Wakolosai 3

Kanuni Za Kuishi Maisha Matakatifu

1 Basi, kwa kuwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu, Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu.

2 Yafikirini mambo yaliyo juu, wala si ya duniani.

3 Kwa maana ninyi mlikufa, nao uhai wenu sasa umefichwa pamoja na Kristo katika Mungu.

4 Wakati Kristo atakapotokea yeye aliye uzima wenu ndipo nanyi mtakapotokea pamoja naye katika utukufu.

5 Kwa hiyo, ueni kabisa cho chote kilicho ndani yenu cha asili ya kidunia: Yaani, uasherati, uchafu, tamaa mbaya, mawazo mabaya na kutamani, ambayo ndiyo ibada ya sanamu.

6 Kwa sababu ya mambo haya, ghadhabu ya Mungu inakuja.

7 Ninyi pia zamani mlienenda katika mambo haya mlipoishi maisha hayo.

8 Lakini sasa yawekeni mbali nanyi mambo kama haya yote, yaani: Hasira, ghadhabu, uovu, masingizio na lugha chafu kutoka midomoni mwenu.

9 Msiambiane uongo kwa maana mmevua kabisa utu wenu wa kale pamoja na matendo yake,

10 nanyi mmevaa utu mpya unaofanywa upya katika ufahamu sawasawa na mfano wa Muumba wake.

11 Hapa hakuna Myunani wala Myahudi, aliyetahiriwa wala asiyetahiriwa, asiyestaarabika wala aliyestaarabika, mtumwa wala mtu huru, bali Kristo ni yote na ndani ya wote.

12 Kwa hiyo, kwa kuwa ninyi mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu, wapendwao sana, jivikeni moyo wa huruma, utu wema, unyenyekevu, upole na uvumilivu.

13 Vumilianeni na kusameheana. Mtu akiwa na lalamiko lo lote dhidi ya mwenzake, sameheaneni kama vile Bwana alivyowasamehe ninyi.

14 Zaidi ya maadili haya yote jivikeni upendo, ambao ndio unaofunga kila kitu pamoja katika umoja mkamilifu.

15 Amani ya Kristo na itawale mioyoni mwenu, kwa kuwa ninyi kama viungo vya mwili mmoja mmeitiwa amani. Tena iweni watu wa shukrani.

16 Neno la Kristo na likae kwa wingi ndani yenu, mkifundishana na kuonyana katika hekima yote, mkimwimbia Mungu zaburi, nyimbo na tenzi za rohoni huku mkiwa na shukrani mioyoni mwenu.

17 Lo lote mfanyalo, ikiwa ni kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika Jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba katika yeye.

Kanuni Katika Madaraka Ya Nyumbani

18 Ninyi wake, watiini waume zenu, kama inavyostahili katika Bwana.

19 Ninyi waume, wapendeni wake zenu, wala msiwe na uchungu dhidi yao.

20 Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika mambo yote, kwa maana hivi ndivyo inavyompendeza Bwana.

21 Ninyi akina baba msiwachokoze watoto wenu, wasije wakakata tamaa.

22 Ninyi watumwa, watiini mabwana zenu wa hapa duniani katika mambo yote. Fanyeni hivyo si wakiwepo tu, bali mkimwogopa Mungu, wala si kwa kutafuta upendeleo wao wakati wanapowaona.

23 Lo lote mfanyalo, fanyeni kwa moyo kama watu wanaomtumikia Bwana na si wanadamu.

24 Kwa kuwa mnajua kwamba mtapokea urithi wenu kutoka kwa Bwana kuwa thawabu yenu. Ni Bwana Yesu Kristo mnayemtumikia.

25 Ye yote atendaye mabaya atalipwa kwa ajili ya mabaya yake, wala hakuna upendeleo.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/COL/3-8cca7b89906432ece482487c00ec4398.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

18 + 11 =