1 Laiti ungelipasua mbingu na kushuka chini,
kwamba milima ingelitetemeka mbele zako!
2 Kama vile moto uteketezavyo vijiti
na kusababisha maji kuchemka,
shuka ukafanye jina lako lijulikane kwa adui zako
na kusababisha mataifa yatetemeke mbele zako!
3 Kwa maana ulipofanya mambo ya kutisha
ambayo hatukuyatazamia,
ulishuka nayo milima ikatetemeka mbele zako.
4 Tangu nyakati za zamani hakuna ye yote aliyesikia,
hakuna sikio lililotambua,
hakuna jicho lililomwona Mungu mwingine ila wewe,
anayetenda mambo kwa ajili ya wale wamngojeao.
5 Uliwasaidia watu wale watendao yaliyo haki kwa furaha,
wale wazikumbukao njia zako.
Lakini wakati tulipoendelea kutenda dhambi kinyume na njia zako,
ulikasirika.
Tutawezaje basi kuokolewa?
6 Sisi sote tumekuwa kama mtu aliye najisi,
nayo matendo yetu yote ya uadilifu
ni kama matambaa machafu;
sisi sote tunasinyaa kama jani
na kama upepo maovu yetu hutupeperusha.
7 Hakuna ye yote anayeliitia jina lako
wala anayejitahidi kukushika,
kwa kuwa umetuficha uso wako
na kutuacha tudhoofike
kwa sababu ya dhambi zetu.
8 Lakini, EeBwana, wewe ndiwe Baba yetu.
Sisi ni udongo wa mfinyanzi
wewe ndiye mfinyanzi;
sisi sote tu kazi ya mkono wako.
9 EeBwana, usikasirike kupita kiasi,
usizikumbuke dhambi zetu milele.
Ee Bwana, utuangalie, twakuomba,
kwa kuwa sisi sote tu watu wako.
10 Miji yako mitakatifu imekuwa jangwa;
hata Sayuni ni jangwa,
Yerusalemu imekuwa ukiwa.
11 Hekalu letu takatifu na tukufu, mahali ambapo baba zetu walikusifu wewe,
limechomwa kwa moto,
navyo vitu vyote tulivyovithamini vimeharibika.
12 EeBwana, baada ya haya yote, utajizuia?
Je, utanyamaza kimya na kutuadhibu kupita kiasi?
—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/ISA/64-c505bafdc93ede5028d0667993427f8b.mp3?version_id=1627—