Wimbo Ulio Bora 2

1 Mimi ni ua la waridi la Sharoni,

yungiyungi ya bondeni. Mpenzi

2 Kama yungiyungi katikati ya miiba

ndivyo alivyo mpenzi wangu katikati ya wanawali.

3 Kama mti wa mtofaa miongoni mwa miti ya msituni

ndivyo alivyo mpenzi wangu

miongoni mwa wanaume vijana.

Ninafurahia kuketi kivulini mwa mwanaume huyu,

na tunda lake ni tamu kwangu.

4 Amenichukua mpaka kwenye ukumbi wa karamu,

na bendera ya huyu mwanaume

juu yangu ni upendo.

5 Nitie nguvu kwa zabibu kavu,

niburudishe kwa matofaa,

kwa maana ninazimia kwa mapenzi.

6 Mkono wa kushoto uko chini ya kichwa changu,

na mkono wake wa kuume unanikumbatia.

7 Binti za Yerusalemu, ninawaagiza

kwa paa na kwa ayala wa shambani:

Msichochee wala kuamsha mapenzi

hata yatakapotaka yenyewe.

8 Sikiliza! Mpenzi wangu!

Tazama! Huyu hapa anakuja,

akirukaruka juu milimani

akizunguka juu ya vilima.

9 Mpenzi wangu ni kama paa au swala kijana.

Tazama! Anasimama nyuma ya ukuta wetu,

akitazama kupitia madirishani,

akichungulia kimiani.

10 Mpenzi wangu alizungumza na kuniambia,

“Inuka, mpenzi wangu,

mrembo wangu, tufuatane.

11 Tazama! Wakati wa masika umepita,

mvua imekwisha imekwenda zake.

12 Maua yanatokea juu ya nchi;

majira ya kuimba yamewadia,

sauti za njiwa zinasikika

katika nchi yetu.

13 Mtini unatunga matunda yake ya mwanzoni,

zabibu zinazochanua zaeneza harufu yake nzuri.

Inuka, njoo, mpenzi wangu,

mrembo wangu, tufuatane.”

14 Hua wangu penye nyufa za majabali,

mafichoni pembezoni mwa mlima,

nionyeshe uso wako,

na niisikie sauti yako,

kwa maana sauti yako ni tamu,

na uso wako unapendeza.

15 Tukamatie mbweha,

mbweha wadogo wale

wanaoharibu mashamba ya mizabibu,

mashamba yetu ya mizabibu yaliyochanua.

16 Mpenzi wangu ni wangu, nami ni wake,

hujilisha katikati ya yungiyungi.

17 Mpaka jua linapochomoza,

na vivuli vikimbie,

rudi, mpenzi wangu,

na uwe kama paa,

au kama ayala kijana

juu ya vilima vya Betheri.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/SNG/2-e8bb73f313408f6ed2c4314bc12546ae.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

one × three =