Mathayo 19

Yesu Afundisha Kuhusu Talaka

1 Yesu alipomaliza kusema maneno haya, aliondoka Galilaya, akaenda sehemu za Uyahudi, ng’ambo ya Mto Yordani.

2 Umati mkubwa wa watu ukamfuata, naye akawaponya huko.

3 Baadhi ya Mafarisayo wakamjia ili kumjaribu wakamwuliza, “Ni halali mtu kumwacha mke wake kwa sababu yo yote?”

4 Akawajibu, “Je, hamkusoma kwamba hapo mwanzo Muumba aliwaumba mtu mume na mtu mke.

5 Naye akasema, ‘Kwa sababu hii mtu atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe na hao wawili watakuwa mwili mmoja?’

6 Hivyo si wawili tena, bali ni mwili mmoja. Kwa hiyo kile alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe.”

7 Wakamwuliza, “Kwa nini basi Mose aliagiza mtu kumpa mkewe hati ya talaka na kumwacha?”

8 Yesu akawajibu, “Mose aliwaruhusu kuwaacha wake zenu kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu. Lakini tangu mwanzo haikuwa hivyo.

9 Mimi nawaambia, ye yote amwachaye mkewe isipokuwa kwa sababu ya uasherati naye akaoa mke mwingine, anazini. Naye amwoaye yule mwanamke aliyeachwa pia anazini.”

10 Wanafunzi wake wakamwambia, “Kama hali ndiyo hii kati ya mume na mke, ni afadhali mtu asioe!”

11 Yesu akawaambia, “Si watu wote wanaoweza kupokea neno hili, isipokuwa wale tu waliojaliwa na Mungu

12 Kwa maana wengine ni matowashi kwa sababu wamezaliwa hivyo, wengine wamefanywa matowashi na wanadamu, na wengine wamejifanya matowashi kwa ajili ya Ufalme wa Mbinguni. Yeye awezaye kulipokea neno hili na alipokee.”

Yesu Awabariki Watoto Wadogo

13 Kisha watoto wadogo wakaletwa kwa Yesu ili aweke mikono yake juu yao na awaombee. Lakini wanafunzi wake wakawakemea wale waliowaleta.

14 Yesu akasema, “Waacheni watoto wadogo waje kwangu, wala msiwazuie, kwa maana Ufalme wa Mbinguni ni wa wale walio kama hawa.”

15 Naye akaweka mikono yake juu yao, akaondoka huko.

Kijana Tajiri

16 Mtu mmoja akamjia Yesu na kumwuliza, “Mwalimu mwema, nifanye jambo gani jema ili nipate uzima wa milele?”

17 Yesu akamjibu, “Mbona unaniita mimi mwema? Hakuna aliye mwema ila Mmoja tu, ndiye Mungu: Lakini ukitaka kuingia uzimani, zitii amri.”

18 Yule mtu akamwuliza, “Amri zipi?”

Yesu akamjibu, “Usiue, usizini, usiibe, usishuhudie uongo,

19 waheshimu baba yako na mama yako na umpende jirani yako kama nafsi yako.”

20 Yule kijana akasema, “Hizi zote nimezishika. Je, bado nimepungukiwa na nini?”

21 Yesu akamwambia, “Kama ukitaka kuwa mkamilifu, nenda, ukauze vitu vyote ulivyo navyo na hizo fedha uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni. Kisha njoo, unifuate.”

22 Yule kijana aliposikia hayo, akaenda zake kwa huzuni, kwa sababu alikuwa na mali nyingi.

Hatari Za Utajiri

23 Ndipo Yesu akawaambia wanafunzi wake, “Amin, amin nawaambia, itakuwa vigumu kwa mtu tajiri kuingia katika Ufalme wa Mbinguni.

24 Tena nawaambia, ni rahisi zaidi kwa ngamia kupita kwenye tundu la sindano kuliko mtu tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.”

25 Wanafunzi wake waliposikia haya, walishangaa sana na kuuliza, “Ni nani basi awezaye kuokoka?”

26 Lakini Yesu akawatazama, akawaambia, “Kwa mwanadamu jambo hili haliwezekani, lakini kwa Mungu mambo yote yanawezekana.”

27 Ndipo Petro akamjibu, “Tazama, sisi tumeacha kila kitu na kukufuata, tutapata nini basi?”

28 Yesu akawaambia, “Amin, amin nawaambia, wakati wa kufanywa upya vitu vyote, wakati Mwana wa Adamu atakapoketi kwenye kiti chake cha utukufu cha enzi, ninyi mliomfuata pia mtaketi katika viti vya enzi kumi na viwili, mkiyahukumu makabila kumi na mawili ya Israeli.

29 Kila mmoja aliyeacha nyumba au ndugu zake wa kiume au wa kike au baba au mama au watoto au mashamba kwa ajili yangu, atapokea mara mia zaidi ya hayo na ataurithi uzima wa milele.

30 Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho, nao walio wa mwisho watakuwa wa kwanza.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/MAT/19-044f95bd7456d6ffbb6211b35e77dea2.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

15 − one =