Wimbo Ulio Bora 1

1 Wimbo ulio Bora wa Solomoni.

Shairi La Kwanza

2 Unibusu kwa busu la kinywa chako,

kwa maana upendo wako unafurahisha kuliko divai.

3 Manukato yako yananukia vizuri,

jina lako ni kama manukato yaliyomiminwa.

Ndiyo sababu wanawali wanakupenda!

4 Nichukue twende nawe, na tufanye haraka!

Mfalme na anilete ndani ya vyumba vyake.

Tunakushangilia na kukufurahia,

tutasifu upendo wako zaidi kuliko divai.

Tazama ni jinsi gani ilivyo haki wakupende!

5 Mimi ni mweusi, lakini napendeza,

Enyi binti za Yerusalemu,

weusi kama mahema ya Kedari,

kama mapazia ya hema la Solomoni.

6 Usinikazie macho kwa sababu mimi ni mweusi,

kwa sababu nimefanywa mweusi na jua.

Wana wa mama yangu walinikasirikia

na kunifanya niwe mtunza mashamba ya mizabibu,

shamba langu mwenyewe la mizabibu nimeliacha.

7 Niambie, wewe ambaye ninakupenda,

unalisha wapi kundi lako la kondoo

na ni wapi unapowapumzisha kondoo wako adhuhuri.

Kwa nini niwe kama mwanamke aliyefunikwa shela

karibu na makundi ya rafiki zako?

8 Kama hujui, ewe mwanamke mzuri kuliko wote,

fuata nyayo za kondoo

na kulisha wana-mbuzi wako

karibu na hema za wachungaji.

9 Mpenzi wangu, ninakufananisha na farasi jike

aliyefungwa katika mojawapo ya magari ya vita ya Farao.

10 Mashavu yako yanapendeza yakiwa na vipuli,

shingo yako ikiwa na mikufu ya vito.

11 Tutakufanyia vipuli vya dhahabu,

vyenye kupambwa kwa fedha.

12 Wakati mfalme alipokuwa mezani pake,

manukato yangu yasambaza harufu yake nzuri.

13 Mpenzi wangu kwangu mimi ni kifuko cha manemane

kati ya matiti yangu.

14 Mpenzi wangu kwangu mimi ni kama kishada cha maua ya mhina

yaliyochanua kutoka mashamba ya mizabibu ya En-Gedi.

15 Tazama jinsi ulivyo mzuri, mpenzi wangu!

Tazama jinsi ulivyo mzuri!

Macho yako ni kama ya hua.

16 Tazama jinsi ulivyo mzuri, mpenzi wangu!

O, tazama ni jinsi gani unavyopendeza!

Na kitanda chetu ni cha majani mabichi mazuri.

17 Nguzo za nyumba yetu ni mierezi,

na mapao yetu ni miberoshi.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/SNG/1-aa5542e6a01defc4e02688125b839d1d.mp3?version_id=1627—

Wimbo Ulio Bora 2

1 Mimi ni ua la waridi la Sharoni,

yungiyungi ya bondeni. Mpenzi

2 Kama yungiyungi katikati ya miiba

ndivyo alivyo mpenzi wangu katikati ya wanawali.

3 Kama mti wa mtofaa miongoni mwa miti ya msituni

ndivyo alivyo mpenzi wangu

miongoni mwa wanaume vijana.

Ninafurahia kuketi kivulini mwa mwanaume huyu,

na tunda lake ni tamu kwangu.

4 Amenichukua mpaka kwenye ukumbi wa karamu,

na bendera ya huyu mwanaume

juu yangu ni upendo.

5 Nitie nguvu kwa zabibu kavu,

niburudishe kwa matofaa,

kwa maana ninazimia kwa mapenzi.

6 Mkono wa kushoto uko chini ya kichwa changu,

na mkono wake wa kuume unanikumbatia.

7 Binti za Yerusalemu, ninawaagiza

kwa paa na kwa ayala wa shambani:

Msichochee wala kuamsha mapenzi

hata yatakapotaka yenyewe.

8 Sikiliza! Mpenzi wangu!

Tazama! Huyu hapa anakuja,

akirukaruka juu milimani

akizunguka juu ya vilima.

9 Mpenzi wangu ni kama paa au swala kijana.

Tazama! Anasimama nyuma ya ukuta wetu,

akitazama kupitia madirishani,

akichungulia kimiani.

10 Mpenzi wangu alizungumza na kuniambia,

“Inuka, mpenzi wangu,

mrembo wangu, tufuatane.

11 Tazama! Wakati wa masika umepita,

mvua imekwisha imekwenda zake.

12 Maua yanatokea juu ya nchi;

majira ya kuimba yamewadia,

sauti za njiwa zinasikika

katika nchi yetu.

13 Mtini unatunga matunda yake ya mwanzoni,

zabibu zinazochanua zaeneza harufu yake nzuri.

Inuka, njoo, mpenzi wangu,

mrembo wangu, tufuatane.”

14 Hua wangu penye nyufa za majabali,

mafichoni pembezoni mwa mlima,

nionyeshe uso wako,

na niisikie sauti yako,

kwa maana sauti yako ni tamu,

na uso wako unapendeza.

15 Tukamatie mbweha,

mbweha wadogo wale

wanaoharibu mashamba ya mizabibu,

mashamba yetu ya mizabibu yaliyochanua.

16 Mpenzi wangu ni wangu, nami ni wake,

hujilisha katikati ya yungiyungi.

17 Mpaka jua linapochomoza,

na vivuli vikimbie,

rudi, mpenzi wangu,

na uwe kama paa,

au kama ayala kijana

juu ya vilima vya Betheri.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/SNG/2-e8bb73f313408f6ed2c4314bc12546ae.mp3?version_id=1627—

Wimbo Ulio Bora 3

1 Usiku kucha kwenye kitanda changu

nilimtafuta yule moyo wangu umpendaye;

nilimtafuta huyo mwanaume lakini sikumpata.

2 Sasa nitaondoka na kuzunguka mjini,

kupitia katika barabara zake

na viwanjani;

nitamtafuta yule moyo wangu umpendaye.

Kwa hiyo nilimtafuta

lakini sikumpata huyo mwanaume.

3 Walinzi walinikuta

walipokuwa wakizunguka mji.

Nikawauliza, “Je, mmemwona

yule moyo wangu umpendaye?”

4 Kitambo kidogo tu baada ya kuwapita

nilimpata yule moyo wangu umpendaye.

Nilimshika na sikumwachia aende mpaka nilipomleta

katika nyumba ya mama yangu,

katika chumba cha yule aliyenichukua mimba.

5 Binti za Yerusalemu, ninawaagiza

kwa paa na kwa ayala wa shambani:

Msichochee wala kuamsha mapenzi

hata yatakapotaka yenyewe.

6 Ni nani huyu anayekuja kutoka jangwani

kama nguzo ya moshi,

anayenukia manemane na uvumba

iliyotengenezwa kwa vikolezo vyote

vya mfanyabiashara?

7 Tazama! Ni gari la Solomoni

lisindikizwalo na mashujaa sitini,

walio wakuu sana wa Israeli,

8 wote wamevaa panga,

wote wazoefu katika vita,

kila mmoja na upanga wake pajani,

wamejiandaa kwa ajili ya hofu za usiku.

9 Mfalme Solomoni alijitengenezea gari;

alitengeneza kwa mbao kutoka Lebanoni.

10 Nguzo zake alitengeneza za fedha,

kitako chake kwa dhahabu.

Kiti chake kilikuwa kimepambwa kwa zambarau,

gari lake limenakishiwa njumu,

kwa ndani limefunikwa kwa upendo

wa binti za Yerusalemu.

11 Tokeni nje, ninyi binti za Sayuni,

mumtazame Mfalme Solomoni

akiwa amevaa taji,

taji ambalo mama yake alimvika

siku ya arusi yake,

siku ambayo moyo wake ulishangilia.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/SNG/3-92b9f3c5a11759d9568a6fa395eeeddb.mp3?version_id=1627—

Wimbo Ulio Bora 4

1 Tazama jinsi ulivyo mzuri, mpenzi wangu!

O, jinsi ulivyo mzuri!

Macho yako nyuma ya shela yako

ni kama ya hua.

Nywele zako ni kama kundi la mbuzi

zikishuka kutoka Mlima Gileadi.

2 Meno yako ni kama kundi la kondoo

waliokatwa manyoya sasa hivi,

watokao kuogeshwa.

Kila mmoja ana pacha lake,

hakuna hata mmoja aliye peke yake.

3 Midomo yako ni kama uzi mwekundu,

kinywa chako kinapendeza.

Mashavu yako nyuma ya shela yako

ni kama vipande viwili vya komamanga.

4 Shingo yako ni kama mnara wa Daudi,

uliojengwa kwa madaha,

juu yake zimetundikwa ngao elfu,

zote ni ngao za mashujaa.

5 Matiti yako mawili ni kama wana paa wawili,

kama mapacha ya wana paa

wale wajilishao katikati ya yungiyungi.

6 Hata papambazuke na vivuli vikimbie,

nitakwenda kwenye mlima wa manemane

na kwenye kilima cha uvumba.

7 Wewe ni mzuri kote, mpenzi wangu,

hakuna hitilafu ndani yako.

8 Twende pamoja nami kutoka Lebanoni,

bibi arusi wangu,

twende pamoja nami kutoka Lebanoni.

Shuka kutoka ncha ya Amana,

kutoka juu ya Seniri, kilele cha Hermoni,

kutoka mapango ya simba

na kutoka mlima wapendapo kukaa chui.

9 Umeiba moyo wangu, dada yangu,

bibi arusi wangu;

umeiba moyo wangu

kwa mtupo mmoja wa macho yako,

kwa kito kimoja cha thamani cha mkufu wako.

10 Tazama jinsi pendo lako linavyofurahisha,

dada yangu, bibi arusi wangu!

Ni mara ngapi zaidi pendo lako linafurahisha kuliko divai,

na harufu ya manukato yako zaidi

kuliko kikolezo cho chote!

11 Midomo yako inadondosha utamu kama sega la asali,

bibi arusi wangu;

maziwa na asali viko chini ya ulimi wako.

Harufu nzuri ya mavazi yako ni kama ile ya Lebanoni.

12 Wewe ni bustani iliyofungwa, dada yangu,

bibi arusi wangu;

wewe ni chanzo cha maji

kilichozungushiwa kabisa,

chemchemi yangu peke yangu.

13 Mimea yako ni bustani ya komamanga

yenye matunda mazuri sana,

yenye hina na nardo,

14 nardo na zafarani,

mchai na mdalasini,

pamoja na kila aina ya mti wa uvumba,

manemane na udi,

na aina zote za vikolezo bora kuliko vyote.

15 Wewe ni chemchemi ya bustani,

kisima cha maji yatiririkayo,

yatiririkayo kutoka Lebanoni.

16 Amka, upepo wa kaskazini,

na uje, upepo wa kusini!

Vuma juu ya bustani yangu,

ili harufu yake nzuri iweze kuenea mpaka ng’ambo.

Mpendwa wangu na aje bustanini mwake

na kuonja matunda mazuri sana.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/SNG/4-b7bfa511541d24823c02d513c04318ac.mp3?version_id=1627—

Wimbo Ulio Bora 5

1 Nimekuja kwenye bustani yangu, dada yangu,

bibi arusi wangu;

nimekusanya manemane yangu pamoja

na kikolezo changu.

Nimekula sega langu la asali na asali yangu;

nimekunywa divai yangu na maziwa yangu.

Kuleni, enyi marafiki, mnywe;

kunyweni ya kutosha, Ee wapenzi.

2 Nililala lakini moyo wangu ulikuwa macho.

Sikiliza! Mpenzi wangu anabisha:

“Nifungulie, dada yangu, mpenzi wangu,

hua wangu, asiye na hitilafu.

Kichwa changu kimeloa umande,

na nywele zangu manyunyu ya usiku.”

3 Nimevua joho langu:

je, ni lazima nivae tena?

Nimenawa miguu yangu:

je, ni lazima niichafue tena?

4 Mpenzi wangu aliweka mkono wake kwenye tundu la komeo;

moyo wangu ulianza kugonga kwa ajili yake.

5 Niliinuka kumfungulia mpenzi wangu,

mikono yangu ilidondosha manemane,

vidole vyangu vikitiririka manemane,

penye vipini vya komeo.

6 Nilimfungulia mpenzi wangu,

lakini mpenzi wangu alishaondoka;

alikuwa amekwenda zake.

Moyo wangu ulishuka kwa kuondoka kwake.

Nilimtafuta lakini sikumpata.

Nilimwita lakini hakunijibu.

7 Walinzi walinikuta

walipokuwa wakifanya zamu za ulinzi mjini.

Walinipiga, walinijeruhi,

walininyang’anya joho langu,

hao walinzi wa kuta!

8 Enyi binti za Yerusalemu, ninawaagiza:

kama mkimpata mpenzi wangu,

mtamwambia nini?

Mwambieni ninazimia kwa mapenzi.

9 Je, mpendwa wako ni bora kuliko wengine namna gani,

ni mzuri sana kupita wanawake wote?

Je, mpendwa wako ni mzuri kuliko wengine,

kwa namna gani,

hata unatuagiza hivyo?

10 Mpenzi wangu anang’aa tena mwekundu kwa afya,

wakuvutia miongoni mwa wanaume kumi elfu.

11 Kichwa chake ni dhahabu safi kuliko zote,

nywele zake ni za mawimbi

na ni nyeusi kama kunguru.

12 Macho yake ni kama ya hua

kandokando ya vijito vya maji,

aliyeogeshwa kwenye maziwa,

yamepangwa kama vito vya thamani.

13 Mashavu yake ni kama matuta ya vikolezo

yakitoa manukato.

Midomo yake ni kama yungiyungi

inayodondosha manemane.

14 Mikono yake ni fimbo za dhahabu

iliyopambwa kwa Krisolitho.

Mwili wake ni kama pembe ya ndovu iliyong’arishwa

iliyopambwa na yakuti samawi.

15 Miguu yake ni nguzo za marmar

zilizosimikwa katika vitako vya dhahabu safi.

Sura yake ni kama Lebanoni,

mzuri kama miti yake ya mierezi.

16 Kinywa chake chenyewe ni utamu,

kwa ujumla yeye ni wa kupendeza.

Huyu ndiye mpenzi wangu, huyu ndiye rafiki yangu,

Ee binti za Yerusalemu.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/SNG/5-ecc48cc679f9d87d8ca6243ded71bc45.mp3?version_id=1627—

Wimbo Ulio Bora 6

1 Mpenzi wako amekwenda wapi,

yule mzuri kupita wanawake wote?

Mpenzi wako amegeukia njia ipi,

tupate kumtafuta pamoja nawe?

2 Mpenzi wangu amekwenda bustanini mwake,

kwenye vitalu vya vikolezo,

kujilisha bustanini

na kukusanya yungiyungi.

3 Mimi ni wake mpenzi wangu,

na mpenzi wangu ni wangu mimi;

huyu mwanaume hulisha katikati ya yungiyungi.

4 Wewe ni mzuri, mpenzi wangu, kama Tirza,

upendezaye kama Yerusalemu,

umetukuka kama jeshi lenye bendera.

5 Uyageuze macho yako mbali nami,

yananigharikisha.

Nywele zako ni kama kundi la mbuzi

wanaotelemka kutoka Gileadi.

6 Meno yako ni kama kundi la kondoo

wanaotoka kuogeshwa.

Kila mmoja ana pacha lake,

hakuna hata mmojawapo aliye peke yake.

7 Mashavu yako nyuma ya shela yako

ni kama vipande viwili vya komamanga.

8 Panaweza kuwapo malkia sitini,

masuria themanini

na mabikira wasiohesabika;

9 lakini hua wangu, mkamilifu wangu,

ni wa namna ya pekee,

binti pekee kwa mama yake,

kipenzi cha yeye aliyemzaa.

Wanawali walimwona na kumwita mbarikiwa;

malkia na masuria walimsifu.

10 Ni nani huyu atokeaye kama mapambazuko,

mzuri kama mwezi, mwangavu kama jua,

ametukuka kama majeshi yenye bendera?

11 Nilitelemka kwenye kichaka cha miti ya milozi

ili kutazama machipuko ya bondeni,

kuona kama mizabibu imechipua

au kama mikomamanga imechanua maua.

12 Kabla sijang’amua,

shauku yangu iliniweka

katikati ya magari ya kifalme ya kukokotwa na farasi.

13 Rudi, rudi, Ee Mshulami;

rudi, rudi ili tupate kukutazama!

Kwa nini kumtazama Mshulami,

# kama kutazama ngoma ya Mahanaimu?

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/SNG/6-6e5ca2b6b3f2cbc660fcf8246dd18bce.mp3?version_id=1627—

Wimbo Ulio Bora 7

1 Ee binti wa mwana wa mfalme,

tazama jinsi inavyopendeza miguu yako katika viatu!

Miguu yako yenye madaha ni kama vito vya thamani,

kazi ya mikono ya fundi stadi.

2 Kitovu chako ni kama bilauri ya mviringo

ambayo kamwe haikosi divai iliyochanganywa.

Kiuno chako ni kichuguu cha ngano

kilichozungukwa kwa yungiyungi.

3 Matiti yako ni kama wana paa wawili,

mapacha wa swala.

4 Shingo yako ni kama mnara wa pembe ya ndovu.

Macho yako ni vidimbwi vya Heshboni

karibu na lango la Beth-Rabi.

Pua yako ni kama mnara wa Lebanoni

ukitazama kuelekea Dameski.

5 Kichwa chako kinakuvika taji kama mlima Karmeli.

Nywele zako ni kama zulia nene la kutundika ukutani;

mfalme ametekwa na mashungi yake.

6 Tazama jinsi ulivyo mzuri na unavyopendeza,

Ee pendo, kwa uzuri wako!

7 Umbo lako ni kama la mtende,

nayo matiti yako kama vishada vya matunda.

8 Nilisema, “Nitakwea mtende,

nami nitayashika matunda yake.”

Matiti yako na yawe kama vishada vya mzabibu,

harufu nzuri ya pumzi yako kama matofaa,

9 na kinywa chako kama divai

bora kuliko zote.

Divai na iende moja kwa moja kwa mpenzi wangu,

ikitiririka pole pole juu ya midomo na meno.

10 Mimi ni mali ya mpenzi wangu,

nayo shauku yake ni juu yangu.

11 Njoo, mpenzi wangu, twende mashambani,

twende tukalale huko vijijini.

12 Hebu na twende mapema

katika mashamba ya mizabibu

tuone kama mizabibu imechipua,

kama maua yake yamefunguka,

pia kama mikomamanga imetoa maua:

huko nitakupa penzi langu.

13 Mitunguja hutoa harufu zake nzuri,

kwenye milango yetu kuna matunda mazuri,

mapya na ya zamani,

ambayo nimekuhifadhia wewe,

mpenzi wangu.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/SNG/7-5c3cefdcb92e234defb3e7eb7ef32ca3.mp3?version_id=1627—

Wimbo Ulio Bora 8

1 Laiti ungelikuwa kwangu kama ndugu wa kiume,

ambaye aliyanyonya matiti ya mama yangu!

Kisha, kama ningekukuta huko nje,

ningelikubusu,

wala hakuna mtu ye yote angelinidharau.

2 Ningelikuongoza na kukuleta

katika nyumba ya mama yangu,

yeye ambaye amenifundisha.

Ningelikupa divai iliyokolezwa unywe,

asali ya maua ya mikomamanga yangu.

3 Mkono wa kushoto wa huyo mwanaume

uko chini ya kichwa changu,

na mkono wake wa kuume unanikumbatia.

4 Binti za Yerusalemu, ninawaagiza:

msichochee wala kuamsha mapenzi

hata yatakapotaka yenyewe.

5 Ni nani huyu anayekuja kutoka nyikani

akimwegemea mpenzi wake?

Nilikuamsha chini ya mtofaa,

huko mama yako alipotunga mimba yako,

huko yeye alipata utungu akakuzaa.

6 Nitie kama muhuri moyoni mwako,

kama muhuri kwenye mkono wako;

kwa maana upendo una nguvu kama mauti,

wivu wake ni mkatili kama kuzimu.

Unachoma kama mwali wa moto,

kama mwali mkubwa wa moto waBwanahasa.

7 Maji mengi hayawezi kuuzimisha upendo,

mito haiwezi kuugharikisha.

Kama mtu angelitoa mali yote ya nyumbani mwake

kwa ajili ya upendo,

angelidharauliwa kabisa.

8 Tunaye dada mdogo,

matiti yake hayajakua bado.

Tutafanya nini kwa ajili ya dada yetu

wakati atakapokuja kuposwa?

9 Kama yeye ni ukuta,

tutajenga minara ya fedha juu yake.

Na kama yeye ni mlango,

tutamzungushia mbao za mierezi.

10 Mimi ni ukuta,

nayo matiti yangu ni kama minara.

Ndivyo ambavyo nimekuwa machoni pake

kama yule anayeleta utoshelevu.

11 Solomoni alikuwa na shamba la mizabibu huko Baal-Hamoni;

alikodisha shamba lake la mizabibu kwa wapangaji.

Kila mmoja angeleta kwa ajili ya matunda yake

# shekeli 1,000za fedha.

12 Lakini shamba langu la mizabibu

ambalo ni langu mwenyewe

ni langu kutoa;

hizo shekeli 1,000 ni kwa ajili yako, Ee Solomoni,

# na shekeli mia mbili

ni kwa ajili ya wale wanaotunza matunda yake.

13 Wewe ukaaye bustanini

pamoja na marafiki mliohudhuria,

unisikizishe na mimi sauti yako!

14 Njoo, mpenzi wangu,

uwe kama swala

au kama ayala mdogo

juu ya milima iliyojaa vikolezo.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/SNG/8-300629cf01a2155acb27cbc174e33610.mp3?version_id=1627—

Mhubiri 1

Kila Kitu Ni Ubatili Mtupu

1 Maneno ya Mhubiri, mwana wa Daudi, mfalme huko Yerusalemu:

2 “Ubatili mtupu! Ubatili mtupu!”

Mhubiri anasema.

“Ubatili mtupu!

Kila kitu ni ubatili.”

3 Mwanadamu anafaidi nini kutokana na kazi yake yote

anayotaabikia chini ya jua?

4 Vizazi huja na vizazi hupita,

lakini dunia inadumu milele.

5 Jua huchomoza na jua huzama,

nalo huarakisha kurudi maawioni.

6 Upepo huvuma kuelekea kusini

na kugeukia kaskazini,

hurudia mzunguko huo huo,

daima ukirudia njia yake.

7 Mito yote hutiririka baharini,

hata hivyo bahari kamwe haijai.

Mahali mito inapotoka,

huko hurudi tena.

8 Vitu vyote vinachosha,

zaidi kuliko mtu anavyoweza kusema.

Jicho kamwe halitosheki kutazama,

wala sikio halishibi kusikia.

9 Kile kilichokuwapo kitakuwapo tena,

kile kilichofanyika kitafanyika tena,

hakuna kilicho kipya chini ya jua.

10 Kuna kitu cho chote ambacho mtu anaweza kusema,

“Tazama! Kitu hiki ni kipya”?

Kilikuwapo tangu zamani za kale,

kilikuwapo kabla ya wakati wetu.

11 Hakuna kumbukumbu ya watu wa zamani,

hata na wale ambao hawajaja bado

hawatakumbukwa

na wale watakaofuata baadaye.

Hekima Ni Ubatili

12 Mimi, Mhubiri, nilikuwa mfalme katika Yerusalemu.

13 Nilitumia muda wangu wote kujifunza na kuvumbua kwa hekima yote yanayofanyika chini ya mbingu. Jinsi gani Mungu ameweka mzigo mzito juu ya wanadamu!

14 Nimeshaona mambo yote yanayotendeka chini ya jua, hayo yote ni ubatili, hii ni kukimbiza upepo.

15 Kilichopindika hakiwezekani kunyoshwa,

kile ambacho hakipo haiwezekani kukihesabu.

16 Niliwaza mwenyewe, “Tazama, nimekua na kuongezeka katika hekima kuliko ye yote aliyewahi kutawala Yerusalemu kabla yangu. Nimekuwa na uzoefu mkubwa wa hekima na maarifa.”

17 Ndipo nilipojitahidi kufahamu kutofautisha hekima, wazimu na upumbavu, lakini nikatambua hata hili nalo ni kukimbiza upepo.

18 Kwa kuwa hekima nyingi huleta huzuni kubwa;

maarifa yanapoongezeka, masikitiko yanaongezeka.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/ECC/1-cc76df45a6ce50f66cc53b5ad9a9a9e2.mp3?version_id=1627—

Mhubiri 2

Anasa Ni Ubatili

1 Nikafikiri moyoni mwangu, “Haya basi, nitakujaribu kwa anasa nione ni lipi lililo jema.” Lakini hilo nalo likaonekana ni ubatili.

2 Nikasema, “Kicheko nacho ni upumbavu. Nayo matokeo ya anasa ni nini?”

3 Nikajaribu kujifurahisha kwa mvinyo na kukumbatia upumbavu, huku bado akili yangu inaniongoza kwa hekima. Nilitaka kuona ni lipi bora watu wafanye kwa siku chache wanazoishi chini ya mbingu.

4 Nikafanya miradi mikubwa: Nikajijengea majumba na kulima mashamba ya mizabibu.

5 Nikatengeneza bustani na viwanja vya starehe nikaotesha huko kila aina ya miti ya matunda.

6 Nikajenga mabwawa ya kukusanya maji ya kunyweshea hii miti iliyokuwa inastawi vizuri.

7 Nikanunua watumwa wa kiume na wa kike na watumwa wengine walizaliwa nyumbani mwangu. Pia nilikuwa na makundi ya ng’ombe, kondoo na mbuzi kuliko mtu ye yote aliyewahi kuishi Yerusalemu kabla yangu.

8 Nikajikusanyia fedha na dhahabu, hazina za wafalme na za majimbo. Nikajipatia waimbaji wanaume na wanawake, nazo nyumba za masuria: vitu ambavyo moyo wa mwanadamu hufurahia.

9 Nikawa maarufu sana kuliko mtu mwingine ye yote aliyepata kuishi Yerusalemu kabla yangu. Katika haya yote bado nikawa nina hekima.

10 Sikujinyima kitu cho chote ambacho macho yangu yalikitamani,

hakuna anasa ambayo niliunyima moyo wangu.

Moyo wangu ulifurahia kazi zangu zote,

hii ilikuwa thawabu ya kazi zangu zote.

11 Hata hivyo nilipokuja kuangalia yote ambayo

mikono yangu ilikuwa imefanya

na yale niliyotaabika kukamilisha,

kila kitu kilikuwa ni ubatili, ni kukimbiza upepo;

hapakuwa na faida yo yote chini ya jua.

Hekima Na Upumbavu Ni Ubatili

12 Kisha nikageuza mawazo yangu kufikiria hekima,

wazimu na upumbavu.

Ni nini zaidi mtu anayetawala baada ya mfalme

anachoweza kufanya ambacho hakijafanywa?

13 Nikaona kuwa hekima ni bora kuliko upumbavu,

kama vile nuru ilivyo bora kuliko giza.

14 Mtu mwenye hekima ana macho katika kichwa chake,

lakini mpumbavu anatembea gizani;

lakini nikaja kuona kwamba

wote wawili hatima yao inafanana.

15 Kisha nikafikiri moyoni mwangu,

“Hatima ya mpumbavu itanipata mimi pia.

Nitafaidi nini basi kwa kuwa na hekima?”

Nikasema moyoni mwangu,

“Hili nalo ni ubatili.”

16 Kwa maana kwa mtu mwenye hekima,

kama ilivyo kwa mpumbavu,

hatakumbukwa kwa muda mrefu,

katika siku zijazo wote watasahaulika.

Kama vile ilivyo kwa mpumbavu,

mtu mwenye hekima pia lazima atakufa!

Kutaabika Ni Ubatili

17 Kwa hiyo nikachukia maisha, kwa sababu kazi inayofanyika chini ya jua ilikuwa masikitiko kwangu. Yote hayo ni ubatili, ni kukimbiza upepo.

18 Nikachukia kila kitu nilichokuwa nimetaabikia chini ya jua, kwa sababu ni lazima nimwachie yule ajaye baada yangu.

19 Nani ajuaye kama atakuwa ni mtu mwenye hekima au mpumbavu? Lakini hata hivyo yeye ndiye atakayetawala kazi zote ambazo nimemiminia juhudi na ustadi chini ya jua. Hili nalo ni ubatili.

20 Kwa hiyo moyo wangu ukaanza kukata tamaa juu ya kazi yangu yote niliyoifanya kwa taabu chini ya jua.

21 Kwa kuwa mtu anaweza kufanya kazi yake kwa hekima, maarifa na ustadi, kisha analazimika kuacha vyote alivyo navyo kwa mtu mwingine ambaye hajavifanyia kazi. Hili nalo pia ni ubatili tena ni balaa kubwa.

22 Mtu atapata nini kwa taabu yote na kuhangaika kwa bidii katika kazi anayotaabikia chini ya jua?

23 Siku zake zote kazi yake ni maumivu na masikitiko, hata usiku akili yake haipati mapumziko. Hili nalo pia ni ubatili.

24 Hakuna kitu bora anachoweza kufanya mtu zaidi ya kula na kunywa na kuridhika katika kazi yake. Hili nalo pia, ninaona, latokana na mkono wa Mungu,

25 kwa sababu pasipo yeye, ni nani awezaye kula na kufurahi?

26 Kwa yule mtu anayempendeza Mungu, Mungu humpa hekima, maarifa na furaha, bali kwa mwenye dhambi Mungu humpa kazi ya kukusanya na kuhifadhi utajiri ili Mungu ampe yule anayempenda. Hili nalo pia ni ubatili, ni kukimbiza upepo.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/ECC/2-b84de2feed7fea8d107bdf984d0ebe1a.mp3?version_id=1627—