1 Usiku kucha kwenye kitanda changu
nilimtafuta yule moyo wangu umpendaye;
nilimtafuta huyo mwanaume lakini sikumpata.
2 Sasa nitaondoka na kuzunguka mjini,
kupitia katika barabara zake
na viwanjani;
nitamtafuta yule moyo wangu umpendaye.
Kwa hiyo nilimtafuta
lakini sikumpata huyo mwanaume.
3 Walinzi walinikuta
walipokuwa wakizunguka mji.
Nikawauliza, “Je, mmemwona
yule moyo wangu umpendaye?”
4 Kitambo kidogo tu baada ya kuwapita
nilimpata yule moyo wangu umpendaye.
Nilimshika na sikumwachia aende mpaka nilipomleta
katika nyumba ya mama yangu,
katika chumba cha yule aliyenichukua mimba.
5 Binti za Yerusalemu, ninawaagiza
kwa paa na kwa ayala wa shambani:
Msichochee wala kuamsha mapenzi
hata yatakapotaka yenyewe.
6 Ni nani huyu anayekuja kutoka jangwani
kama nguzo ya moshi,
anayenukia manemane na uvumba
iliyotengenezwa kwa vikolezo vyote
vya mfanyabiashara?
7 Tazama! Ni gari la Solomoni
lisindikizwalo na mashujaa sitini,
walio wakuu sana wa Israeli,
8 wote wamevaa panga,
wote wazoefu katika vita,
kila mmoja na upanga wake pajani,
wamejiandaa kwa ajili ya hofu za usiku.
9 Mfalme Solomoni alijitengenezea gari;
alitengeneza kwa mbao kutoka Lebanoni.
10 Nguzo zake alitengeneza za fedha,
kitako chake kwa dhahabu.
Kiti chake kilikuwa kimepambwa kwa zambarau,
gari lake limenakishiwa njumu,
kwa ndani limefunikwa kwa upendo
wa binti za Yerusalemu.
11 Tokeni nje, ninyi binti za Sayuni,
mumtazame Mfalme Solomoni
akiwa amevaa taji,
taji ambalo mama yake alimvika
siku ya arusi yake,
siku ambayo moyo wake ulishangilia.
—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/SNG/3-92b9f3c5a11759d9568a6fa395eeeddb.mp3?version_id=1627—