Waebrania 1

Mwana Ni Mkuu Kuliko Malaika

1 Zamani Mungu alisema na baba zetu kwa njia ya manabii mara nyingi na kwa njia mbalimbali,

2 lakini katika siku hizi za mwisho anasema nasi kwa njia ya Mwanawe, ambaye amemweka kuwa mrithi wa vitu vyote, na ambaye kwa yeye aliuumba ulimwengu.

3 Mwana ni mng’ao wa utukufu wa Mungu na mfano halisi wa nafsi yake, akivihifadhi vitu vyote kwa neno lake lenye uweza. Akiisha kufanya utakaso kwa ajili ya dhambi, aliketi mkono wa kuume wa Ukuu huko mbinguni.

4 Kwa hiyo alifanyika bora kuliko malaika, kama jina alilorithi lilivyo bora kuliko lao.

5 Kwa maana ni malaika yupi ambaye wakati wo wote Mungu alipata kumwambia,

“Wewe ni Mwanangu;

leo mimi nimekuzaa?”

Au tena,

“Mimi nitakuwa Baba yake,

naye atakuwa Mwanangu?”

6 Tena, Mungu amletapo mzaliwa wake wa kwanza ulimwenguni, husema,

“Malaika wote wa Mungu na wamsujudu.”

7 Anenapo kuhusu malaika husema,

“Huwafanya malaika zake kuwa upepo,

watumishi wake kuwa miali ya moto.”

8 Lakini kwa habari za Mwana asema,

“Kiti chako cha enzi, Ee Mungu,

kitadumu milele na milele,

nayo haki itakuwa fimbo ya utawala

ya ufalme wako.

9 Umependa haki na kuchukia uovu;

kwa hiyo Mungu, Mungu wako,

amekuweka juu ya wenzako

kwa kukupaka mafuta ya furaha.”

10 Pia asema,

“Hapo mwanzo, Ee Bwana, uliweka misingi ya dunia,

nazo mbingu ni kazi ya mikono yako.

11 Hizo zitaangamia, lakini wewe utadumu;

zote zitachakaa kama vazi.

12 Utazikung’utakung’uta kama joho,

kama vazi zitachakaa.

Bali wewe hubadiliki,

wala miaka yako kamwe haitakoma.”

13 Je, ni kwa malaika yupi ambaye Mungu amepata kumwambia wakati wo wote,

“Wewe keti mkono wangu wa kuume

mpaka nitakapowaweka adui zako

chini ya nyayo zako”?

14 Je, malaika wote si roho watumikao waliotumwa kuwahudumia wale watakaorithi wokovu?

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/HEB/1-477941132c7f821e41229c8efd63f530.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

4 + 8 =