Waebrania 2

Wokovu Mkuu

1 Kwa hiyo, imetupasa kuwa waangalifu sana kuhusu kile tulichosikia, ili tusije tukakiacha.

2 Kwa kuwa ujumbe ulionenwa na malaika ulikuwa imara na kila uasi na kutokutii kulipata adhabu ya haki,

3 je, sisi tutapaje kupona kama tusipojali wokovu mkuu namna hii? Wokovu huu, ambao mwanzo ulitangazwa na Bwana, kisha ulithibitishwa kwetu na wale waliomsikia.

4 Pia Mungu aliushuhudia kwa ishara, maajabu na kwa miujiza mbalimbali, na karama za Roho Mtakatifu alizozigawa kulingana na mapenzi yake.

Yesu Alifananishwa Na Ndugu Zake

5 Mungu hakuuweka ulimwengu ujao ambao tunanena habari zake chini ya malaika.

6 Lakini kuna mahali mtu fulani ameshuhudia akisema:

“Mwanadamu ni kitu gani hata umfikirie,

mwana wa mwanadamu ni nani hata umjali?

7 Umemfanya kuwa chini kidogo kuliko malaika;

umemvika taji ya utukufu na heshima,

8 nawe umeweka vitu vyote chini ya miguu yake.”

Kwa kuweka vitu vyote chini yake, Mungu hakuacha kitu cho chote ambacho hakukiweka chini ya mwanadamu. Lakini kwa sasa, hatuoni kwamba kila kitu kiko chini yake.

9 Lakini twamwona Yesu, aliyefanywa chini kidogo kuliko malaika, sasa akiwa amevikwa taji ya utukufu na heshima kwa sababu alistahimili mauti, ili kwamba kwa neema ya Mungu apate kuonja mauti kwa ajili ya kila mtu.

10 Ili kuwaleta wana wengi katika utukufu, ilimpendeza Mungu, kwa ajili yake na kwa kupitia yeye kila kitu kilichopo, kumkamilisha mwanzilishi wa wokovu wao kwa njia ya mateso.

11 Yeye awafanyaye watu kuwa watakatifu na wale ambao hufanywa watakatifu, wote hutoka katika jamaa moja. Hivyo Yesu haoni aibu kuwaita ndugu zake.

12 Yeye husema,

“Nitalitangaza jina lako kwa ndugu zangu;

mbele ya kusanyiko nitaimba sifa zako.”

13 Tena,

“Nitaweka tumaini langu kwake.”

Tena anasema,

“Niko hapa, mimi pamoja na watoto Mungu alionipa.”

14 Basi kwa kuwa watoto wana nyama na damu, yeye pia alishiriki katika ubinadamu wao, ili kwa kifo chake, apate kumwangamiza huyo mwenye nguvu za mauti, yaani, Shetani,

15 na kuwaweka huru wale waliokuwa utumwani maisha yao yote kwa sababu ya kuogopa mauti.

16 Kwa kuwa ni dhahiri kwamba hakuja kusaidia malaika, bali uzao wa Abrahamu.

17 Kwa sababu hii ilibidi afanane na ndugu zake kwa kila hali, ili apate kuwa Kuhani Mkuu mwenye huruma na mwaminifu katika kumtumikia Mungu, ili pia apate kufanya upatanisho kwa ajili ya dhambi za watu.

18 Kwa kuwa yeye mwenyewe aliteswa alipojaribiwa, aweza kuwasaidia wale wanaojaribiwa.

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/HEB/2-78e98b66fd5465ac246ee7a9922b7933.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

twenty + 20 =