1 Wakorintho 13

Karama Ya Upendo

1 Hata kama nitasema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa kengele inayolialia au toazi livumalo.

2 Ningekuwa na karama ya unabii na kujua siri zote na maarifa yote, hata kama nina imani kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, mimi si kitu.

3 Kama nikitoa mali yote niliyo nayo na kama nikijitolea mwili wangu uchomwe moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu.

4 Upendo huvumilia, upendo hufadhili, upendo hauoni wivu, hauna majivuno. Upendo hauna kiburi.

5 Haukosi kuwa na adabu. Upendo hautafuti mambo yake, haukasiriki upesi, hauweki kumbukumbu ya mabaya.

6 Upendo haufurahii mabaya bali hufurahi pamoja na kweli.

7 Upendo huvumilia yote, huamini yote, hutumaini yote, hustahimili yote.

8 Upendo haushindwi kamwe. Lakini ukiwepo unabii, utakoma; zikiwepo lugha, zitakoma; yakiwepo maarifa, yatapita.

9 Kwa maana tunafahamu kwa sehemu na tunatoa unabii kwa sehemu.

10 Lakini ukamilifu utakapokuja, yale yasiyo kamili yatatoweka.

11 Nilipokuwa mtoto, nilisema kama mtoto, niliwaza kama mtoto, nilifikiri kama mtoto. Nilipokuwa mtu mzima niliacha mambo ya kitoto.

12 Kwa maana sasa tunaona taswira kama ya kwenye kioo, lakini wakati huo tutaona wazi. Sasa nafahamu kwa sehemu, wakati huo nitafahamu kikamilifu, kama vile mimi ninavyofahamika kikamilifu.

13 Basi sasa, yanadumu mambo haya matatu: Imani, tumaini na upendo. Lakini lililo kuu miongoni mwa haya matatu ni upendo.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/1CO/13-3abe1747968f2652e7e85c1ce78adfe6.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

eight − four =