Yohana 2

Arusi Huko Kana

1 Siku ya tatu kulikuwa na arusi katika mji wa Kana ya Galilaya, naye mama yake Yesu alikuwako huko.

2 Yesu pamoja na wanafunzi wake walikuwa wamealikwa arusini pia.

3 Divai ilipokwisha, mama yake Yesu akamwambia, “Wameishiwa na divai.”

4 Yesu akamwambia, “Mwanamke, nina nini nawe? Saa yangu haijawadia.”

5 Mama yake akawaambia wale watumishi, “Lo lote atakalowaambia, fanyeni.”

6 Basi ilikuwapo huko mitungi sita ya kuhifadhia maji iliyotengenezwa kwa mawe kwa ajili ya kujitakasa kwa desturi ya Kiyahudi, kila mtungi ungeweza kuchukua vipipa viwili au vitatu.

7 Yesu akawaambia wale watumishi, “Ijazeni hiyo mitungi maji.” Nao wakaijaza ile mitungi mpaka juu.

8 Kisha akawaambia, “Sasa choteni hayo maji kidogo, mpelekeeni mkuu wa meza.”

Hivyo wakachota, wakampelekea.

9 Yule mkuu wa meza akayaonja yale maji ambayo yalikuwa yamebadilika kuwa divai. Hakujua divai hiyo ilikotoka ingawa wale watumishi waliochota yale maji wao walifahamu. Basi akamwita bwana arusi kando

10 akamwambia, “Watu wote hutoa kwanza divai nzuri, kisha huleta ile divai hafifu wageni wakisha kunywa vya kutosha, lakini wewe umeiweka ile nzuri kupita zote mpaka sasa.”

11 Huu, ndio uliokuwa mwujiza wa kwanza Yesu aliofanya huko Kana ya Galilaya. Hivyo Yesu alidhihirisha utukufu wake na wanafunzi wake wakamwamini.

Yesu Atakasa Hekalu

12 Baada ya hayo, Yesu pamoja na mama yake, ndugu zake na wanafunzi wake, walishuka mpaka Kapernaumu wakakaa huko siku chache.

13 Ilipokaribia wakati wa Pasaka ya Wayahudi, Yesu alipanda kwenda Yerusalemu.

14 Huko Hekaluni aliwakuta watu wakiuza ng’ombe, kondoo na njiwa na wengine walikuwa wameketi mezani wakibadili fedha.

15 Akatengeneza mjeledi kutokana na kamba, akawafukuza wote kutoka kwenye eneo la Hekalu pamoja na kondoo na ng’ombe. Akazipindua meza za wale wabadili fedha na kuzimwaga fedha zao.

16 Akawaambia wale waliokuwa wakiuza njiwa, “Waondoeni hapa! Mnathubutuje kuifanya nyumba ya Baba yangu kuwa mahali pa biashara?”

17 Wanafunzi wake wakakumbuka kuwa imeandikwa: “Wivu wa nyumba yako utanila.”

18 Ndipo Wayahudi wakamwuliza, “Unaweza kutuonyesha ishara gani ili kuthibitisha mamlaka uliyo nayo ya kufanya mambo haya?”

19 Yesu akawajibu, “Libomoeni hili Hekalu, nami nitalijenga tena kwa siku tatu!”

20 Wale Wayahudi wakamjibu, “Hekalu hili lilijengwa kwa muda wa miaka arobaini na sita, nawe wasema utalijenga kwa siku tatu?”

21 Lakini yeye Hekalu alilozungumzia ni mwili wake.

22 Baada ya kufufuka kutoka kwa wafu, wanafunzi wake wakakumbuka yale aliyokuwa amesema. Ndipo wakayaamini Maandiko na yale maneno Yesu aliyokuwa amesema.

23 Ikawa Yesu alipokuwa Yerusalemu kwenye Sikukuu ya Pasaka, watu wengi waliona ishara na miujiza aliyokuwa akifanya, wakamwamini.

24 Lakini Yesu hakujiaminisha kwao kwa sababu aliwajua wanadamu wote.

25 Hakuhitaji ushuhuda wa mtu ye yote kuhusu mtu, kwa kuwa alijua yote yaliyokuwa moyoni mwa mtu.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/JHN/2-48bc4dbf98cb12b7d01420aee1805e03.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

three − 1 =