Yeremia 6

Yerusalemu Imezingirwa Na Jeshi

1 “Kimbieni kwa usalama wenu, enyi watu wa Benyamini!

Kimbieni kutoka Yerusalemu!

Pigeni tarumbeta katika Tekoa!

Inueni ishara juu ya Beth-Hakeremu!

Kwa kuwa maafa yanaonekana yakitoka kaskazini

na uharibifu wa kutisha.

2 Nitamwangamiza Binti Sayuni,

aliye mzuri sana na mororo.

3 Wachungaji pamoja na makundi yao ya kondoo

na mbuzi watakuja dhidi yake;

watapiga mahema yao kumzunguka,

kila mmoja akichunga kundi lake mwenyewe.”

4 “Jiandaeni kwa vita dhidi yake!

Inukeni na tumshambulie mchana!

Lakini, ole wetu, mchana unaisha

na vivuli vya jioni vinazidi kuwa virefu.

5 Kwa hiyo inukeni, tufanye mashambulizi usiku

na kuharibu ngome zake!”

6 Hivi ndivyo asemavyoBwanaMwenye Nguvu Zote:

“Kateni miti mjenge boma

kuzunguka Yerusalemu.

Mji huu ni lazima uadhibiwe,

umejazwa na uonevu.

7 Kama vile kisima kinavyomwaga maji yake,

ndivyo anavyomwaga uovu wake.

Ukatili na maangamizi yasikika ndani yake,

ugonjwa wake na majeraha yake

viko mbele yangu daima.

8 Pokea onyo, Ee Yerusalemu,

la sivyo nitageukia mbali nawe

na kuifanya nchi yako kuwa ukiwa

asiweze mtu kuishi ndani yake.”

9 Hivi ndivyo asemavyoBwanaMwenye Nguvu Zote:

“Wao na wayakusanye mabaki ya Israeli

kwa uangalifu kama kwenye mzabibu;

pitisha mkono wako kwenye matawi tena,

kama yeye avunaye zabibu.”

10 Niseme na nani na kumpa onyo?

Ni nani atakayenisikiliza mimi?

# Masikio yao yameziba

kwa hiyo hawawezi kusikia.

Neno laBwanani chukizo kwao,

hawalifurahii.

11 Lakini nimejaa ghadhabu yaBwana,

nami siwezi kuizuia.

“Wamwagie watoto walioko barabarani,

na juu ya vijana waume

waliokusanyika pamoja;

mume na mke watakumbwa kwa pamoja ndani yake,

hata nao wazee waliolemewa na miaka.

12 Nyumba zao watapewa watu wengine,

pamoja na mashamba yao na wake zao,

nitakapounyosha mkono wangu

dhidi ya wale waishio katika nchi,”

asemaBwana.

13 “Kuanzia aliye mdogo kabisa hadi mkubwa kabisa,

wote wanatamani kupata faida isiyo halali;

makuhani na manabii wanafanana,

wote wanafanya udanganyifu.

14 Hufunga majeraha ya watu wangu

kama vile hawakuumia sana.

Husema, ‘Amani, amani,’

wakati hakuna amani.

15 Je, wanaona aibu kwa ajili ya tabia yao

inayochukiza mno?

Hapana, hawana aibu hata kidogo;

hawajui hata kuona haya.

Kwa hiyo wataanguka miongoni mwa hao walioanguka,

watashushwa nitakapowaadhibu,”

asemaBwana.

16 Hivi ndivyo asemavyoBwana:

“Simama kwenye njia panda utazame,

ulizia mapito ya zamani,

ulizia wapi ilipo njia nzuri, uifuate hiyo,

nanyi mtapata raha nafsini mwenu.

Lakini ninyi mlisema, ‘Hatutaipita hiyo.’

17 Niliweka walinzi juu yenu na kusema,

‘Sikieni sauti ya tarumbeta!’

Lakini mkasema, ‘Hatutasikiliza.’

18 Kwa hiyo sikilizeni, Enyi mataifa,

angalieni, Enyi mashahidi,

lile litakalowatokea.

19 Sikia Ee nchi:

Ninaleta maafa juu ya watu hawa,

matunda ya mipango yao,

kwa sababu hawakusikiliza maneno yangu

na wameikataa sheria yangu.

20 Wanifaa nini uvumba kutoka Sheba

au udi wa harufu nzuri kutoka nchi ya mbali?

Sadaka zako za kuteketezwa hazikubaliki,

dhabihu zako hazinifurahishi mimi.”

21 Kwa hiyo hivi ndivyo asemavyoBwana:

“Nitawawekea vikwazo mbele ya watu hawa.

Baba na wana wao watajikwaa juu yake,

majirani na marafiki wataangamia.”

22 Hivi ndivyo asemavyoBwana:

“Tazama, jeshi linakuja

kutoka nchi ya kaskazini,

taifa kubwa linaamshwa

kutoka miisho ya dunia.

23 Wamejifunga pinde na mkuki,

ni wakatili na hawana huruma.

Wanatoa sauti kama bahari inayonguruma

wanapokuwa wamepanda farasi zao,

wanakuja kama watu walioandaliwa tayari kwa vita

kukushambulia wewe, Ee Binti Sayuni.”

24 Tumesikia taarifa zao,

nayo mikono yetu imelegea.

Uchungu umetushika,

maumivu kama mwanamke

mwenye utungu wa kuzaa.

25 Usitoke kwenda mashambani

au kutembea barabarani,

kwa kuwa adui ana upanga

na kuna vitisho kila upande.

26 Enyi watu wangu, vaeni magunia

mjivingirishe kwenye majivu,

ombolezeni kwa kilio cha uchungu

kama amliliaye mwana pekee,

kwa maana ghafula

mharabu atatujia.

27 “Nimekufanya wewe kuwa kitu cha kujaribu chuma

na watu wangu kama mawe yenye madini,

ili upate kuzijua na kuzijaribu njia zao.

28 Wote ni waasi sugu,

wakienda huko na huko kusengenya.

Wao ni shaba na chuma,

wote wanatenda kwa upotovu.

29 Mivuo inavuma kwa nguvu,

kinachoungua kwa huo moto ni risasi,

lakini pamoja na kusafisha kote huku ni bure;

waovu hawaondolewi.

30 Wanaitwa fedha iliyokataliwa,

kwa sababuBwanaamewakataa.”

—https://d1b84921e69nmq.cloudfront.net/337/32k/JER/6-e49680ec34ceddf994d47cedcf5c68f0.mp3?version_id=1627—

Leave a comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *

16 − 8 =