1 Mpenzi wako amekwenda wapi,
yule mzuri kupita wanawake wote?
Mpenzi wako amegeukia njia ipi,
tupate kumtafuta pamoja nawe?
2 Mpenzi wangu amekwenda bustanini mwake,
kwenye vitalu vya vikolezo,
kujilisha bustanini
na kukusanya yungiyungi.
3 Mimi ni wake mpenzi wangu,
na mpenzi wangu ni wangu mimi;
huyu mwanaume hulisha katikati ya yungiyungi.
4 Wewe ni mzuri, mpenzi wangu, kama Tirza,
upendezaye kama Yerusalemu,
umetukuka kama jeshi lenye bendera.
5 Uyageuze macho yako mbali nami,
yananigharikisha.
Nywele zako ni kama kundi la mbuzi
wanaotelemka kutoka Gileadi.
6 Meno yako ni kama kundi la kondoo
wanaotoka kuogeshwa.
Kila mmoja ana pacha lake,
hakuna hata mmojawapo aliye peke yake.
7 Mashavu yako nyuma ya shela yako
ni kama vipande viwili vya komamanga.
8 Panaweza kuwapo malkia sitini,
masuria themanini
na mabikira wasiohesabika;
9 lakini hua wangu, mkamilifu wangu,
ni wa namna ya pekee,
binti pekee kwa mama yake,
kipenzi cha yeye aliyemzaa.
Wanawali walimwona na kumwita mbarikiwa;
malkia na masuria walimsifu.
10 Ni nani huyu atokeaye kama mapambazuko,
mzuri kama mwezi, mwangavu kama jua,
ametukuka kama majeshi yenye bendera?
11 Nilitelemka kwenye kichaka cha miti ya milozi
ili kutazama machipuko ya bondeni,
kuona kama mizabibu imechipua
au kama mikomamanga imechanua maua.
12 Kabla sijang’amua,
shauku yangu iliniweka
katikati ya magari ya kifalme ya kukokotwa na farasi.
13 Rudi, rudi, Ee Mshulami;
rudi, rudi ili tupate kukutazama!
Kwa nini kumtazama Mshulami,
# kama kutazama ngoma ya Mahanaimu?
—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/SNG/6-6e5ca2b6b3f2cbc660fcf8246dd18bce.mp3?version_id=1627—