Maombi Ya Habakuki
1 Sala ya nabii Habakuki iliyoimbwa kwa shigionothi.
2 Bwana, nimezisikia sifa zako,
nami naogopa, EeBwana.
Fufua kazi yako katikati ya miaka,
katikati ya miaka tangaza habari yako;
katika ghadhabu kumbuka rehema.
3 Mungu alitoka Temani,
yeye aliye Mtakatifu kutoka Mlima Parani.
Utukufu wake ulifunika mbingu
na sifa zake zikaifunika dunia.
4 Mng’ao wake ulikuwa kama jua lichomozalo,
mionzi ilimulika kutoka mkononi mwake,
ambako nguvu zake zilifichwa.
5 Tauni ilimtangulia;
maradhi ya kuambukiza
yalifuata nyayo zake.
6 Alisimama, akaitikisa dunia;
alitazama, na kuyafanya mataifa yatetemeke.
Milima ya zamani iligeuka mavumbi
na vilima vilivyozeeka vikaanguka.
Njia zake ni za milele.
7 Niliona watu wa Kushani katika dhiki,
na makazi ya Midiani katika maumivu makali.
8 EeBwana, uliikasirikia mito?
Je, ghadhabu yako ilikuwa dhidi ya vijito?
Je, ulighadhibikia bahari ulipoendesha farasi
wako na magari yako ya ushindi?
9 Uliufunua upindi wako
na kuita mishale mingi.
Uliigawa dunia kwa mito;
10 milima ilikuona ikatetemeka.
Mafuriko ya maji yakapita huko;
vilindi vilinguruma
na kuinua mawimbi yake juu.
11 Jua na mwezi vilisimama kimya mbinguni
katika mng’ao wa mishale yako inayoruka,
na katika mng’ao wa mkuki wako umeremetao.
12 Kwa ghadhabu ulipita juu ya dunia
na katika hasira ulikanyaga mataifa.
13 Ulikuja kuwaokoa watu wako,
kumwokoa masiya wako.
Ulimponda kiongozi wa nchi ya uovu,
ukamvua toka kichwani hadi wayo.
14 Kwa mkuki wake mwenyewe ulitoboa kichwa chake
wakati mashujaa wake
walipofurika nje kwa kishindo kututawanya,
wakifurahi kama waliokaribu kutafuna
wale wanyonge waliokuwa mafichoni.
15 Ulikanyaga bahari kwa farasi wako,
ukisukasuka maji makuu.
16 Nilisikia na moyo wangu ukagonga kwa nguvu,
midomo yangu ikatetemeka kwa hofu
niliposikia sauti;
uchakavu ukanyemelea mifupa yangu,
na miguu yangu ikatetemeka.
Hata hivyo nitasubiri kwa uvumilivu siku ya maafa
kuyajilia mataifa yaliyotuvamia.
17 Ingawa mtini hauchanui maua
na hakuna zabibu juu ya mizabibu,
ingawaje mzeituni hauzai,
na hata mashamba hayatoi chakula,
iwapo hakuna kondoo katika banda
wala ng’ombe katika zizi,
18 hata hivyo nitashangilia katikaBwana,
nitamfurahia Mungu Mwokozi wangu.
19 BwanaMwenyezi ni nguvu yangu;
huifanya miguu yangu kama miguu ya paa,
huniwezesha kupita juu ya vilima.
(Kwa kiongozi wa uimbaji. Kwa vinanda vyangu vya nyuzi.)
—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/HAB/3-bec1d4175c363e1dfe8d2d3391793194.mp3?version_id=1627—