2 Wakorintho 3

Wahudumu Wa Agano Jipya

1 Je, tunaanza tena kujisifu wenyewe? Au tunahitaji kupata barua za utambulisho kwenu au kutoka kwenu, kama watu wengine?

2 Ninyi wenyewe ndio barua yetu iliyoandikwa katika mioyo yetu, inayojulikana na kusomwa na kila mtu.

3 Nanyi mwadhihirisha wazi kwamba ninyi ni barua itokayo kwa Kristo, matokeo ya huduma yetu, ambayo haikuandikwa kwa wino bali kwa Roho wa Mungu aliye hai, si katika vibao vya mawe, bali katika vibao ambavyo ni mioyo ya wanadamu.

4 Hili ndilo tumaini tulilo nalo mbele za Mungu kwa njia ya Kristo.

5 Si kwamba sisi tunafikiri kuwa tunaweza kufanya jambo lo lote wenyewe, lakini nguvu yetu inatoka kwa Mungu.

6 Yeye ndiye aliyetuwezesha sisi kuwa wahudumu wa Agano Jipya: si wa andiko, bali wa Roho; kwa kuwa andiko huua bali Roho hutia uzima.

Utukufu Wa Agano Jipya

7 Basi ikiwa ile huduma iliyoleta mauti, ile iliyoandikwa kwa herufi juu ya jiwe ilikuja kwa utukufu hata Waisraeli wakawa hawawezi kuutazama uso wa Mose kwa sababu ya ule utukufu wake, ingawa ulikuwa ni wa kufifia,

8 je, huduma ya Roho haitakuwa na utukufu zaidi?

9 Ikiwa huduma ile iwahukumuyo wanadamu ina utukufu, je, haitakuwa ya utukufu zaidi ile huduma iletayo haki?

10 Kwa maana kile kilichokuwa na utukufu sasa hakina utukufu ukilinganisha na huu utukufu uzidio sana wa Agano Jipya.

11 Ikiwa kile kilichokuwa kinafifia kilikuja kwa utukufu, si zaidi sana utukufu wa kile kinachodumu?

12 Kwa hiyo, kwa kuwa tunalo tumaini hili, tuna ujasiri sana.

13 Sisi si kama Mose, ambaye ilimpasa kuweka utaji ili kufunika uso wake ili Waisraeli wasiuone ule mng’ao uliokuwa juu yake wakati ukififia na hatimaye kutoweka.

14 Lakini akili zao zilipumbazwa, kwa maana mpaka leo utaji ule ule hufunika wakati Agano la Kale lisomwapo. Huo utaji haujaondolewa kwa maana ni katika Kristo peke yake unaondolewa.

15 Hata leo, Torati ya Mose isomwapo, utaji hufunika mioyo yao.

16 Lakini wakati wo wote mtu anapomgeukia Bwana, “utaji unaondolewa.”

17 Basi Bwana ndiye Roho. Mahali alipo Roho wa Bwana hapo pana uhuru.

18 Nasi sote, tukiwa na nyuso zisizotiwa utaji tunaakisi utukufu wa Bwana, kama kwenye kioo. Nasi tunabadilishwa ili tufanane naye, toka utukufu hadi utukufu mkuu zaidi, utokao kwa Bwana, ambaye ndiye Roho.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/2CO/3-5de02adfa7c0bebf39de62a416f664d5.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

nine − 6 =