2 Wafalme 10

Jamii Ya Ahabu Yauawa

1 Wakati huu katika Samaria walikuwepo wana sabini wa nyumba ya Ahabu. Kwa hiyo Yehu akaandika barua na kuzituma Samaria kwa: Maafisa wa Yezreeli, kwa wazee na kwa walezi wa watoto wa Ahabu. Akasema,

2 “Mara tu barua hii itakapokufikia, kwa kuwa wana wa bwana wako wapo pamoja nawe, nawe una magari ya vita na farasi, mji wenye ngome na silaha,

3 mchague mwenye uwezo zaidi kati ya wana wa bwana wako na umweke juu ya kiti cha enzi cha baba yake. Kisha upigane kwa ajili ya nyumba ya bwana wako.”

4 Lakini wakaogopa sana na kusema, “Ikiwa wafalme wawili hawakuweza kupambana na Yehu, sisi tutawezaje?”

5 Basi msimamizi wa jumba la kifalme, mtawala wa mji, wazee na walezi wakatuma ujumbe huu kwa Yehu: “Sisi tu watumishi wako na tutafanya kila kitu utakachosema. Hatutamteuwa mtu ye yote kuwa mfalme, wewe fanya uonalo kuwa ni bora.”

6 Kisha Yehu akawaandikia barua ya pili, akisema, “Ikiwa ninyi mko upande wangu na mtanitii mimi, twaeni vichwa vya wana wa bwana wenu na mnijie huku Yezreeli kesho wakati kama huu.”

Wakati huo wana sabini wa kifalme, walikuwa wakiishi pamoja na viongozi wa mji wa Samaria, ambao walikuwa wakiwalea.

7 Hiyo barua ilipowafikia, watu hawa wakawachukuwa wale wana sabini wa mfalme na kuwachinja wote. Wakaweka vichwa vyao ndani ya makapu na kumpelekea Yehu huko Yezreeli.

8 Mjumbe alipofika, akamwambia Yehu, “Wameleta vichwa vya wana wa mfalme.”

Ndipo Yehu akaagiza, “Viwekeni katika marundo mawili katika ingilio la lango la mji mpaka asubuhi.”

9 Asubuhi yake, Yehu akatoka nje. Akasimama mbele ya watu wote na akasema, “Hamna hatia. Ni mimi niliyefanya shauri baya dhidi ya bwana wangu na kumwua, lakini ni nani aliyewaua wote hawa?

10 Fahamuni basi kwamba, hakuna neno ambaloBwanaamesema dhidi ya nyumba ya Ahabu ambalo halitatimia.Bwanaamefanya lile aliloahidi kupitia mtumishi wake Eliya.”

11 Hivyo Yehu akaua kila mtu huko Yezreeli aliyekuwa amebaki wa nyumba ya Ahabu, ikiwa ni pamoja na wakuu wake, rafiki zake wa karibu na makuhani wake, hakuacha ye yote anusurike.

12 Kisha Yehu akaondoka kuelekea Samaria. Alipokuwa njiani karibu na nyumba ya kukatia manyoya ya kondoo, yaani, Beth-Ekedi ya wachunga kondoo,

13 Yehu akakutana na watu wa jamaa ya Ahazia mfalme wa Yuda akauliza, “Ninyi ni nani?”

Wao wakasema, “Sisi ni jamaa ya Ahazia, nasi tumeshuka kuwasalimu jamaa ya mfalme na ya mama malkia.”

14 Yehu akaagiza, “Wakamateni wakiwa hai!” Kwa hiyo wakawachukua wakiwa hai, watu arobaini na wawili, na kuwachinja kando ya kisima cha Beth-Ekedi. Hakuacha ye yote anusurike.

15 Baada ya kuondoka hapo, alimkuta Yehonadabu mwana wa Rekabu, aliyekuwa akienda kumlaki. Yehu akamsalimu na kusema, “Je, moyo wako ni mnyofu kwangu kama moyo wangu ulivyo kwako?”

Yehonadabu akajibu, “Ndiyo.”

Yehu akasema, “Kama ndivyo, nipe mkono wako.” Yeye akampa mkono, naye Yehu akampandisha kwenye gari lake la vita.

16 Yehu akasema, “Twende pamoja ukaone wivu wangu kwa ajili yaBwana.” Hivyo wakasafiri pamoja kwenye gari lake.

17 Yehu alipofika Samaria, akawaua wale wote waliokuwa wamesalia wa jamaa ya Ahabu, akawaangamiza, sawasawa na neno laBwanaalilosema kwa kupitia Eliya.

Watumishi Wa Baali Wauawa

18 Kisha Yehu akawaleta watu wote pamoja na kuwaambia, “Ahabu alimtumikia Baali kidogo, Yehu atamtumikia zaidi.

19 Sasa waiteni manabii wote wa Baali, watumishi wake wote na makuhani wake wote. Hakikisheni kwamba hakuna hata mmoja atakayekosekana, kwa sababu ninakwenda kutoa kafara kubwa sana kwa Baali. Ye yote atakayeshindwa kuja hataendelea kuishi.” Lakini Yehu alifanya hivyo kwa hila ili apate kuwaangamiza watumishi wote wa Baali.

20 Yehu akasema, “Itisheni kusanyiko kwa heshima ya Baali.” Basi wakatangaza jambo hilo.

21 Kisha akapeleka ujumbe katika Israeli yote na watumishi wote wa Baali wakaja, hakuna hata mmoja ambaye hakufika. Wakasongana ndani ya hekalu la Baali mpaka likajaa tangu mwanzo hadi mwisho wake.

22 Naye Yehu akamwambia yule aliyekuwa mtunza chumba cha mavazi, “Leta majoho kwa ajili ya watumishi wote wa Baali.” Basi akawaletea majoho.

23 Kisha Yehu na Yehonadabu mwana wa Rekabu wakaingia ndani ya hekalu la Baali. Yehu akawaambia watumishi wa Baali, “Tazameni kila mahali mhakikishe kwamba hakuna hata mtumishi mmoja waBwanaaliye hapa pamoja nanyi, wawe ni watumishi wa Baali tu.”

24 Kwa hiyo wakaingia ndani ili kutoa kafara na sadaka ya kuteketezwa. Wakati huu, Yehu alikuwa amewaweka watu wake themanini akiwa amewapa onyo kwamba, “Ikiwa mmoja wenu atamwachia mtu ye yote ninayemweka mikononi mwake atoroke, itakuwa uhai wako kwa uhai wake.”

25 Mara baada ya Yehu kutoa sadaka ya kuteketezwa akawaamuru walinzi na maafisa: “Ingieni ndani, waueni; asitoroke hata mmoja.” Basi wakawakatakata kwa upanga. Walinzi na maafisa wakazitupa zile maiti nje na kisha wakaingia mahali pa ndani pa kuabudia miungu katika hekalu la Baali.

26 Wakaileta ile nguzo ya kuabudiwa nje ya hekalu la Baali na wakaichoma moto.

27 Wakabomoa ile nguzo ya kuabudiwa ya Baali pamoja na hekalu la Baali, nao watu wakapafanya kuwa choo hadi leo.

28 Kwa hiyo Yehu akaangamiza kuabudiwa kwa Baali katika Israeli.

29 Hata hivyo, hakuziacha dhambi za Yeroboamu mwana wa Nebati, ambazo alikuwa amesababisha Israeli kuzitenda, yaani, kuabudu ndama za dhahabu huko Betheli ya Dani.

30 Bwanaakamwambia Yehu, “Kwa kuwa umefanya vyema kwa kutimiza yaliyo sawa machoni pangu na umetenda kwa nyumba ya Ahabu yale yote niliyokuwa nimekusudia kutenda, wazao wako wataketi juu ya kiti cha enzi cha Israeli hadi kizazi cha nne.”

31 Lakini Yehu hakuwa mwangalifu kushika sheria zaBwana, Mungu wa Israeli, kwa moyo wake wote. Hakuziacha dhambi za Yeroboamu, ambazo alikuwa amesababisha Israeli kuzitenda.

32 Katika siku hizo,Bwanaakaanza kupunguza ukubwa wa Israeli. Hazaeli akawashinda Waisraeli sehemu zote za nchi yao

33 mashariki ya Yordani katika nchi yote ya Gileadi (eneo la Gadi, Reubeni na Manase), kutoka Aroeri karibu na Bonde la Arnoni kupitia Gileadi hadi Bashani.

34 Kwa matukio mengine ya utawala wa Yehu, yote aliyofanya na mafanikio yake yote, je, hayakuandikwa katika kitabu cha kumbukumbu cha wafalme wa Israeli?

35 Yehu akalala pamoja na baba zake naye akazikwa huko Samaria. Naye Yehoahazi mwanawe akaingia mahali pake kuwa mfalme badala yake.

36 Muda Yehu aliotawala juu ya Israeli huko Samaria ilikuwa miaka ishirini na minane.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/2KI/10-39c42e8055d8fe053eeeace2fb8aa4a6.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

6 − one =