Mhubiri 7

Hekima

1 Afadhali sifa nzuri kuliko manukato safi,

nayo siku ya kufa kuliko ya kuzaliwa.

2 Afadhali kwenda kwenye nyumba ya msiba

kuliko kwenda kwenye nyumba ya karamu,

kwa kuwa kifo ni hatima ya kila mwanadamu,

imewapasa walio hai kuliweka hili mioyoni mwao.

3 Huzuni ni afadhali kuliko kicheko,

kwa sababu uso wenye huzuni wafaa kwa moyo.

4 Moyo wa wenye hekima uko katika nyumba ya msiba,

lakini moyo wa wapumbavu uko katika nyumba ya anasa.

5 Afadhali kusikia karipio la mtu mwenye hekima,

kuliko kusikiliza wimbo wa wapumbavu.

6 Kama ilivyo kuvunjika kwa miiba chini ya sufuria,

ndivyo kilivyo kicheko cha wapumbavu.

Hili nalo pia ni ubatili.

7 Dhuluma humfanya mtu mwenye hekima kuwa mpumbavu,

nayo rushwa huuharibu moyo.

8 Mwisho wa jambo ni bora kuliko mwanzo wake,

uvumilivu ni bora kuliko kiburi.

9 Usiwe mwepesi kukasirika rohoni mwako,

kwa kuwa hasira hukaa kifuani mwa wapumbavu.

10 Usiseme, “Kwa nini siku za kale zilikuwa bora kuliko siku hizi?”

Kwa maana si hekima kuuliza maswali kama hayo.

11 Hekima, kama ulivyo urithi, ni kitu chema

na huwafaidia wale walionao jua.

12 Hekima ni ulinzi kama fedha ilivyo ulinzi,

lakini faida ya maarifa ni hii:

kwamba hekima huhifadhi maisha ya aliye nayo.

13 Tafakari kile Mungu alichokitenda:

Nani awezaye kunyosha

kile ambacho yeye amekipinda?

14 Nyakati zikiwa nzuri, ufurahi,

lakini nyakati zikiwa mbaya tafakari:

Mungu amefanya hiyo moja,

# naam sanjarina hiyo nyingine.

Kwa hiyo, mwanadamu hawezi kugundua

kitu cho chote kuhusu maisha yake ya baadaye.

15 Katika maisha haya yangu ya ubatili nimeshaona haya mawili:

mtu mwadilifu akiangamia katika uadilifu wake,

naye mtu mwovu akiishi maisha marefu katika uovu wake.

16 Usiwe mwenye haki kupita kiasi,

wala usiwe na hekima kupita kiasi:

kwa nini kujiangamiza mwenyewe?

17 Usiwe mwovu kupita kiasi,

wala usiwe mpumbavu:

kwa nini kufa kabla ya wakati wako?

18 Ni vyema kushika hilo moja

na wala usiache hilo jingine likupite.

# Mtu amchaye Mungu ataepuka huko kupita kiasi.

19 Hekima humfanya yeye aliye nayo kuwa na uwezo zaidi

kuliko watawala kumi katika mji.

20 Hakuna mtu mwenye haki duniani

ambaye hufanya mambo ya haki

na kamwe asitende dhambi.

21 Usitie maanani kila neno linalosemwa na watu,

la sivyo, waweza kumsikia

mtumishi wako akikulaani:

22 kwa kuwa unafahamu moyoni mwako

kwamba wewe mwenyewe mara nyingi

umewalaani wengine.

23 Yote haya niliyajaribu kwa hekima, nikasema,

“Nimeamua kuwa na hekima”:

lakini hii ilikuwa nje ya uwezo wangu.

24 Vyo vyote hekima ilivyo,

hekima iko mbali sana na imejificha,

ni nani awezaye kuigundua?

25 Nikageuza fikira zangu ili kuelewa,

kuchunguza na kuitafuta hekima

na kusudi la mambo,

na ili kuelewa ujinga wa uovu,

na wazimu wa upumbavu.

26 Nimeona jambo lililo chungu kuliko mauti,

mwanamke ambaye ni mtego,

ambaye moyo wake ni wavu wa kutegea

na mikono yake ni minyororo.

Mtu ampendezaye Mungu atamkwepa,

bali mwenye dhambi atanaswa naye.

27 Mhubiri anasema, “Tazama, hili ndilo nililogundua:

“Nimegundua kitu kimoja baada ya kingine nilipokuwa katika kusudi la mambo:

28 ningali natafiti

lakini sipati:

nilimpata mwanaume mmoja mnyofu miongoni mwa elfu,

lakini hakuna mwanamke mmoja mnyofu miongoni mwao.

29 Hili ndilo peke yake nililolipata:

Mungu amemwumba mwanadamu mnyofu,

lakini mwanadamu amebuni mambo mengi.”

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/ECC/7-bb770d9d7fb56c496e8a2f42a0aa51b9.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

14 − three =