2 Petro 2

Walimu Wa Uongo Na Uangamivu Wao

1 Lakini pia waliinuka manabii wa uongo miongoni mwa watu, kama vile watakavyokuwako walimu wa uongo miongoni mwenu, ambao kwa siri, wataingiza mafundisho yasiyopatana na kweli hata kumkana Bwana wa pekee aliyewanunua na kujiletea juu yao maangamizi ya haraka.

2 Hata hivyo, wengi watafuata njia zao za ufisadi ambao kwa ajili yao njia ya kweli itatukanwa.

3 Nao katika tamaa zao mbaya, watajipatia faida kwenu kwa maneno ya madanganyo waliyotunga wenyewe. Lakini hukumu imekwisha kutangazwa dhidi yao tangu zamani, ambayo haikawii wala uangamivu wao haujalala usingizi.

4 Kwa maana kama Mungu hakuwasamehe malaika walipotenda dhambi, bali aliwatupa kuzimu, katika vifungo vya giza wakae humo mpaka ije hukumu;

5 kama hakuusamehe ulimwengu wa kale alipoleta gharika juu ya watu wale wasiomcha Mungu, akamhifadhi Noa, mhubiri wa haki, pamoja na watu wengine saba;

6 kama aliihukumu miji ya Sodoma na Gomora kwa kuiteketeza kwa moto ikawa majivu na kuifanya kuwa kielelezo kwa yale yatakayowapata wale wasiomcha Mungu

7 na kama alimwokoa Loti, mtu mwenye haki, ambaye alihuzunishwa na maisha machafu ya watu wapotovu

8 (kwa sababu yale matendo mapotovu aliyoyaona na kuyasikia huyo mtu mwenye haki alipoishi miongoni mwao yalimhuzunisha siku baada ya siku),

9 ikiwa hivyo ndivyo, basi Bwana anajua jinsi ya kuwaokoa wacha Mungu kutoka katika majaribu na kuwaweka waasi katika adhabu hadi siku ya hukumu.

10 Hii ni hakika hasa kwa wale wanaofuata tamaa mbaya za mwili na kudharau mamlaka.

Kwa ushupavu na kwa kiburi watu hawa hawaogopi kunena mabaya dhidi ya viumbe vya mbinguni,

11 lakini hata malaika, ingawa wana nguvu na uwezo zaidi, hawaleti mashtaka dhidi ya viumbe kama hao mbele za Bwana.

12 Lakini watu hawa hukufuru katika mambo wasiyoyafahamu. Wao ni kama wanyama wasio na akili, viumbe wanaotawaliwa na hisia za mwili, waliozaliwa ili wakamatwe na kuchinjwa. Hawa nao kama wanyama wataangamizwa pia.

13 Watalipwa madhara kwa ajili ya madhara waliyowatendea wengine. Huhesabu kuwa ni fahari kufanya karamu za ulevi na ulafi mchana peupe. Wao ni mawaa na dosari, wakijifurahisha katika anasa zao wanaposhiriki katika karamu zenu.

14 Wakiwa na macho yaliyojaa uzinzi, kamwe hawaachi kutenda dhambi. Huwashawishi wale wasio imara, wao ni hodari kwa kutamani, wana wa laana!

15 Wameiacha njia iliyonyoka, wakapotoka na kuifuata njia ya Balaamu mwana wa Beori aliyependa mshahara wa uovu.

16 Lakini Balaamu kwa ajili ya uovu wake, alikemewa na punda, mnyama asiyejua kusema, akaongea akitumia sauti ya mwanadamu na kuzuia wazimu wa huyo nabii.

17 Watu hawa ni chemchemi zisizo na maji na ukungu upeperushwao na tufani, ambao giza nene limewekwa tayari kwa ajili yao.

18 Kwa maana wao hunena maneno makuu mno ya upumbavu na kwa tamaa mbaya za uasherati huwashawishi watu ambao ndipo tu wamejiondoa miongoni mwa wale wanaoishi katika ufisadi.

19 Huwaahidi uhuru hao waliowanasa, wakati wao wenyewe ni watumwa wa ufisadi. Kwa maana mtu ni mtumwa wa kitu cho chote kinachomtawala.

20 Kwa kuwa kama wameukimbia upotovu wa dunia kwa kumjua Bwana wetu na Mwokozi Yesu Kristo, kisha wakanaswa tena humo na kushindwa, hali yao ya mwisho ni mbaya zaidi kuliko ile ya kwanza.

21 Ingelikuwa afadhali kwao kama wasingeliijua kamwe njia ya haki, kuliko kuijua kisha wakaiacha ile amri takatifu waliyokabidhiwa.

22 Imetukia kwao sawasawa na ile mithali ya kweli isemayo: “Mbwa ameyarudia matapishi yake mwenyewe,” tena nyingine yasema, “Nguruwe aliyeoshwa amerudi kugaagaa matopeni.”

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/2PE/2-65ea23a992cbf57b7e114cf8cb1ea166.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

20 − 20 =