Nehemiah 4

Upinzani Wakati Wa Ujenzi

1 Sanbalati aliposikia kwamba tulikuwa tunajenga upya ukuta, alikasirika na akawa na uchungu sana. Aliwadhihaki Wayahudi,

2 mbele ya rafiki zake na jeshi la Samaria, akisema, “Hawa Wayahudi wanyonge wanafanya nini? Je, wataweza kuurudishia ukuta wao? Je, watatoa dhabihu? Je, wataweza kumaliza kuujenga kwa siku moja? Je, wataweza kufufua mawe kutoka katika malundo ya vifusi yaliyoungua hivyo?”

3 Tobia Mwamoni, aliyekuwa upande wake akasema, “Wanachokijenga, hata kama mbweha angepanda juu yake, huo ukuta wao wa mawe angelibomoa!”

4 Ee Mungu wetu, utusikie, kwa kuwa tumedharauliwa. Warudishie matukano yao kwenye vichwa vyao wenyewe. Uwatoe ili wawe nyara katika nchi ya waliowateka.

5 Usiusitiri uovu wao wala usifute dhambi zao mbele zako, kwa kuwa wamewatukana wajenzi mbele ya macho yao.

6 Basi tuliujenga upya ukuta mpaka wote ukafikia nusu ya kimo chake, kwa kuwa watu walifanya kazi kwa moyo wote.

7 Lakini wakati Sanbalati, Tobia, Waarabu, Waamoni na watu wa Ashdodi waliposikia kuwa ukarabati wa kuta za Yerusalemu ulikuwa umeendelea na mianya ilikuwa inazibwa, walikasirika sana.

8 Wote walifanya shauri pamoja kuja kupigana dhidi ya Yerusalemu na kuchochea machafuko dhidi yake.

9 Lakini tulimwomba Mungu wetu na kuweka ulinzi mchana na usiku kupambana na tishio hili.

10 Wakati ule ule, watu wa Yuda wakasema, “Nguvu za wafanya kazi zinapungua, nacho kifusi ni kingi mno kiasi kwamba hatuwezi kuujenga upya ukuta.”

11 Pia adui zetu walisema, “Kabla hawajajua au kutuona, tutakuwa pale pale katikati yao na tutawaua na kuikomesha hiyo kazi.”

12 Kisha Wayahudi ambao waliishi karibu nao walikuja zaidi ya mara kumi na kutuambia, “Po pote mtakapoelekea, watatushambulia.”

13 Kwa hiyo nikaweka baadhi ya watu nyuma ya sehemu za chini za ukuta kwenye sehemu zilizo wazi, nikawaweka kufuatana na jamaa zao, wakiwa na panga zao, mikuki na pindi zao.

14 Baada ya kuona hali ilivyo, nikasimama na kuwaambia wakuu, maafisa na wengine wote, “Msiwaogope. Mkumbukeni Bwana, ambaye ni mkuu mwenye kuogofya. Piganeni kwa ajili ya ndugu zenu, wana wenu na binti zenu, wake zenu na nyumba zenu.”

15 Adui zetu waliposikia kwamba tumetambua hila yao na kwamba Mungu amevuruga shauri lao, sote tulirudi kwenye ukuta, kila mmoja kwenye kazi yake.

16 Kuanzia siku ile na kuendelea, nusu ya watu wangu walifanya kazi ya ujenzi na nusu nyingine wakashika mikuki, ngao, pindi na kinga ya kifuani. Maafisa walijipanga nyuma ya watu wote wa Yuda

17 waliokuwa wakijenga ukuta. Wale waliobeba vifaa vya ujenzi walifanya kazi yao kwa mkono mmoja na kushika silaha kwa mkono mwingine,

18 kila mjenzi alijifunga upanga wake upande mmoja akiwa anafanya kazi. Lakini mtu wa kupiga baragumu alikaa pamoja nami.

19 Kisha nikawaambia wakuu, maafisa na watu wengine wote, “Kazi hii ni kubwa na imeenea sehemu kubwa, nasi tumetawanyika kila mmoja yuko mbali na mwenzake juu ya ukuta.

20 Po pote mtakaposikia sauti ya baragumu, jiungeni nasi huko. Mungu wetu atatupigania!”

21 Basi tuliendelea na kazi, nusu ya watu wakishikilia mikuki, kuanzia maawio ya jua hadi nyota zilipoonekana.

22 Wakati huo pia niliwaambia watu, “Kila mtu na msaidizi wake wakae ndani ya Yerusalemu wakati wa usiku, ili waweze kutumika kama walinzi wakati wa usiku na kufanya kazi wakati wa mchana.”

23 Mimi, wala ndugu zangu, wala watu wangu, wala walinzi waliokuwa pamoja nami hatukuvua nguo zetu. Kila mmoja alikuwa na silaha yake, hata alipokwenda kuchota maji.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/NEH/4-7476571ae9dda5724d64d4fd62d031e3.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

two + sixteen =