1 Laiti ungelikuwa kwangu kama ndugu wa kiume,
ambaye aliyanyonya matiti ya mama yangu!
Kisha, kama ningekukuta huko nje,
ningelikubusu,
wala hakuna mtu ye yote angelinidharau.
2 Ningelikuongoza na kukuleta
katika nyumba ya mama yangu,
yeye ambaye amenifundisha.
Ningelikupa divai iliyokolezwa unywe,
asali ya maua ya mikomamanga yangu.
3 Mkono wa kushoto wa huyo mwanaume
uko chini ya kichwa changu,
na mkono wake wa kuume unanikumbatia.
4 Binti za Yerusalemu, ninawaagiza:
msichochee wala kuamsha mapenzi
hata yatakapotaka yenyewe.
5 Ni nani huyu anayekuja kutoka nyikani
akimwegemea mpenzi wake?
Nilikuamsha chini ya mtofaa,
huko mama yako alipotunga mimba yako,
huko yeye alipata utungu akakuzaa.
6 Nitie kama muhuri moyoni mwako,
kama muhuri kwenye mkono wako;
kwa maana upendo una nguvu kama mauti,
wivu wake ni mkatili kama kuzimu.
Unachoma kama mwali wa moto,
kama mwali mkubwa wa moto waBwanahasa.
7 Maji mengi hayawezi kuuzimisha upendo,
mito haiwezi kuugharikisha.
Kama mtu angelitoa mali yote ya nyumbani mwake
kwa ajili ya upendo,
angelidharauliwa kabisa.
8 Tunaye dada mdogo,
matiti yake hayajakua bado.
Tutafanya nini kwa ajili ya dada yetu
wakati atakapokuja kuposwa?
9 Kama yeye ni ukuta,
tutajenga minara ya fedha juu yake.
Na kama yeye ni mlango,
tutamzungushia mbao za mierezi.
10 Mimi ni ukuta,
nayo matiti yangu ni kama minara.
Ndivyo ambavyo nimekuwa machoni pake
kama yule anayeleta utoshelevu.
11 Solomoni alikuwa na shamba la mizabibu huko Baal-Hamoni;
alikodisha shamba lake la mizabibu kwa wapangaji.
Kila mmoja angeleta kwa ajili ya matunda yake
# shekeli 1,000za fedha.
12 Lakini shamba langu la mizabibu
ambalo ni langu mwenyewe
ni langu kutoa;
hizo shekeli 1,000 ni kwa ajili yako, Ee Solomoni,
# na shekeli mia mbili
ni kwa ajili ya wale wanaotunza matunda yake.
13 Wewe ukaaye bustanini
pamoja na marafiki mliohudhuria,
unisikizishe na mimi sauti yako!
14 Njoo, mpenzi wangu,
uwe kama swala
au kama ayala mdogo
juu ya milima iliyojaa vikolezo.
—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/SNG/8-300629cf01a2155acb27cbc174e33610.mp3?version_id=1627—