Ezekieli 29

Unabii Dhidi Ya Misri

1 Katika mwaka wa kumi, mwezi wa kumi, siku ya kumi na mbili, neno laBwanalikanijia kusema:

2 “Mwanadamu, elekeza uso wako juu ya Farao mfalme wa Misri na utabiri dhidi yake na dhidi ya Misri yote.

3 Nena, nawe useme: ‘Hili ndiloBwanaMwenyezi asemalo:

“ ‘Mimi ni kinyume nawe, Farao, mfalme wa Misri,

joka kubwa ulalaye katikati ya vijito vyako.

Unasema, “Mto Nile ni wangu mwenyewe;

niliufanya kwa ajili yangu mwenyewe.”

4 Lakini nitatia ndoana katika mataya yako

nami nitawafanya samaki wa vijito vyako

washikamane na magamba yako.

Nitakutoa katikati ya vijito vyako,

pamoja na samaki wote

walioshikamana na magamba yako.

5 Nitakutupa jangwani,

wewe pamoja na samaki wote wa vijito vyako.

Utaanguka uwanjani,

nawe hutakusanywa au kuchukuliwa.

Nitakutoa uwe chakula

kwa wanyama wa nchi

na ndege wa angani.

6 Ndipo wale wote waishio Misri watakapojua kuwa Mimi ndimiBwana.

“ ‘Umekuwa fimbo ya tete kwa nyumba ya Israeli.

7 Walipokushika kwa mikono yao, ulivunjika na kuchana mabega yao, walipokuegemea, ulivunjika na migongo yao ikateguka.

8 “ ‘Kwa hiyo hili ndiloBwanaMwenyezi asemalo: Nitaleta upanga juu yako na kuua watu wako na wanyama wao.

9 Misri itakuwa ukiwa na isiyolimwa wala kukaliwa na watu. Ndipo watakapojua kuwa Mimi ndimiBwana.

“ ‘Kwa sababu ulisema, “Mto Nile ni wangu; mimi niliufanya,”

10 kwa hiyo mimi ni kinyume nawe na kinyume na vijito vyako, nami nitaifanya nchi ya Misri kuwa magofu na ukiwa isiyolimwa wala kukaliwa na watu kuanzia Migdoli hadi Aswani, hata kufikia mpakani wa Ethiopia.

11 Hakuna unyayo wa mtu au mnyama utakaopita ndani yake, wala hakuna ye yote atakayeishi humo kwa muda wa miaka arobaini.

12 Nitaifanya nchi ya Misri ukiwa, miongoni mwa nchi zilizo ukiwa, nayo miji yake itabaki ukiwa miaka arobaini miongoni mwa miji iliyo magofu. Nami nitawatawanya Wamisri miongoni mwa mataifa na kuwafukuza huko na huko katika nchi nyingine.

13 “ ‘Lakini hili ndiloBwanaMwenyezi asemalo: Mwishoni mwa hiyo miaka arobaini, nitawakusanya Wamisri kutoka katika mataifa walikotawanywa.

14 Nitawarudisha kutoka kwenye kutekwa kwao na kuwaweka katika Pathrosi, nchi ya baba zao. Huko watakuwa na ufalme usiokuwa na nguvu.

15 Utakuwa ufalme dhaifu kuliko zote na kamwe Misri haitajikweza tena juu ya mataifa mengine. Nitaufanya ufalme wake dhaifu sana kiasi kwamba kamwe hautatawala tena juu ya mataifa mengine.

16 Misri haitakuwa tena tumaini la watu wa Israeli bali itakuwa kumbukumbu ya dhambi yao kwa kuigeukia kuomba msaada. Ndipo watakapojua kuwa Mimi ndimiBwanaMwenyezi.’ ”

17 Katika mwaka wa ishirini na saba, mwezi wa kwanza, siku ya kwanza, neno laBwanalikanijia, kusema:

18 “Mwanadamu, Nebukadneza mfalme wa Babeli aliongoza jeshi lake kufanya kazi ngumu dhidi ya Tiro; kila kichwa kilipata upaa na kila bega likachunika. Lakini yeye na jeshi lake hawakupata malipo yo yote kutokana na muda wote alioongoza hiyo vita dhidi ya Tiro.

19 Kwa hiyo hili ndiloBwanaMwenyezi asemalo: Nitaitia Misri mikononi mwa Nebukadneza mfalme wa Babeli, naye atachukua utajiri wa Misri. Atateka mateka na kuchukua nyara mali za Misri kama ujira kwa ajili ya jeshi lake.

20 Nimempa mfalme wa Babeli nchi ya Misri kuwa ujira kwa juhudi zake kwa sababu yeye na jeshi lake walifanya kwa ajili yangu, asemaBwanaMwenyezi.

21 “Katika siku hiyo nitaifanya nyumba ya Israeli iwe na nguvu nami nitakifungua kinywa chako miongoni mwao. Ndipo watakapojua kwamba Mimi ndimiBwana.”

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/EZK/29-5437dd410916fae9f64647825480fa5b.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

12 + six =