Mambo ya Walawi 15

Kutokwa Na Umajimaji Usababishao Unajisi

1 Bwanaakawaambia Mose na Aroni,

2 “Semeni na Waisraeli na mkawaambie: ‘Wakati mtu ye yote anapotokwa na usaha mwilini, usaha huo ni najisi.

3 Iwe kwamba unaendelea kutiririka kutoka mwilini mwake au umeziba, utamfanya kuwa najisi. Hivi ndivyo usaha wake utakavyomletea unajisi:

4 “ ‘Kitanda cho chote atakacholala mtu mwenye kutokwa na usaha kitakuwa najisi, na cho chote atakachokalia kitakuwa najisi.

5 Ye yote atakayegusa kitanda chake ni lazima afue nguo zake na aoge kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni.

6 Ye yote atakayeketi juu ya kitu cho chote alichokalia mwenye kutokwa na usaha, ni lazima afue nguo zake, na aoge kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni.

7 “ ‘Ye yote atakayemgusa mtu mwenye kutokwa na usaha ni lazima afue nguo zake na aoge kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni.

8 “ ‘Ikiwa mtu mwenye kutokwa na usaha atamtemea mate mtu ye yote ambaye ni safi, mtu huyo ni lazima afue nguo zake na aoge kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni.

9 “ ‘Kila tandiko ambalo mtu huyo atalikalia wakati wa kupanda mnyama litakuwa najisi

10 na ye yote atakayegusa kitu cho chote alichokuwa amekalia atakuwa najisi mpaka jioni; ye yote atakayeinua vitu hivyo, ni lazima afue nguo zake na aoge kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni.

11 “ ‘Ye yote atakayeguswa na mtu anayetokwa na usaha bila kunawa mikono yake kwa maji, ni lazima afue nguo zake na aoge kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni.

12 “ ‘Chungu cha udongo kitakachoguswa na mtu huyo ni lazima kivunjwe, na kifaa cho chote cha mbao kitaoshwa kwa maji.

13 “ ‘Wakati mtu atakapotakasika kutokwa usaha kwake, anapaswa kuhesabu siku saba za kawaida ya ibada ya utakaso; ni lazima afue nguo zake na aoge kwa maji safi, naye atatakasika.

14 Siku ya nane, atachukua hua wawili au makinda mawili ya njiwa, aje mbele zaBwanakwenye ingilio la Hema la Kukutania na kumpa kuhani.

15 Kuhani atavitoa dhabihu, huyo mmoja kwa ajili ya sadaka ya dhambi na huyo mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. Kwa njia hii atafanya upatanisho mbele zaBwanakwa ajili ya huyo mtu kwa sababu ya kutokwa usaha kwake.

16 “ ‘Wakati mtu akitokwa na shahawa, ni lazima aoge mwili mzima kwa maji, na atakuwa najisi mpaka jioni.

17 Vazi lo lote ama ngozi yenye shahawa juu yake ni lazima ioshwe kwa maji, na itakuwa najisi mpaka jioni.

18 Ikiwa mtu atalala na mwanamke na kukawa na kutoka kwa shahawa, ni lazima wote waoge kwa maji, nao watakuwa najisi mpaka jioni.

19 “ ‘Ikiwa mwanamke atatokwa na damu ya kawaida ya mwezi, atakuwa najisi kwa siku saba, na ye yote atakayemgusa atakuwa najisi mpaka jioni.

20 “ ‘Cho chote atakacholalia wakati wake wa hedhi kitakuwa najisi, na cho chote atakachokikalia kitakuwa najisi.

21 Ye yote atakayegusa kitanda chake ni lazima afue nguo zake na aoge kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni.

22 Ye yote atakayegusa cho chote atakachokalia ni lazima afue nguo zake na aoge kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni.

23 Kiwe ni kitanda ama cho chote alichokuwa amekikalia, ikiwa mtu ye yote atakigusa, atakuwa najisi mpaka jioni.

24 “ ‘Ikiwa mwanaume atalala naye na ile damu ya mwezi ikamgusa, atakuwa najisi kwa siku saba; kitanda cho chote atakachokilalia huyo mwanaume kitakuwa najisi.

25 “ ‘Ikiwa mwanamke atatokwa na damu kwa siku nyingi zaidi ya siku zake za mwezi au amekuwa na damu inayoendelea zaidi ya kipindi chake, atakuwa najisi kwa kipindi chote cha shida hiyo, kama ilivyokuwa katika siku za hedhi yake.

26 Kitanda cho chote atakachokilalia huyo mwanamke wakati akiendelea kutokwa na damu kitakuwa najisi, kama kilivyokuwa kitanda chake wakati wa siku zake za hedhi, na cho chote atakachokalia kitakuwa najisi, kama wakati wake wa hedhi.

27 Ye yote agusaye vitu hivyo atakuwa najisi; ni lazima afue nguo zake na kuoga kwa maji, naye atakuwa najisi mpaka jioni.

28 “ ‘Wakati atakapotakasika kutoka hedhi yake, ni lazima ahesabu siku saba, na baada ya hapo atakuwa safi kwa kawaida ya ibada.

29 Siku ya nane ni lazima achukue hua wawili au makinda mawili ya njiwa na kuyaleta kwa kuhani kwenye mlango wa Hema la Kukutania.

30 Kuhani atatoa dhabihu, huyo mmoja kwa ajili ya sadaka ya dhambi na huyo mwingine kwa ajili ya sadaka ya kuteketezwa. Kwa njia hii, atafanya upatanisho kwa ajili yake mbele zaBwanakwa sababu ya unajisi wa kutokwa damu kwake.

31 “ ‘Ni lazima uwatenge Waisraeli kutokana na vitu ambavyo vinawafanya najisi, ili wasife katika unajisi wao kwa kunajisi makao yangu, ambayo yapo katikati yao.’ ”

32 Haya ni masharti kwa ajili ya mtu mwenye kutokwa na usaha, kwa ajili ya ye yote atakayetokwa na shahawa,

33 kwa ajili ya mwanamke katika siku zake za hedhi, kwa ajili ya mwanaume au mwanamke atokwaye na usaha, na kwa ajili ya mwanaume alalaye na mwanamke ambaye ni najisi kwa kawaida ya ibada.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/LEV/15-e0b1759006a404cd259c5b1906a3978a.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

2 × 3 =