi wangu?’

15 Atawaonyesha chumba kikubwa ghorofani, kilichopambwa tena kilicho tayari. Tuandalieni humo.”

16 Wale wanafunzi wakaondoka na kwenda mjini, nao wakakuta kila kitu kama alivyowaambia. Hivyo wakaandaa chakula cha Pasaka.

17 Ilipofika jioni, Yesu akaja pamoja na wale wanafunzi wake kumi na wawili.

18 Walipokwisha kuketi kwenye nafasi zao, wakati wakila Yesu akawaambia, “Amin, nawaambia, mmoja wenu atanisaliti, yaani, yeye anayekula pamoja nami.”

19 Wakaanza kuhuzunika na kumwambia mmoja baada ya mwingine, “Je, ni mimi Bwana?”

20 Akawajibu, “Ni mmoja miongoni mwenu ninyi kumi na wawili, yule anayechovya mkate kwenye bakuli pamoja nami.

21 Kwa kuwa Mwana wa Adamu yu aenda zake kama vile alivyoandikiwa. Lakini ole wake mtu yule amsalitiye Mwana wa Adamu! Ingelikuwa heri kama mtu huyo asingelizaliwa.”

Kuanzishwa Kwa Meza Ya Bwana

22 Walipokuwa wakila, Yesu akachukua mkate, akashukuru, akaumega na kuwapa wanafunzi wake akisema, “Twaeni mle, huu ndio mwili wangu.”

23 Kisha akachukua kikombe, akashukuru, akawapa wanafunzi wake, wote wakanywa kutoka humo.

24 Akawaambia, “Hii ndiyo damu yangu ya Agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi.

25 Amin nawaambia, sitakunywa tena uzao wa mzabibu mpaka siku ile nitakapokunywa mpya katika Ufalme wa Mungu.”

26 Walipokwisha kuimba wimbo, wakatoka wakaenda kwenye Mlima wa Mizeituni.

Yesu Atabiri Kuwa Petro Atamkana

27 Yesu akawaambia, “Ninyi nyote mtaniacha, kwa maana imeandikwa:

“ ‘Nitampiga mchungaji,

nao kondoo watatawanyika.’

28 Lakini baada ya kufufuka, nitawatangulia kwenda Galilaya.”

29 Petro akasema, “Hata kama wengine wote watakuacha, mimi sitakuacha.”

30 Yesu akamwambia, “Amin, nakuambia; leo, usiku huu, kabla jogoo hajawika mara mbili, utanikana mara tatu.”

31 Lakini Petro akasisitiza akasema, “Hata kama inanipasa kufa pamoja nawe, sitakukana.” Nao wale wanafunzi wengine wote wakasema vivyo hivyo.

Yesu Akiomba Bustanini Gethsemane

32 Wakaenda mahali paitwapo Gethsemane, Yesu akawaambia wanafunzi wake, “Kaeni hapa wakati ninakwenda kule kuomba.”

33 Kisha akawachukua pamoja naye Petro, Yakobo na Yohana. Naye akaanza kuhuzunika sana na kutaabika.

34 Akawaambia, “Moyo wangu umejawa na huzuni kiasi cha kufa. Kaeni hapa na mkeshe.”

35 Akaenda mbele kidogo, akajitupa chini kifudifudi akaomba akisema, kama ikiwezekana saa hiyo ya mateso imwepuke.

36 Akasema, “Abba, Baba, mambo yote yawezekana kwako. Niondolee kikombe hiki, lakini si kama nitakavyo mimi, bali mapenzi yako yatimizwe.”

37 Akarudi kwa wanafunzi wake akawakuta wamelala, naye akamwambia Petro, “Simoni, umelala? Je, hukuweza kukesha hata kwa saa moja?

38 Kesheni na kuomba msije mkaingia majaribuni. Roho iko radhi lakini mwili ni dhaifu.”

39 Akaenda tena kuomba akisema maneno yale yale.

40 Aliporudi kwa wanafunzi wake, akawakuta tena wamelala, kwa sababu macho yao yalikuwa mazito. Nao hawakujua la kumwambia.

41 Akaja mara ya tatu, akawaambia, “Bado mmelala na kupumzika? Imetosha! Saa imewadia. Tazama, Mwana wa Adamu anasalitiwa mikononi mwa wenye dhambi.

42 Amkeni! Twendeni zetu! Tazameni, msaliti wangu yuaja!”

Yesu Akamatwa

43 Yesu alipokuwa bado anazungumza, Yuda, mmoja wa wale wanafunzi kumi na wawili, akatokea akiwa pamoja na umati wa watu wenye panga na marungu, waliokuwa wametumwa na viongozi wa makuhani, walimu wa sheria na wazee.

44 Basi Yuda, yule msaliti, alikuwa amewapa ishara wale watu kuwa: “Yule nitakayembusu, ndiye, mkamateni na mchukueni akiwa chini ya ulinzi.”

45 Kwa hiyo Yuda alipofika, akamwendea Yesu akamwambia, “Rabi”na kumbusu.

46 Wale watu wakamkamata Yesu, wakamweka chini ya ulinzi.

47 Ndipo mmoja wa wale waliokuwa wamesimama karibu akachomoa upanga wake na kumpiga mtumishi wa Kuhani Mkuu, akamkata sikio.

48 Kisha Yesu akawaambia, “Mmekuja mkiwa na panga na marungu kana kwamba mimi ni mnyang’anyi?

49 Siku zote nilikuwa pamoja nanyi nikifundisha Hekaluni, wala hamkunikamata. Lakini maandiko na yatimie.”

50 Ndipo wanafunzi wake wote wakamwacha, wakakimbia.

51 Kijana mmoja, ambaye hakuwa amevaa kitu isipokuwa alijitanda nguo ya kitani, alikuwa akimfuata Yesu. Wakamkamata,

52 akakimbia uchi, akaliacha vazi lake.

Yesu Mbele Ya Baraza

53 Wakampeleka Yesu kwa Kuhani Mkuu, nao viongozi wa makuhani, wazee na walimu wa sheria wakakusanyika pamoja.

54 Petro akamfuata kwa mbali, mpaka kwenye ua wa Kuhani Mkuu. Huko akaketi pamoja na walinzi, akiota moto.

55 Viongozi wa makuhani na wajumbe wote wa Barazawalikuwa wanatafuta ushahidi dhidi ya Yesu ili wapate kumwua, lakini hawakupata.

56 Wengi wakatoa ushahidi wa uongo dhidi yake, lakini maelezo yao hayakukubaliana.

57 Ndipo wengine wakasimama wakatoa ushahidi wa uongo dhidi yake, wakisema,

58 “Sisi tulimsikia akisema, ‘Mimi nitalibomoa Hekalu hili lililojengwa na wanadamu na katika siku tatu nitajenga jingine ambalo halikujengwa na wanadamu.’ ”

59 Lakini hata hivyo, ushahidi wao haukukubaliana.

60 Kuhani Mkuu akasimama mbele ya hilo Baraza akamwuliza Yesu, “Je, wewe huwezi kujibu mashtaka haya ambayo watu hawa wameleta juu yako?”

61 Lakini Yesu akakaa kimya, hakusema neno lo lote.

# Kuhani Mkuu akamwuliza tena, “Je, wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu Mbarikiwa?”

62 Yesu akajibu, “Mimi ndimi, nanyi mtamwona Mwana wa Adamu ameketi mkono wa kuume wa Mwenye Nguvu, akija na mawingu ya mbinguni.”

63 Kuhani Mkuu akararua mavazi yake, akasema, “Tuna haja gani tena ya mashahidi zaidi?

64 Ninyi mmesikia hayo makufuru. Uamuzi wenu ni nini?”

Wote wakamhukumu kwamba anastahili kifo.

65 Kisha baadhi ya watu wakaanza kumtemea mate, wakamfunga kitambaa machoni, wakampiga kwa ngumi na kumwambia, “Tabiri ni nani aliyekupiga!” Walinzi wakamchukua na kumpiga makofi.

Petro Amkana Yesu

66 Petro alipokuwa bado yuko chini kwenye ua wa jumba la kifalme, tazama akaja mmoja wa watumishi wa kike wa Kuhani Mkuu.

67 Alipomwona Petro akiota moto, akamtazama sana, akamwambia,

“Wewe pia ulikuwa pamoja na Yesu, Mnazareti.”

68 Lakini Petro akakana, akasema, “Sijui wala sielewi unalosema.” Naye akaondoka kuelekea kwenye njia ya kuingilia.

69 Yule mtumishi wa kike alipomwona hapo mahali, akawaambia tena wale waliokuwa wamesimama hapo, “Huyu mtu ni mmoja wao.”

70 Lakini Petro akakana tena.

Baada ya muda kidogo wale waliokuwa wamesimama hapo karibu na Petro wakamwambia, “Hakika wewe ni mmoja wao, kwa maana wewe pia ni Mgalilaya!”

71 Petro akaanza kulaani na kuapa, akawaambia, “Simjui huyu mtu mnayesema habari zake.”

72 Papo hapo jogoo akawika mara ya pili. Ndipo Petro akakumbuka lile neno Yesu alilokuwa amemwambia, “Kabla jogoo hajawika mara mbili, utanikana mara tatu.” Akavunjika moyo, akalia sana.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/MRK/14-7a9efe0cc8ababf2afd3d1d15b07bf38.mp3?version_id=1627—